“Simamieni ukweli” Askofu Kimaryo awaasa mapadri

MAPADRI wametakiwa kuwa wakweli katika kila jambo watendalo ili kuwakomboa wanyonge na wahitaji kutoka katika hali mbaya kimaisha na kiroho.
Askofu wa Jimbo Katoliki Same Mhashamu Rogarth Kimaryo ametoa rai hiyo katika Misa Takatifu ya uzinduzi wa Jubilei ya miaka 100 ya upadri Tanzania Bara katika Jimbo hilo.
“Mapadri lazima muuige mfano wa Nabii Yeremia aliyeitwa na Mwenyezi Mungu na kupewa majukumu yaliyomfanya akabiliane na wafalme, wakuu, makuhani na watu wa mamlaka akitetea ukweli hata kutaka kukatwa kichwa, lakini alisimamia alichotumwa na Mwenyezi Mungu na kukitimiza,” amesema Askofu Kimaryo
Amesema mapadri wametumwa na Mungu ili kuutumikia wito kwa kuwatetea wanyonge na kujitenga na faida na tamaa za kidunia ambazo zitawaingiza katika matatizo makubwa, hivyo wanatakiwa kuyaishi mafunzo ya Kanisa tu.
“Hapa duniani mmeteuliwa kuwasaidia wahitaji tu kiroho, siyo kuzitumia elimu zenu kubwa na talanta kujitajirisha, hayo mngeyapata kirahisi nje ya wito wa kipadri, mkiyazingatia haya mtaungana nami pamoja na viongozi wa Kanisa Katoliki kujihakikishia faida pekee tutakayoikuta mbinguni,”
Akiirejea hati ya Baba Mtakatifu Fransisko juu ya mazingira “LAUDATO SI”, amewataka mapadri kukaa pamoja na jamii na kusaidia kuyalinda mazingira kwa kupanda miti mingi na kuhifadhi uoto wa asili kwani mazingira ni uhai.
“Serikali inafanya jitihada kubwa kuhamasisha uhifadhi mazingira, tunatakiwa kuiunga mkono kuhifadhi mazingira kwa kuotesha miti mingi, kuhifadhi vizuri mazingira yanayotuzunguka, kukaa pamoja na kujadili mbinu mbadala ya kuzuia uchomaji mikaa, ukataji miti na kutoishia kutoa matamko tu kwa wanaoharibu mazingira”.
Pia Askofu Kimaryo ameitaka jamii kuisoma na kuizingatia hati ya Baba Mtakatifu juu ya Ndoa “AMORIS LAETITIA” kwani ina mchango mkubwa katika kuzilinda familia.
“Ndoa imara na tamu inapimwa katika maeneo mbalimbali ya kimsingi ambayo ni upendo wa kweli, msamaha na uvumilivu, endapo mtazingatia haya kama yalivyoainishwa katika hati ya Baba Mtakatifu ndoa zenu zitadumu milele,” amesisitiza
Akiongelea miaka 100 ya upadri katika Jimbo la Same ambapo padri wa kwanza mzalendo alipata daraja hilo mwaka 1937, Askofu Kimaryo amesema kazi haikuwa rahisi mtu mweusi kupewa daraja hilo kutokana na sababu nyingi za kipindi hicho hasa ikizngatiwa kuwa nchi ilikuwa haijapata uhuru.
Amewapongeza Maaskofu watangulizi katika Jimbo hilo, mapadri, watawa walio hai na waliotangulia mbele ya haki kutokana na jitihada zao ambazo zimesababisha Jimbo kukua.
Hata hivyo ameitaka jamii kuwaombea Maaskofu, mapadri, watawa na viongozi wengine wa kidini kwani wao si wakamilifu ili waeneze injili kwa watu wengi zaidi.
Mapadri wazalendo wanne wa kwanza jimboni Same ni pamoja na Padri Andrea Kivaria, Padri Leonard Kiure(1951), Padri Phocas Abedi(1961) na Padri Sabbas Msuya(1961)


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU