Walionusurika kifo mgodini Geita waapa kumrudia Mungu

·     
Watoa siri uchimbaji dhahabu, walivyozama na kuokolewa
·      Waanza kushuhudia Habari Njema kwa wengine


“TUMEMUONA Mungu kwa namna ya ajabu sana ambayo hailezeki kwa ufasaha. Ametutendea makuu tukiwa shimoni kwa muda wa siku tano. Tuna deni kubwa kwake maana tusipomjua na kumwelekea ni sawa na kujitenga naye” ni kauli ya mmoja watu 15 walionusurika baada ya kuzama  katika mgodi wa RZU.

Wahanga hao 15 walifukiwa na kifusi na kukaa shimoni kwa muda siku 4 na kuokolewa siku ya tano wakiwa salama na hivyo kuibua shangwe kwa wakazi wa eneo hilo waliokusanyika kushuhudia jitihada za uokoaji huo, huku wahanga hao wakimtaja Mungu kama mwokozi wao.

Mmoja wa Wahanga hao Anicet Masanja amesema kuwa yeye binafsi alikuwa mbali na masuala ya Mungu lakini katika tukio hilo amekiri kuwa ameuona wema wa Mungu kwao na kuahidi kujiwekea mazingira ya kuwa karibu na Mungu wa kuhakikisha anasali kila mara.

"Mimi nilikua mbali na masuala ya Mungu lakini ukweli usiofichika ni kwamba mkono wa Mungu kwetu umeonekana bila kificho. Kweli Mungu ni mwaminifu na ana huruma na watu wake japo tunamfanyia maasi kila mara, mimi mwenyewe nikimo,  lakini hakuangalia hayo na hivyo kutuokoa" amesema.

Ameongeza kuwa "Tusipomrudia Mungu, hasa mimi binafsi, tutakuwa wajinga wakubwa na kwa upande wangu natamani na ninaomba Mungu anisaidie nienende katika mwenendo mwema kisha nimfuate katika roho na kweli”.

Mhanga mwingine wa tukio hilo Dickson moris (25) amesema kuwa mara kadhaa alikuwa akisikia watu hasa wahubiri wakitaja miujiza ya Mungu, huku yeye akiwa mwenye kubeza kauli hizo lakini akasema muujiza wa ajabu umetokea kwake na wenzake hao 15.

"Sina ubishi tena na Mungu juu ya uwepo wake na matendo makuu anayotenda na aliyotutendea sisi viumbe wake, hata tusiompenda na kumfuata. Tuna deni kubwa kwake. Iwapo tutaendelea kuwa na kiburi katika kumfuata, sijui nini kitatupata maana ametutoa kuzimu tunapaswa kumtukuza kwa matendo yetu mema" ameeleza.

Aidha wahanga wengine wa tukio hilo wamekiri wazi kuwa hata shughuli zao za uchimbaji hazitakiwi kabisa kumtaja Mungu na mara kadhaa wakiona kuna mtu miongoni mwao anamtaja Mungu, humchukulia mtu huyo kuwa anawazibia rziki kwa kuwa wao wanaamini kuwa dhahabu na Mungu haviendani.

Kutokana na tukio hilo wahanga hao wamekiri kuwa dhana ya kutomhusisha Mungu katika uchimbaji wa madini ni dhana potofu, huku wakihoji kuwa kama dhahabu na Mungu haviendani kwa nini Mungu amewaokoa wakiwa wanatafuta dhahabu, tena kutoka sehemu ambayo kwa hali ya kawaida asingeweza kuokoka hata mmoja.

Wakati huo huo watu mbalimbali wamevipongeza vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama liiwemo jeshi la Polisi mkoani Geita, jeshi la uokoaji la zimamoto, makampuni binafsi ya uchimbaji madini yaliyotoa vifaa vyao vya kuokolea pamoja na wananchi wa kawaida walijitoa muhanga kufanikisha uokoaji huo.

Hata hivyo wananchi hao wamesikitishwa na wachimbaji kutoka nje ya nchi kuja kuwekeza tena katika sekta muhimu ya madini huku wakiwa na zana duni na hivyo nao kuonekana kama wachimbaji wadongo wasio na zana za kisasa.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU