Askofu Chengula: Wafarijini wagonjwa

WAAMINI Wakatoliki wametakiwa kuwahudumia wagonjwa kwa moyo wote, kuwafariji na kutambua uwepo wa Kristo ndani ya wagonjwa hao wanaowahudumia.
Hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Mbeya, Mhashamu Evarist Chengula wakati akitoa Homilia katika Adhimisho la Ibada ya Misa Takatifu ya Wagonjwa iliyofanyika katika Kanisa la Roho Mtakatifu, Parokia ya Ruanda, Jimbo Katoliki Mbeya.
Katika ibada hiyo, Askofu Chengula amesema watu wote wanatakiwa kuwatunza wagonjwa huku wakiamini wanambeba Kristo, maana kutofanya hivyo kunasababisha wagonjwa kujiona wamekataliwa na ulimwengu huku wakikata tamaa na kuhusisha magonjwa na imani za kishirikina, jambo linalosababisha chuki na uongo kwa binadamu.
Amesema wagonjwa ni kielelezo  cha upendo  wa Kristo  kushirikishwa katika mateso ya Yesu, hivyo wanapaswa wajiweke mikononi mwa Mama Bikira Maria  maana kwa mateso wayapatayo ni ukombozi  kwao kwakuwa Yesu Kristo ni Mganga.
“Kutembelea Wagonjwa ni njia mojawapo ya kuwarejesha kutoka katika mawazo ya kuwekwa pembezoni mwa jamii, na baadhi ya wagonjwa wengine wanapona kabisa kutokana na imani zao, huku wakijiona sawa sawa na wasio wagonjwa kutokana na faraja kutoka kwa ndugu jamaa na marafiki.” Amesema Askofu Chengula.
Ikumbukwe kuwa kila mwaka tarehe 11 Februari Kanisa Katoliki huadhimisha kumbukumbu ya Bikira Maria Mama  wa Lurdi, ambapo siku hiyo pia iliteuliwa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili (ii) kuwa mahususi kwa ajili ya kuwaombea wagonjwa, kwani wagonjwa wengi wanaoenda Hija Lurdi wanapata uponyaji.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU