USIFIKIRIE UZEE, FIKIRIA KUISHI



OKTOBA Mosi ya kila mwaka ni siku iliyoteuliwa na Umoja wa Mataifa kuadhimisha uwepo wa wazee katika jamii kote ulimwenguni. Siku hii ilianza kuadhimishwa rasmi Oktoba 1, 1991 kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu mambo yanayowalenga wazee ikiwemo kutoheshimu haki za wazee, kutazama mahitaji na maslahi ya wazee na kuhakikisha mzee popote alipo ulimwenguni anapata huduma za msingi za kijamii kama vile huduma bora za afya.
Maadhimisho ya siku ya wazee duniani ni moja kati ya jitihada za Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UN) katika kutambua na  kuhamasisha jamii kuweza kulinda na kutetea haki za wazee duniani kote.Umoja wa Mataifa umetenga siku hii kwa lengo la kutafakari hali ya maisha ya wazee na changamoto zinazowakabili; na hivyo kuweka mipango thabiti ya kuboresha maisha yao na kuwafanya waishi maisha ya heshima, hadhi, na kuthaminiwa utu wao. 
Siku hii inaakisi mila na desturi nzuri za kuwaenzi wazee kwa kutambua kuwa wazee ndiyo chanzo cha urithi wa historia ya nchi, washauri wa familia na jamii, watu wenye hekima, na walezi katika jamii. Hivyo jamii inao wajibu wa kuwaondolea vikwazo wazee katika kupata huduma za kijamii ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua pale ambapo mzee ananyanyaswa au kutendewa isivyostahili.
Wazee wapewe mafao yao kwa wakati kwakuwa ni nguvu kazi yao na ni haki yao, lakini uzee si mwisho wa maisha. Uzee si mwisho wa kufanya maendeleo. Uzee si mwisho wa ndoto ya mafanikio. Mtu mmoja alipostaafu kazi kwa mtazamo wake baada ya kupata mafao alianza kutapanya mafao yake.
Alifanya sherehe, alifanya starehe za kila aina, aliwafurahisha watu mbalimbali kwa pesa yake akidhani yeye anakaribia kufa kwa sababu kustaafu ni uzee, hivyo kwa nadharia yake na mapokeo yake ya kidunia aliamini ukiitwa mzee unasubiri kufa. Mwezake aliyestaafu naye baada ya kupata mafao alijiwekeza kibiashara. Yule aliyefikiria kufa alishangazwa miaka ikienda lakini ‘hakioni’ kifo.
Wakati huo akiwa na hali mbaya ya aibu mtaani, alimtafuta rafiki yake aliyestaafu naye na alipompata alimkuta akiwa tajiri mkubwa anayetegemewa katika Wilaya fulani. Alishangaa, lakini alisaidiwa kiuchumi naye akawa mfanyabiashara.
Uzee si kufa wala uzee si ugonjwa ama uzee si uchawi. Uzee ni umri si mvi. Siku hizi hata vijana wanaota mvi. Siku hizi baadhi ya vijana wanaonekana wazee na wazee wanaonekana vijana. Jambo hili linatokana na mazingira ya wakati na mtindo wa maisha. Kuwa mzee si kwamba huwezi kufanya kazi. Usifikirie uzee ni kifo, bali fikiria kuishi.
Yoshiharu Shiozaki wa nchini Japani, mwenye umri wa miaka 73, anafanya kazi ya kushauri wale wanaotaka kununua au kuuza ardhi au nyumba anasema hivi: “Ninatambua kwamba ili niwe na afya nzuri ni lazima nifanye mazoezi kwa ukawaida. Nimekuwa nikitunza bustani ndogo kwa muda wa miaka michache iliyopita.
Ninajisikia vizuri sana baada ya mazoezi hayo. Ili nitimize mengi iwezekanavyo nimejitahidi kufuata kanuni hii: ‘Kusitasita ni mwizi wa wakati; na kuahirisha mambo ni msaidizi wake.” “Ninatambua kwamba ili niwe na afya nzuri ni lazima nifanye mazoezi kwa ukawaida.” “Nina maumivu ya kiuno, msukumo mkubwa wa damu, na ugonjwa wa masikio. Ninasafiri kwa baiskeli kutoka nyumbani hadi ofisini siku nne kila juma; kwenda na kurudi ni umbali wa kilometa 12.
Mazoezi hayo ni mazuri, kwa kuwa hayaumizi mgongo wangu lakini huimarisha misuli yangu ya miguu. Ninajitahidi kuishi kwa amani pamoja na wengine hasa majirani. Ninajitahidi kutozingatia udhaifu na makosa ya wengine. Nimetambua kwamba watu huitikia upesi wanapotiwa moyo kuliko wanapochambuliwa.” ‘Ninajitahidi kutozingatia udhaifu wa wengine.’
Endapo kila mtu angepewa nafasi ya kueleza nini maana ya uzee angesema vile anavyofikiria. Wengine wangesema uzee ni kukunjamana kwa ngozi, uzee ni kuwa na mvi nyingi, uzee ni kuwa na hekima, uzee ni kutembelea fimbo, uzee ni kuwa na macho mekundu, mzee ni yule anayepinga mabadiliko ya kijamii, uzee ni ugonjwa, mzee ni yule anayeshindwa kutembea na wengine wangesema kustaafu kazi ni uzee.
Wengi hudhani kwamba wazee wengi hutegemea watu wengine. Hiyo si kweli. Gazeti la The New York Times Magazine lilisema kwamba nchini Marekani, ‘wazee wengi wanaojitegemea ni watu wa tabaka ya kati katika jamii ambao wana fedha nyingi, na watu wanaochunguza jamii wametambua kwamba idadi ya wazee wenye nguvu walio matajiri inaongezeka.’
Hekima ya wazee inaonwa kuwa yenye thamani kubwa katika jiji la Troyes huko Ufaransa na mahali penginepo. Hekima hiyo inafaidi watoto wanaofundishwa na wazee ufundi kama vile useremala, kutengeneza kioo, kukata mawe, ujenzi, na ufundi wa mabomba baada ya shule.
Bila shaka, furaha yetu ya uzeeni inaweza kuathiriwa kwa sababu ya ubaguzi na maoni ya wengine, lakini kwa kawaida inaathiriwa pia na mtazamo wetu. Wewe mwenyewe unaweza kufanya nini ili uwe mtendaji, kimwili na kiakili, hata ingawa mwili wako unazidi kuzeeka?.
Utaona kwamba wazee hao wote wanaendelea kufanya kazi ama kazi ya kuajiriwa ama ya kujitolea. Ukweli usiofurahisha ni kwamba, sasa hivi unaposoma habari hii wewe pia unaendelea kuzeeka. (Mhubiri 12:1) Hata hivyo, kwa hekima utatii maneno haya ya gazeti la Bulletin of the World Health Organization: “Kama vile afya nzuri inavyomwezesha mtu kuwa mtendaji, ndivyo utendaji unavyofanya mtu awe mwenye afya.”
……………………………………

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU