SHIRIKA LA MABINTI WA MARIA LAPONGEZWA



PADRI  Alfred Lwamba wa Jimbo Kuu Katoliki Mwanza amelipongeza shirika la Masista la Mabinti wa Maria kwa kazi nzuri wanayofanya ndani ya Kanisa na kwa jamii yote kwani licha ya mambo ya kiroho  pia wamekuwa wakitoa  huduma nzuri kwenye  sekta ya elimu  na afya pamoja na kuwapatia malezi bora watoto wanaosoma katika shule zao.
Pongezi hizo amezitoa baada ya misa takatifu  kwenye sherehe ya ufunguzi wa jengo la utawala la ghorofa mbili la shule ya Sekondari ya Lumala iliyopo  Jimbo Kuu Katoliki Mwanza inayoendeshwa na shirika la Mabinti wa Maria ambako wamekuwa wakitoa malezi na elimu bora kwa watoto wanaosoma hapo.
Padri Lwamba amesema uwekezaji uliofanywa na shirika hilo  katika huduma za jamii hasa elimu na afya ni kwa maslahi mapana ya jamii na taifa kwa ujumla  na wamekuwa wakitimiza wajibu huo katika kuwalea watoto kimaadili mema na maarifa yatakayowasaidia baadaye katika  kulitumikia Taifa.
Amesema elimu inayotolewa katika shule ya Lumala kuanzia chekechea, msingi hadi Sekondari kidato cha nne ni elimu bora na malezi  mema ya  kiroho  kwa watoto wote  bila ubaguzi wa kidini.
Padri Lwamba amewahimiza wazazi na walezi kuwekeza zaidi katika kuwasomesha watoto kwa sababu wakitaka wawe madaktari, marubani, walimu na wataalamu mbalimbali ni lazima watumie fursa kuhakikisha wanawasomesha watoto.   
“Hata maadiko matakatifu katika Biblia yametwambia kuwa “ mshike sana elimu usije ukamwacha akaenda zake” kwa hiyo ndugu zangu wazazi na  walezi  tunawajibu wa kuwasomesha watoto waweze kupata elimu bora,” amesema padri Lwamba.
Nayo jamii ya Jimbo Kuu Katoliki Mwanza wamelipongeza shirika la Masista la Mabinti wa Maria lenye makao yake makuu Jimbo Kuu Tabora kwa kazi nzuri wananazofanya katika suala la elimu na malezi bora kwa watoto wanaosoma katika shule  hiyo inayoendesha shirika hilo.
Mzazi Erick Odhiambo ambaye pia ni Mwenyekiti wa ujenzi akiongea kwa niaba ya wazazi wenye watoto wanaosoma katika shule hiyo iliyopo parokia ya Ilemela katika Jimbo Kuu Mwanza ametoa pongezi kwa shirika hilo kwa kujenga shule hiyo na kutoa huduma za kiroho ikiwemo suala la elimu na malezi bora kwa watoto wao wanaosoma hapo.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Benjamin Perman amewashukuru wazazi na walezi kwa ushirikiano wao mzuri na kuahidi  kuendelea kutoa elimu bora, malezi mazuri ya kiroho na kimwili kwa watoto wote bila kujali tofauti za kiimani.
Makamu Mama Mkuu wa Shirika la Mabinti wa Maria lenye makao makuu Kipalapala Jimbo Kuu Katoliki Tabora Sista Maria Evodia Lupagaro aliyemuwakilisha Mama Mkuu Theresia Sungi, amesema karama yao ni upendo, huruma na huduma na ameipongeza jamii na Serikali kwa ushirikiano wao kwa shirika wanapoihudumia  jamii.
Sista Lupagaro amesema wanaishukuru Serikali kwa kuwapatia kibali cha kuanzisha na kuendesha shule hiyo na imekuwa ikiwakagua na kuwapa miongozo mbalimbali kielimu katika kuendesha shule lengo likiwa kuwasaidia watoto wa Taifa la kesho.





Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU