‘Makanisa yataiwezesha Tanzania ya viwanda’ Dkt. Kigwangala

KATIKA kuelekea uchumi wa viwanda nchini makanisa yametajwa kuwa mdau muhimu katika kufanikisha adhma hiyo, kwa jinsi yalivyoweka kipaumbele kwa utoaji huduma katika sekta za afya, elimu, sayansi na teknolojia.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamisi Kigwangala katika maadhimisho ya jubilei ya miaka 25 ya Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii nchini (CSSC), yaliyofanyika jijini Dar es salaam hivi karibuni na kuhudhuriwa na mamia ya wajumbe.
Dkt. Kigwangala ameeleza kuwa Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii imekua mdau muhimu katika kuratibu na kusimamia huduma za jamii hapa nchini, hususani huduma za elimu na afya, na hivyo kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi nchini.
“Kama mnavyofahamu, nchi yetu iko kwenye mpango wa kuelekea kwenye uchumi wa viwanda, lengo hili litafikiwa tu iwapo nchi yetu itakuwa na watu wenye afya bora na elimu ya kutosha ambao wataweza kushiriki kikamilifu na kutoa mchango wao katika kufanikisha adhma hii kwa kufanya kazi kwa bidii na weledi” ameeleza.
Aidha Dkt. Kigwangala ameeleza kuwa nchi haiwezi kuendelea kama watu wake wanasumbuliwa na maradhi, ujinga na umasikini, na hivyo kuipongeza CSSC kwa kuwa mdau muhimu katika kupambana na maradhi, ujinga na umasikini.
Kwa upande wake Rais wa CSSC, Askofu Dkt. Alex Malasusa ameeleza kuwa tume hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali kwa lengo la kuleta amani kwa watanzania wote, kwa kupeleka huduma muhimu kwa kila kiumbe bila kujali rangi, kabila au dini.
“Kanisa kwa maana ya madhehebu yote yaliyo mwanachama wa CSSC yataendelea kutoa huduma hii muhimu, huu ndiyo wito wetu. Tunapofanya kazi hizi kwetu ni sehemu ya ibada, na kutokufanya ni kukiuka hali ya kutoa upendo wa Mungu kwa wanaohitaji” ameeleza Askofu Malasusa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa CSSC, Peter Maduki ametaja mafanikio yaliyofikiwa na tume hiyo kuwa ni pamoja na kuboresha mfumo wa elimu, kupanua na kuboresha utoaji huduma za afya huku ubia katika huduma za afya unaimarishwa.

Mpaka sasa tume inazo taasisi za elimu zaidi ya 1000 zikijumuisha shule na vituo vya kutolea elimu. Kwa upande wa afya tume ina vituo vya afya vipatavyo 900, ikiwa ni pamoja na hospitali 102, vituo vya afya 102 na zahanati 696.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU