Jimbo Kuu Tabora lafungua jubilei miaka 100 ya upadri


ASKOFU Mkuu Paulo Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora amezindua Jubilei ya Miaka 100 ya Upadri ngazi ya Jimbo na kuwasihi waamini  kuwaombea mapadri ili watekeleze majukumu yao kwa hekima na unyenyekevu.

Ufunguzi wa Jubilei hiyo umefanyika hivi karibuni katika Kanisa Kuu la jimbo hilo huku Askofu Mkuu Ruzoka akisisitiza kuwa, upadri si kazi nyepesi na ni maisha yanayohitaji sala na imani thabiti kwa Mungu. Hivyo ni vyema mapadri wakazidi kuomba kuongezewa imani ili wadumu katika maisha hayo ya kumtumikia Mungu na kuinjilisha kama walivyofanya wamisionari wa Kwanza.

“Maisha ya Upadri si lelemama! zipo changamoto mbalimbali ambazo mapadri wanakutana nazo. Changamoto hizo mtaendelea kukutana nazo lakini jambo la msingi ni kuzikabidhi kwa Kristo aliye asili ya wito wenu ili apambane nazo. Hizo ndizo dhoruba walizokutana nazo wafuasi wa Kristo wakiwa safarini na Kristo mwenyewe akazituliza .

Hivyo ninawasihi mapadri  kumuomba Mungu daima awajalie fadhila ya Hekima kama ile ya Sulemani. Hekima iliyomsaidia kuliongoza Taifa Teule la Israel. Mkumbuke kuwa pale Taifa la Israeli lilipomsahau Mungu na kufanya yao, lilisambaratika, kadhalika padri naye asipomtegemea Mungu katika utume wake hawezi kufanikiwa hata mara moja,” amesema Askofu Mkuu Ruzoka.

Aidha amewakumbusha wazazi wajibu wao wa kuwalea vema watoto wao na kuwaandaa ili wapende maisha ya upadri na utawa. Kamwe wazazi wasiwazuie watoto wao kuingia maisha ya miito mitakatifu kwa ajili ya kumtumikia Mungu na Taifa lake.


Wito pia ulitolewa kwa waamini wote kutunza Imani iliyokwisha pandwa katika mioyo yao na Kristo mwenyewe kwa njia ya Sakramenti za Kanisa kupitia mapadri.
Amesisitiza; “Kumpata padri mmoja ni zaidi ya kuongoa watu elfu Kumi, hii yote ni kusema  kuwa, padri kwa nafasi yake ndiye muadhimishaji wa matakatifu ya Mungu kwa ajili  ya kuwapeleka watu wengi kwa Kristo kwa njia ya Masakrameni na mafundisho yake. 
Hivyo mapadri wanapaswa kutunza zawadi hiyo waliyopewa na Mungu, kwani palipo na padri kuna Ekalisti Takatifu, na penye Ekaristi Takatifu pana padri.”


Katika Adhimisho hilo pia waamini wote wamealikwa kuwaombea Mapadri wa Kwanza katika Jimbo hilo Kuu la Tabora ambao sasa ni marehemu, yaani Pd. Raphael Kavula, Pd. Simon Makulumo, na Pd. Philipo Luziga wote waliopadirishwa Agosti mwaka  1928 na Mjumbe wa Baba Mtakatifu Arthur Hinsley.


Jubilei hizi pacha yaani ya miaka 150 ya Uinjilishaji na miaka 100 ya Upadri Tanzania Bara zilizinduliwa kitaifa Oktoba Mosi mwaka 2016 katika Jimbo Katoliki  Bukoba na Majimbo yanaendelea kuzindua Jibilei hizo katika ngazi ya majimbo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU