‘Kanisa siyo mshindani, ni mtumishi’ Ask. Ngalalekumtwa

RAIS wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amesema kuwa Kanisa halina wazo lolote la ushindani katika utoaji wa huduma zake, bali linafanya hayo yote kwa kuwa huo ni utume na wito wake.
Ameeleza hayo katika maadhimisho ya jubilei ya miaka 25 ya Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii nchini (CSSC), yaliyofanyika jijini Dar es salaam, na kubainisha kuwa Kanisa linatumia rasilimali zake kwa ajili ya ustawi wa taifa na watu wake.
“Kanisa siyo mfanya biashara, na siyo mshindani ila ni mtumishi. Kanisa linaendelea kutoa huduma bora ikiwemo elimu bora na siyo bora elimu, afya na kuwatunza wenye dhiki. Hatuna nia ya kuingia ushindani, tunatumia rasilimali zetu kwa ajili ya taifa letu ili liwe lenye heshima, utu na ustawi” ameeleza Askofu Ngalalekumtwa ambaye pia ni Makamu wa Rais wa CSSC.
Kauli hiyo imeungwa mkono na Rais wa CSSC Askofu Alex Malasusa aliyeweka wazi kwamba makanisa hayatoi huduma za afya na elimu kwa ajili ya kupata faida kiuchumi.
Amesema kuwa makanisa yanajikita katika utoaji wa huduma hizo ikiwa ni sehemu ya wito wake na kwamba hakuna dhamira yoyote ya kujitafutia utajiri kupitia huduma hizo.
Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Askofu Frederick Shoo amesema kuwa CSSC  itaendelea kutoa huduma za jamii na kamwe hawaruhusiwi kuacha wito huo kwani ni sehemu ya utume wao.
Aidha ameongeza kuwa wanahitaji roho ya ushirikiano, roho ya kujitoa kama waliyokuwa nayo waasisi w tume hiyo katika kuwahudumia wanadamu.
“Tunajivunia miaka 25 ya utoaji huduma za jamii, licha ya kukutana na changamoto kadhaa, tunajua changamoto hizo ni fursa kwetu. Tutaendelea kuweka utambulisho katika utoaji wa huduma kama wafuasi wa kristo: yaani upendo, huruma na uadilifu” ameeleza.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU