Kanisa kujenga mwelekeo mpya wa vijana duniani

Kanisa Katoliki linatarajia kufanya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana, ambayo itatoa mwelekeo mpya wa vijana wa kizazi kipya, kutafakari na kufanyia kazi changamoto zinazowakabili vijana ulimwenguni.

Akiongea na Kiongozi ofisini kwake, Mratibu wa Vijana Taifa katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Liberatus Kadio ameeleza kuwa sinodi hiyo itakuwa ni fursa kwa maaskofu kujadili hali ya vijana ulimwenguni kwa kuangazia maisha yao kimaadili na kiroho.
Aidha Padri Kadio ametaja baadhi ya changamoto zinazowakabili vijana kuwa ni pamoja na hali ya kutojaliana, kupungua kwa idadi ya watoto wanaozaliwa, ubaguzi, ukosefu wa ajira, ukimbizi na uhamiaji na uharibifu wa mazingira.

“Kwa kutambua kuwa dunia inabadilika kwa kasi mno, Maaskofu watakutana kuweka mikakati na sera za kichungaji ili kujenga kizazi kipya chenye mwelekeo mpya. Hivyo watatathmini mambo yanayoathiri ujenzi wa kizazi kipya, kwa kutambua kuwa vijana ni wadau wakuu katika mchakato wa mageuzi ya kijamii hivyo hawatakiwi kukosa dira sahihi” amebainisha Padri Kadio.

Ameongeza kuwa sinodi hiyo inalenga kuwasaidia vijana ili wapate utimilifu wa maisha wakitambua kuwa maisha na imani ni zawadi ya Mungu. Amegusia mambo makuu yatakayopewa kipaumbele katika mjadala huo ambayo pia yamebeba kaulimbiu kuwa ni imani na mang’amuzi ya wito, na kuwataka vijana kutambua, kutafsiri na kuchagua kile ambacho Mungu anakitaka katika maisha ya kijana.

“Imani iwasaidie vijana kujenga na kudumisha umoja katika kuishi maisha ya kiroho na kiutu. Lazima vijana wawe na maamuzi sahihi na wasome alama za nyakati na kutambua uwepo wa Roho Mtakatifu katika historia. Aidha katika mang’amuzi ya wito vijana wawe tayari kupokea utume kwa uchaji, ari na moyo mkuu. Wawe tayari kuchukua msalaba na kuubeba vema wakimfuata Kristo” ameeleza.

Sinodi ya Maaskofu kwa vijana itafanyika Oktoba 2018 na kuongozwa na mada isemayo “Vijana, imani na mang’amuzi ya wito”.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU