"TUSIPOFUNDISHA DINI SHULENI MAOVU HAYATAKOMA"



PADRI Gaitan Maswenya, Paroko wa Parokia ya Makole Jimbo Kuu Katoliki Dodoma amesisitiza umuhimu wa watoto wa shule za msingi na sekondari kufundishwa somo la dini shuleni kwao ili kuwajenga kiroho na kiutu.
Padri Maswenya amesema hayo hivi karibuni  alipokuwa akizungumza na KIONGOZI katika mahojiano maalumu.
Amesema kuwa somo la dini shuleni linasaidia kuwajenga watoto kumjua Mungu na kuwafanya wawe wanyenyekevu, hivyo kuwaepusha na majaribu mbalimbali ya shetani ikiwemo vitendo vya wizi, ujambazi na maovu mengine.
“Watoto hawa wanafundishwa masomo ya kawaida na walimu wao, lakini bila ya kuwafundisha somo la dini tutegemee kuvuna mabua,” amesema padri Maswenya.
Ameongeza kuwa Serikali imeandaa mazingira mazuri ambapo imeruhusu viongozi wa madhehebu ya dini kufika katika shule za msingi na Sekondari kufundisha, hivyo hakuna kisingizio chochote cha kukosa kwenda kuwafundisha somo hilo.
“Watoto hawa wengine hawana fursa ya kupata neno la Mungu kwa sababu miongoni mwao hawaendi kanisani kwa sababu moja ama nyingine, kumbe somo la dini litasaidia kuwainjilisha na hivyo kumjua Kristo mkombozi wa dunia.”
Padri Maswenya amefafanua kuwa ili Kanisa liweze kumtangaza Kristo ni lazima lianzie chini kwa watoto wakiwemo wale walioko shuleni.
Amewaasa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kuwasikiliza kwa umakini mapadri na viongozi wengine wa dini wanapofika shuleni kuwafundisha somo la dini ili waweze kulifahamu neno la Mungu ambalo litawasaidia kujenga urafiki na Mwenyezi Mungu.
Katika hatua nyingine Parokia hiyo imefanya sherehe ya kumkumbuka somo wake Mtakatifu Gaspal del Buffalo Alhamisi hii ambapo Ibada ya misa takatifu na mashangilio mbalimbali pamoja na chakula cha pamoja yamefanyika.
Padri Maswenya amewashukuru  waamini wote wa Parokia hiyo kwa majitoleo yao ambayo yamekuwa yakifanikisha shughuli mbalimbali parokiani  hapo. 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU