“Msiogope gharama kuwapa watoto elimu bora” Askofu Amani

Askofu wa jimbo Katoliki Moshi  Mhashamu Isaac Amani ametoa wito kwa waamini na jamii  kwa  ujumla kuhakikisha  wanawapeleka watoto shule na wasiogope gharama katika kwa sababu elimu  bora ina gharama.
Askofu Amani ambaye pia ni msimamizi wa kiti cha Askofu wa Jimbo Katoliki Mbulu ametoa wito huo alipokuwa akizindua rasmi shule ya sekondari ya wasichana ya Michaud  ambayo  ni ya  bweni iliyopo Karatu Jimboni Mbulu na kuitaka jamii isiogope gharama katika kuwasomesha watoto kwa faida ya taifa.
Akihubiri katika misa ya uzinduzi wa sekondari hiyo inayomilikiwa na Masista wa Shirika la Mabinti wa Maria  amesema elimu bora ina gharama na kuwataka waumini na jamii kwa ujumla kuwekeza kwenye elimu kwa kuwasomesha watoto wao.
Askofu Amani amesema ili dunia na taifa liende mbele lazima uwekezaji ufanyike  kwenye elimu ambayo ni ufunguo wa dunia na mwanga wa ulimwengu na kuitaka jamii na waumini kuhakikisha wanawasomesha watoto ili wawe wataalamu na viongozi wazuri wa  taifa hapo baadaye.
“Elimu hutenda miujiza  kwa  mtu aliyesoma lazima tusomeshe watoto wetu na kuwaandaa kuja kuwa wataalamu mbalimbali na viongozi wa kesho  katika kulitumikia kanisa na taifa letu hapo baadaye,” amesema
Askofu Amani amesema elimu humwandaa mtoto kuwa mzalendo kwa taifa hivyo lazima uwekezaji  kwenye suala hilo lenye tija kubwa ambalo pia huwaandaa  wahudumu wazuri wa kiroho, mapadri, watawa na walei ndani ya Kanisa.
Amesema mtu akiwa msomi  humfanya  kutambua thamani ya watu na utu wa wengine  kwa kuishi nao kwa furaha, upatano, msamaha na wenye kumtumainia Mungu na kuwataka waumini wasiogope kuwapeleka shule watoto kwa faida ya maisha yao ya baadaye katika dunia hii ya sayansi na teknolojia.
Amewaasa pia wanafunzi wajitahidi  kusoma sana masomo ya sayansi na waachane na hofu na woga  kuhusu  kulisoma somo hilo  kwa faida ya taifa ili liweze  kupata wataalamu  katika kada  mbalimbali za kuwatumikia watu kiroho na kimwili.
Akisoma risala Sista Catherine Kabula amesema shule hiyo yenye usajili namba S .4970 imeanza rasmi mwaka 2016 na inafundisha masomo ya sayansi, sanaa, TEHAMA na kuitaka jamii kuchangamkia fursa hiyo  kwa kuwapeleka watoto hapo ili wapate elimu bora.
Naye Mama mkuu wa shirika la Mabinti wa Maria, Sista Theresia Sungi amesema kwa kufahamu umuhimu wa elimu katika dunia hii  wameamua kuweka kipaumbele kwenye suala hilo lengo likiwa kuisaidia jamii na kutoa wito kwa wazazi na walezi  kuwapeleka watoto wao katika shule za Kanisa ambazo zimekuwa zikitoa elimu bora na malezi mema ya kiroho na kimwili.
Mkuu wa wilaya ya Karatu, Bi.Theresia Mhongo amelipongeza  Kanisa Katoliki  kuwa limekuwa likifanya kazi nzuri  kwenye huduma za jamii  katika sekta za afya, elimu, maji na kuwashukuru Shirika la Masista wa Mabinti wa Maria kwa kuwekeza kwenye  jambo la elimu kwa sababu wilaya hiyo  inakabiliwa na changamoto nyingi ya uhaba wa shule za sekondari  miongoni mwa jamii.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU