Maaskofu Katoliki wataka hukumu ya kifo itazamwe upya



MAASKOFU wa Kanisa Katoliki nchini wameiasa serikali kubadili sheria inayoruhusu adhabu ya kifo kwa wahalifu badala yake watoe hukumu ya kifungo cha maisha.
Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya ameeleza hayo kwa niaba ya Maaskofu Katoliki Tanzania hivi karibuni huko jimboni TUNDURU-Masasi kwenye ibada ya mazishi ya Askofu wa Jimbo hilo marehemu Castory Msemwa.
“Leo tunapomzika Askofu Msemwa tunakumbuka kuwa mwanadamu anazaliwa na anakufa kupitia vifo mbalimbali ukiwemo uzee na magonjwa. Huo ni mpango wa Mungu kwamba mwanadamu afe ili afike kwenye makao aliyomuandalia.
Lakini kuna vifo ambavyo ni kinyume na mpango wa Mungu ikiwemo sheria inayoruhusu mahakimu kutoa hukumu ya kifo. Aliye na mamlaka ya kuchukua uhai wa mwanadamu ni Mungu peke yake kwani uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu.
Sababu ya vifo vinavyotokea duniani ni sisi wanadamu wenyewe. Maandiko matakatifu yanatuambia Mungu peke yake ndiye ana uwezo na mamlaka ya kuchukua uhai. Uhai ni kitu kitakatifu lakini baadhi yetu tunapuuza.
Tunafahamu kwamba sheria za nchi nyingi duniani zinaruhusu mahakimu kutoa adhabu ya kifo ikiwemo Tanzania. Tunaiomba serikali yetu ione namna ya kubadili sheria hiyo na badala ya kifo, wahalifu wapewe adhabu ya kifungo cha maisha. Kama taifa tusikubali kuridhia mikataba ambayo haiheshimu uhai,” amesisitiza Askofu Mkuu Kinyaiya.
 Aidha maaskofu pia wameisisitiza jamii kuacha kutoa mimba kwani ni namna nyingine ya kutoa uhai wa mwanadamu suala ambalo wamesema ni kosa na ni dhambi kwa anayetoa na yeyote anayeshiriki. Hivyo jamii nzima ina wajibu wa kuheshimu na kutunza uhai ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu.
Wamewaonya vijana ambao ni nguvu ya taifa la Tanzania kuacha kuhatarisha maisha yao kwa kukumbatia utamaduni wa kifo.
“Vijana wanakufa kabla ya wakati wao kwa kudhoofisha miili yao kwa kutumia sumu mbalimbali kama vile mahusiano ya hovyo hovyo, dawa za kulevya nk. Wakidhani ndiyo namna ya kupata starehe kumbe wanajiangamiza.
Tatizo la vijana kujiua wenyewe nalo linaongezeka Tanzania. Kufuatana na ripoti ya Shirika la Afya duniani Tanzania ni kati ya nchi 10 duniani, zinazoongoza kwa watu hasa vijana kujiua.
Wapendwa vijana sisi wazee wenu tunawaasa muachane na huo utamaduni wa kifo, ishini maadili, maadili mliyofundishwa na Askofu Castory MSEMWA, mnayofundishwa na viongozi wenu wa dini mkijua kuwa miili yenu ni hekalu la Roho Mtakatifu,” amesema.
Katika mazishi hayo Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya amesema kuwa, Maaskofu Katoliki Tanzania pia wametaka jamii itafakari pia kifo cha mazingira katika dunia wanayoishi.
Katika barua yake ya pili inayojulikana kama ' Laudato Si' yaani ‘sifa  iwe kwako’ Baba Mtakatifu Fransisko pamoja na mambo mengine anazungumzia jinsi  wanadamu wanavyoiua dunia kwa vitendo mbalimbali. Wanatumia dunia kwa uroho bila mpango kiasi kwamba wanaiua dunia ambayo ni mama yao.
“Matokeo ya madhara yanaturudia kwa njia ya ukame, ongezeko la hewa ya ukaa ambalo ni mbaya kwa afya zetu nk. Tutakimbilia wapi tukiiharibu dunia?
Tunamuasa kila mmoja wenu asiiumize dunia kwa vitendo visivyofaa, kama vile kukata miti hovyohovyo, kuchoma uoto asilia, kuua wanyama nk.” amesisitiza Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.
Ameiasa jamii kuacha kulilia kifo kwani jinsi wanavyomuona Marehemu Askofu Castory Msemwa ndivyo kila mmoja atakuwa hivyo kwani kuzaliwa ni bahati na matokeo yake ni kifo ili mwanadamu aende kuishi na Mungu kwenye makao aliyomuandalia.
“Kuna watu wengi hawajapata bahati ya kuzaliwa duniani kwa sababu hawakutungwa mimba kabisa na hawakuja duniani kabisa na kwakuwa hawakuja duniani kabisa hawatakufa kwa sababu hawapo.
Sisi tuliobahatika kuzaliwa duniani hatma yetu ni kufa ili turudi kwa Baba, hivyo tusilalamikie kifo kwani ni sehemu ya hiyo bahati ya kuishi hapa duniani.
Tumeambiwa kuwa  Askofu MSEMWA amefariki kwa ugonjwa ambapo Mwenyezi Mungu ameamua kumchukua. Sisi kama wanadamu jukumu letu ni kupokea mapenzi ya Mungu ijapokuwa ni magumu kama wanadamu. Tuendelee kumuombea.
Ni wakati wetu wa kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Askofu Msemwa hapa duniani kwani aliyoyafanya hakuna mtu mwingine ambaye anaweza kufanya kwani duniani hakuna watu wawili wanaweza kufanana na kufanya jambo lilelile. Kila mtu ana namna yake ya kutenda, naye alikuwa maalumu.
Tunamshukuru Askofu Msemwa kwa kutumia vipaji vyake kulitumikia Kanisa na jamii kwa ujumla bila kulalamika. Tunaamini kuwa kwakuwa alijitahidi kuishi wito wake kama Padri na Askofu Mwenyezi Mungu atampokea kwake mbinguni.
Suala la msingi ni kuishi ukristo wetu, tuishi maisha ya Sakramenti ili tujitakatifuze, tuwe watu wa toba tujiandae ili siku moja turudi kwa baba yetu Mbinguni,” ameeleza.
Amesema kuwa Maaskofu wanashukuru wote waliojitolea kumuuguza na kujaribu kuokoa maisha ya Askofu Msemwa kuanzia madaktari katika hospitali ya Taifa Muhimbili, India nk.
Pia anashukuru Ubalozi wa Tanzania nchini Oman pamoja na serikali nzima ya Tanzania kwa ushirikiano wa kusafirisha mwili wa marehemu kutoka Oman hadi Tunduru kwenye maziko.
Amesema Maaskofu wote wa Kanisa Katoliki wanaungana na wana Tunduru kufarijiana na kutiana moyo katika kipindi hicho kigumu.
Amewataka mapadri wa Jimbo Katoliki TUNDURU-Masasi kuwa na ushirikiano wakati huo ambapo wanasubiria wapewe msimamizi wa muda.
“Ni wazi kiti cha Askofu hapa Tunduru Masasi kipo wazi, sasa ni wajibu wetu kusali na kuomba ili Roho wa Mungu atuchagulie mchungaji mwingine wa Tunduru Masasi.
Tunawaomba mtunge sala maalumu mtakayoisali kila jumapili baada ya Misa kwa lengo hilo.
Na wakati tukisubiri Askofu mwingine, sisi Maaskofu tunawasihi sana mkae kwa amani, upendo na mshikamano,” amesisitiza Askofu Mkuu Kinyaiya.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU