ASKOFU MFUMBUSA AANDIKA REKODI KONDOA



ASUBUHI na Mapema ya siku ya Jumapili ya tarehe 15/10/2017 katika Kanisa Katoliki Jimbo Katoliki Kondoa Mkoani Dodoma, palifurika waamini kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya wilaya, ndani na nje ya Nchi kuja kujionea namna upendo wa Mungu unavyofanya kazi kwa Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa Mhashamu Bernardin Mfumbusa aliyetimiza miaka 25 ya Upadri.

Misa iliyoambatana na maandamano yaliyofanywa na Maaskofu, Mapadri pamoja na wageni wengi waalikwa kuanzia katika bustani ya uaskofu na kuelekea kanisani, imefanyika katika Kanisa Kuu la Jimbo na kuwashirikisha waamini wengi wakiwemo Maaskofu, Mapadri, Washangwera, viongozi wa Serikali pamoja na viongozi wa Siasa.

Washiriki wa adhimisho hilo la kihistoria kwa wakati tofauti walipata fursa ya kutoa salamu mbalimbali huku wakiuongelea utume wa Askofu Mfumbusa.

Katibu Mkuu Shirikisho la wanachama Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki na Kati (AMECEA), Padri Ferdinand Lugonzo kutoka nchini Kenya amesema kuwa amefurahi sana kushiriki sherehe hii na kumpongeza Askofu kwa hatua aliyoifikia.

"Nimefurahi kushirikiana nanyi katika sherehe hii, nawapongeza sana, hii inadhihirisha ukaribu uliopo kati  ya Askofu, watumishi na waamini. Niseme mmebarikiwa sana  kwa sababu Askofu wa Jimbo hili ni mtu wa kufanya kazi kwa ukaribu na kila mtu. Kwa muda wote amekua akifika katika ofisi za AMECEA Kenya, na kuuliza ni lini tutafika jimboni Kondoa? Amekuwa akiniambia kuwa Kondoa kuna  River Side ( Kando ya Mto), ni kweli nimefika na nimejionea Kondoa namna ilivyo," Amesema  Padri Lugonzo.

Ameongeza kwa niaba ya wenzake waliofuatana naye kuwa "Tunaposherehekea maadhimisho haya lazima tumshike mkono kwa kazi alizofanya, niseme asante sana kwa nafasi hii niliyopewa kwa kusema chochote kwake."

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora, Mhashamu Paulo Ruzoka, amesema kuwa uthibitisho wa mahudhurio ya Maaskofu kutoka katika majimbo mbalimbali yakiwepo Mpanda, Geita, Singida, Mahenge pamoja na Kigoma pia Washangwera waliosoma Seminari za  Tabora, Segerea pamoja na Songea ni ushahidi kuwa Askofu Mfumbusa ni mtu wa kuigwa kwa ushirikiano alioufanya katika kipindi chake cha miaka 7 ya kuliongoza Jimbo Katoliki Kondoa.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei Jimbo, Tius Justine amesema kuwa pamoja na kumpongeza Askofu, Jimbo hilo limetoa fedha kiasi cha milioni kumi na moja, laki saba na elfu kumi na tatu na sabini (11, 713, 70) kumuunga mkono, fedha ambazo zimeelekezwa katika shughuli za maendeleo katika parokia mbalimbali ndani ya Jimbo.

“Ni ukweli usiopingika kuwa tangu Askofu awepo jimboni hapa tumeona maendeleo makubwa yakiwa ni pamoja na kuwepo kwa bustani ya nyanya, ufugaji wa kuku wa mayai, bwawa la samaki pamoja na kuanzishwa kwa mahali pa kupumzikia ambapo ni kandokando ya mto Mkondoa (RIVER SIDE). Pamoja na yote,  mafanikio mengine ni kuanzishwa kwa  parokia mpya ambazo ni Parokia ya Soya, Kidoka, Gonga, Lalta pamoja na tunayotarajia hivi karibuni parokia ya Chemba," amesema Justine.

Wanenavyo Waamini
Naye Valenina Joseph Mkazi wa Tanesko amekiri kwa kusema kuwa jitihada za Askofu zimeonekana kwa haraka pamoja na ukweli kuwa ni muda mchache amelitumikia Jimbo Katoliki Kondoa, hivyo ni shukrani za kipekee kwa Mungu kumleta mtumishi mwenye roho ya kipekee.

Godhard Hunja, Mkazi wa Kilimani amesema kuwa tukio hilo ni la kihistoria kwani Askofu Mfumbusa ana maono ya mbali, kwa jambo kama hili ni kumshukuru Mungu kwani kwa muda mrefu kama huo kwa kumtumikia Mungu kwa kutoa huduma, ni kwa  kuongozwa na Mungu.

Shukrani za kipekee
Askofu Bernardin Mfumbusa licha ya kuwashukuru wote Mwenyezi Mungu pamoja na wote waliohudhuria adhimisho hilo, amesema kuwa miaka 25 iliyopita walikua  36, katika safari moja lakini leo wamebaki  27, na 9 kati ya hao  wameaga Dunia.. "Niseme Ahsanteni sana kwa namna ya kipekee namna mlivyoonesha upendo mkubwa mbele za Bwana, leo katika safari yetu ya mapadri 36 tumebaki mapadri 27, wenzetu 9 wametangulia," amesema Askofu Mfumbusa.

Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU