Upungufu wa chakula waathiri watumiaji wa ARV Bunda

IMEELEZWA kuwa hali ya upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo nchini imeathiri upatikanaji wa chakula cha uhakika katika kaya, huku wilayani Bunda hali hiyo ikipelekea watumiaji wa dawa za kupunguza makali ya Virusi vya Ukimwi (ARV) kushindwa kutumia dawa hizo ipasavyo kutokana na kutokuwa na uhakika wa chakula.
Hayo yamebainishwa hivi karibuni na watumiaji hao walipotembelewa na timu inayoratibu vikundi vya ujasiriamali vinavyosimamiwa na Ushirikiano wa Dini mbalimbali nchini (TIP), kupitia Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) ambapo asilimia kubwa ya vikundi hivyo vinaundwa na watu wanaoishi na virusi vya ukimwi.
Akielezea baadhi ya changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza mradi huo, mmoja wa wajumbe wa kikundi cha Tupendane kilichopo katika kijiji cha Kabasa wilayani Bunda, Bi Esta Maduka amesema kuwa hali ya ukosefu wa mvua kwa muda mrefu katika eneo hilo imepelekea upungufu wa chakula na hivyo kuathiri matumizi sahihi ya dawa hizo za ARV.
“Kuna upungufu mkubwa wa chakula katika kijiji chetu, bei ya mahindi inapanda kila siku na kwa sasa tunanunua mahindi kwa bei ya Shilingi 4500 kwa sado moja. Hali hii inatuathiri sisi tunaoishi na VVU kwani inaathiri ufuasi mzuri wa dawa” ameeleza.
Aidha wajumbe hao wameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kusaidiwa chakula hasa kwa wanaotumia ARV ili waendelee kufuata dozi na kustawisha afya zao.
Katika hatua nyingine wajumbe hao wameupongeza mradi wa TIP kupitia TEC ambao umewawezesha kumudu mahitaji ya maisha yao ya kila siku, huku wengine wakiendesha biashara kutokana na mikopo na akiba wanazojiwekea katika vikundi vyao.
Moja ya faida zinazotajwa na wanakikundi hao kutokana na uwepo wa mradi huo ni pamoja na kupata elimu sahihi inayowawezesha kujikinga na maambukizi mapya ya VVU na matumizi sahihi ya ARV, huku uwepo wao ukitwajwa kusaidia kupunguza unyanyapaa kwa kiasi kikubwa.
“Kikundi kimetusaidia kuwaibua wagonjwa wapya majumbani na kuwaandikia rufaa, kutoa elimu ya lishe bora, kutoa ushauri na kuwatembelea wagonjwa majumbani pamoja na yatima. Pia kikundi kimekuwa chachu ya kuendesha maisha yetu kwani kinatusaidia kupata fedha za kukidhi mahitaji yetu ya kila siku” amesema Julius Manyama.
Naye mjumbe mwingine Musa Mgetu ameweka wazi kuwa mradi huo umemuwezesha kuanzisha biashara ya kuuza bidhaa mbalimbali mgodini, kuendesha shughuli za uchimbaji mdogo wa madini, na kumpatia faida lukuki ikiwa ni pamoja na kumuwezesha kununua ng’ombe wawili.
Kwa upande wake Mratibu wa mradi huo kutoka TEC, Norasco Tereba ameeleza kuwa nia ya mradi huo ni kuwajengea wananchi uwezo na mbinu za kukabiliana na changamoto mbalimbali za maisha, kuwajengea uelewa kuhusu matumizi sahihi ya ARV na umuhimu wa kuzingatia lishe kwa watu wanaoishi na VVU.
“Lengo la mradi ni kuwawezesha watu waliojiunga katika vikundi wapewe mbinu na mafunzo yatakayowasaidia kuendesha maisha yao. Tunalenga kuwajengea uwezo kwa kuwapa ujuzi na elimu ambayo watabaki nayo hata pale wafadhili watakapoondoka” amesema.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU