"HAKUNA TALAKA KANISA KATOLIKI"



KANISA Katoliki linaamini kwamba ndoa ni makubaliano ya mke mmoja na mume mmoja ambapo baada ya makubaliano hayo yaliyofanyika kihalali, hakuna mahakama yeyote inayoweza kutoa talaka kuwatenganisha wanandoa hao vinginevyo mpaka kifo kitakapowatenganisha kadiri ya mpango wa Mwenyezi Mungu.
Ndoa katika Kanisa Katoliki ni miongoni mwa Sakramenti saba, tena ni tendo la kudumu ambalo linafanyika kwa uhalali katika vigezo vyote kwa lengo la kuwapatanisha na kuwaunganisha watu hao wawili kuwa mwili mmoja ili kuunda familia takatifu hatimaye kujenga Kanisa dogo la nyumbani.
Moja  ya majukumu yanayopaswa kutekelezwa na wanandoa mara baada ya kufunga ndoa ni kujihusisha na shughuli za Kanisa mojawapo ikiwa ni kulipa zaka na michango mingine ya Kanisa, japokuwa  kumekuwepo dhana potofu miongoni mwa waamini hasa wanandoa mara baada ya kupata sakramenti hiyo kushindwa kushiriki tena shughuli za Kanisa mfano ibada za jumuiya na ulipaji wa zaka huku wakidhani kwamba si jukumu lao.
Hayo yameelezwa na  padri Abdon Nzegesera wa parokia ya Ilonga jimboni  Morogoro katika adhimisho la ndoa takatifu lililofanyika hivi karibuni ambapo jumla ya ndoa saba zimefungwa kwa pamoja katika Kigango  cha  Mtakatifu Maria mama wa Rozali Takatifu kilichopo Msowero jimboni humo ambayo ni miongoni mwa juhudi za kutokomeza kabisa uchumba sugu.
Padri Abdon amesema kuwa ndoa ni baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, hakuna mwanadamu mwenye mamlaka ya kuitenganisha kutokana na sababu yoyote itakayoweza kujitokeza ambapo ni wajibu wa kila mmoja kujitafakari kwa kina kabla ya kuingia katika agano hilo hali ambayo wakati mwingine wengi wao hutamani kudai talaka mara baada ya kutawala magomvi na mifarakano katika familia hatimaye kutengana kabisa kinyume na sheria za Kanisa.
“Mtambue kwamba chochote kinachounganishwa na Mwenyezi Mungu hakuna mwanadamu mwenye mamlaka ya kutenganisha, ndoa ikishafungwa kanisani kwa utaratibu wa Kanisa kwa uhalali na vigezo vyote, asitokee mtu akaenda kwenye mahakama fulani ya kijiji au serikali kuomba talaka kwa sababu  zozote, hakuna atakayeweza kutoa maamuzi kinyume na sheria za Kanisa Katoliki kwa sababu linapinga uwepo wa talaka na kuwatenganisha mke na mume zaidi ya  Mungu mwenyewe kupitia fumbo la kifo, ukikubali kuingia humu ni afadhali uchukue maamuzi kabla hujasema ndiyo,  siyo kama nawatisha ili muogope bali nawaimarisha mpendane kimamilifu,” amesema padri Nzegesera.
Mbali na hayo padri Nzegesera amesisitiza kuwa changamoto katika maisha ya ndoa zipo, na isiwe chanzo kimojawapo cha kushindwa kuvumiliana, huku akiwahimiza zaidi kudumu katika sala wasisubiri tu kumwomba Mungu na kusali baada ya misukosuko, bali nyumba zao ziwe Kanisa dogo la nyumbani kupata amani, uvumilivu na upendo.
Kwa hiyo na ninyi msisubiri mpaka  misukosuko itokee ndio  mkumbuke kwamba kuna Kanisa, msisubiri mpaka  mpate  shida ndipo mkumbuke kwamba Mungu yupo, msisubiri mpaka migogoro iwazidi ndio muanze kusali, daima muwe watu wa sala muwaalike watakatifu wa mbinguni waweze kuwaombea katika nyumba zenu, majaribu yatakuwepo lakini mkidumu katika sala nyumba zenu zitakuwa Kanisa dogo  la nyumbani, si ajabu hawa hawa wanaoshuhudia ndoa hizi wakawa  wa kwanza kuleta majaribu katika ndoa zenu, vumilieni yote Mwenyezi  Mungu atakuwa pamoja  nanyi,” amesema padre Nzegesera.
Naye Nicholaus Mbota mmoja wa waliofunga ndoa, awali akizungumza kwa niaba ya wanandoa wenza  amesema kuwa waamini walio wengi wanaishi nje ya ukatoliki bila ndoa takatifu kwa kulenga ubinadamu zaidi hasa kuogopa gharama za sherehe, inafika wakati kunajengeka mazoea ya kuzoeana mke na mume na kuweka mbali baraka ya ndoa takatifu kwa misingi ya Kanisa kuishi nje ya masakramenti ya Kanisa, kumbe  jambo  la msingi ni kutimiza sheria  za Kanisa bila kujali  kula na kunywa  kuliko kuishi nje ya baraka.
“Kikubwa tuombeane na  kupendana, suala la ndoa ni kuvumiliana, kupendana, kuchukuliana, kusameheana  na  kubebeana mizigo, nadhani neno samahani linaweza kuokoa ndoa ambayo wakati mwingine ilikuwa katika hatari ya  kufa, mara nyingine kujishusha na kumjua mwenzi  wako ni dawa tosha inayoweza kutusaidia kuishi maisha ya  amani bila kukengeuka kwa sababu hata kutoka nje ya ndoa inatokana na mmojawapo kutomthamini mwenzi wake,  tukiyaishi hayo kila mmoja atakuwa  na hofu ya Mungu ndoa zetu zitakuwa imara zaidi,” amesema Mbota.
Maadhimisho  ya ndoa hizo ni miongoni mwa juhudi zinazofanywa na viongozi wa kiroho hasa paroko Abdon Nzegesera kushirikiana na makatekista wa vigango vinavyozunguka parokia hiyo, ili kuhakikisha kwamba uchumba sugu unapotea miongoni mwa waamini katika Kanisa ili kila muamini awe huru kushiriki masakramenti ya Kanisa hasa Komunio Takatifu.
Parokia ya Ilonga imekuwa na mwendelezo wa kuwakomboa waamini waishio katika uchumba sugu kwa kuwahimiza waamini hao kupitia paroko wao padri Abdon Nzegesera pamoja na makatekista wa vigango hivyo kuepuka uchumba sugu kuishi na familia bila kufunga ndoa takatifu ambapo kuna jumla ya ndoa 18 za waamini waliokuwa wanaishi maisha ya uchumba sugu zimekombolewa, ndoa 11 kutoka kigango cha Gongoni B ndani ya kipindi cha miezi miwili iliyopita na ndoa 7 kutoka kigango cha Msowero parokiani  hapo.




Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU