Kardinali atahadharisha chuki za kidini



θ Asema Kanisa Katoliki halistawi kwa ruzuku za serikali

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo ameonya dhidi ya uzushi wa baadhi ya watu kuwa ruzuku toka serikalini ndizo kichocheo cha maendeleo ya Kanisa hilo.
Akizungumza na gazeti Kiongozi Kardinali Pengo  amesema kuwa, hizo ni chokochoko za wasiolitakia mema Kanisa na kwamba zisipokemewa kwa dhati zinaweza kusababisha chuki za kidini jambo ambalo ni hatari katika jamii.
 “Mimi sina kubwa la kusema ila ninawaambia watu hawa kuwa, wachunguze kwanza kabla ya kusema, hakuna ukweli wowote juu ya Kanisa Katoliki eti linasaidiwa na Serikali na haya ndiyo yanayoleta chokochoko na chuki za kidini baadaye,” amesema Kardinali Pengo.
Ameongeza kuwa, kuna vitu vingi ambavyo vinazungumzwa mtaani juu ya Kanisa Katoliki na kuanza kuamsha chuki, baina ya wale wenye uelewa mdogo kuwa Kanisa Katoliki linapewa fedha na Serikali kitu ambacho si kweli.
Kardinali Pengo ameendelea kusema kuwa Kanisa Katoliki lina vyanzo vyake vingi vya kupata fedha ikiwemo sadaka za waamini, ambazo ndizo zimekuwa chachu ya kuendelea kwake na kuwa kila nchi hapa duniani Kanisa limekuwa likijiendesha lenyewe pasipo kutegemeana.
“Kanisa lina miradi chungu nzima  zikiwemo  shule na hospitali, ambazo zimekuwa zikiingiza fedha na kulisaidia Kanisa kukua na kujitegemea pasipo kutegemea chochote, wanaodai kuwa tunapewa ruzuku na Serikali si wakweli wachunguze, sio kukaa na kuzungumza vitu vya uongo”amesema Kardinali Pengo.
Ameendelea kusema kuwa Kanisa Katoliki halijawahi kupata fedha wala kwenda kuomba msaada serikalini ili kuendesha shughuli zake za uinjilishaji ila watu wasiokuwa na mapenzi mema na Kanisa hilo wamezusha taarifa hizo hewa ndiyo chanzo cha kusambaa kwa chuki ambapo baadhi ya watu wa madhehebu mengine wataamini kitu ambacho si cha kweli.
Aidha Kardinali Pengo amewataka waamini wa kanisa hilo kuendelea kusali na kuwaombea kwa Mungu watu wanaozusha taarifa za uongo  ili wawe na ufahamu wa mambo wajue na kulitambua kanisa katoliki na kuwa wajinze jinsi kanisa hilo linavyojiendesha ili nao wapeleke neema hiyo katika madhehebu yao waweze kuendelea kama kanisa katoliki lilivyoendelea.
Mbali na hilo Kardinali Pengo ametumia fursa hiyo kuendelea kuwatia moyo watu kuvumilia hali ngumu ya maisha yaliyopo sasa kwa kuwa ugumu huo wa maisha ndiyo njia ya kufikia mafanikio.
Amewataka kuacha kulalamikia kitendo cha rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Magufuli kununua ndege na kuanza kwa mchakato wake wa kujenga uwanja wa ndege wa kimataifa huko Chato Mkoani Geita kwa kuwa nalo ni jambo jema.
Amesema ili kufikia mafanikio ni lazima kupitia magumu kwa kuwa kila safari ina changamoto zake na kwa changamoto hizo ni lazima wananchi wafunge mikanda ili kuimaliza amewataka kumuombea rais Magufuli ili kumaliza changamoto hizo na si kumlaumu.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU