TEMEKE YAUNDA KAMATI YA MAHUSIANO BAINA YA DINI MBALIMBALI



Wajumbe wa Kamati ya Mahusiano baina ya Watu wa Dini Mbalimbali wilayani Temeke wakiwa katika picha ya pamoja muda mfupi baada ya kuchaguliwa (Picha na Dalphina Rubyema)



ILI kusimamia shughuli za ustawi wa mwanadamu pasipo kufungamana na upande wowote wa kidini, Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam imefanikiwa kuunda Kamati ya Mahusiano ya Dini mbalimbali (Interfaith) itakayodumu kwa kipindi cha miaka mitatu.
Kamati hiyo yenye wajumbe kutoka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), imeundwa hivi karibuni wakati wa kikao cha siku mbili kilichoratibiwa na ofisi ya Mradi wa Uendelezaji wa Utu wa Mwanadamu (IHDP) unaotekelezwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) kupitia Idara yake ya Haki, Amani na Uadilifu katika Uumbaji (JPIC) na kufadhiliwa na Shirika la Misaada kwa Makanisa la Norway (NCA).
Viongozi hao waliochaguliwa na nafasi zao zikiwa kwenye mabano ni pamoja na Sheikh Zailaih B. Mkoyogope kutoka BAKWATA (Mwenyekiti), Padri Andrew Mtweve toka CCT (Makamu Mwenyekiti), Mchungaji Manase Mwakalile toka CCT (Katibu), Sheikh Ali Mohamed Ali toka BAKWATA (Katibu Msaidizi) na  Padri William Sindano toka TEC (Mhasibu).
Akizungumza kabla ya kuundwa kwa Kamati hiyo, Mkurugenzi wa Mahusiano baina ya Dini Mbalimbali , Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Padri Christian Likoko ambaye pia ni Mshauri wa Kamati hiyo amewaambia washiriki wa kikao hicho kuwa pamoja na mambo mengine, kuundwa kwa kamati hiyo kutawezesha wanaTemeke kujumuika kwa pamoja kujadili mambo ya  amani na maendeleo kwa jamii kwa ufanisi zaidi bila kuathiri imani  ya mtu.
“Uhusiano huu si kwa ajili ya kuingilia au kuathiri imani…kila imani itaendelea kusimama na misingi yake iwe ni kiibada na kuongoza bila kuingiliwa,” amesema Padri Likoko ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Kanisa la Mashahidi wa Uganda, Magomeni Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam na Mshauri wa Kamati hiyo.
Amesema kamati hiyo pia itakuwa na jukumu la kujadili kwa kina vyanzo mbalimbali vinavyoweza kuchochea vurugu na uvunjifu wa amani hivyo kujadili njia bora ya utatuzi.
“Pia kamati itashauri ama kupanga na kutekeleza programu mbalimbali za pamoja zenye lengo la kuleta maendeleo na uwajibikaji kwa jamii katika maeneo ya wilaya ya Temeke,” amesisitiza.
Kwa sasa shughuli za maendeleo zinazosimamiwa chini ya Mahusiano baina ya Dini mbalimbali wilayani Temeke ni zile zinazotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji wa Utu wa Mwanadamu (IHDP) TEC kupitia Idara ya Haki, Amani na Uadilifu katika Uumbaji (JPIC) kwa kufadhiliwa na Shirika la Misaada kwa Makanisa la Norway (NCA).
Awali akitoa utambulisho kwa washiriki wa kikao hicho na shughuli zinazofanyika chini ya IHDP, Mratibu wa Taifa wa Mradi huo Joyce Lusatila, amesema shughuli zimejikita katika maeneo makuu mawili ambayo ni pamoja na  Uwezeshaji wa Kiuchumi (Economic Empowerment) na Ulinzi wa Rasilimali (Resource Governance).
Amesema chini ya uwezeshaji wa kiuchumi shughuli zinazofanyika ni pamoja na zile za Benki za Kijamii Vijiji za Watu wa Dini Mbalimbali (IR-VICOBA) wakati ulinzi wa rasilimali unahusisha masuala ya kuwezesha jamii katika ngazi za msingi kufuatilia Rasilimali za Umma zinazotolewa kwa ajili ya shughuli mbalimbali za Maendeleo katika maeneo yao (PETS). Hata hivyo amesema kuna masuala mtambuka yanayofanyika chini ya mradi huo ambayo aliyataja kuwa ni jinsia na usaidizi wa kisheria.
Akizungumza baada ya kuchaguliwa, Mwenyekiti Sheikh Zailaih Mkoyogope, amesema kamati hiyo itafanya kazi kwa kujituma kwa maslahi ya wananchi wa Temeke bila kujali itikadi za kisiasa, dini, kabila na rangi.
“Tunachoomba ni kupewa ushirikiano unaostahili kutoka TEC kwani kama tulivyoambiwa awali kwamba shughuli hizi upande wa Temeke zinasimamiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Kazi kubwa iliyopo mbele yetu ni kwenda kujitambulisha kama Kamati kwa Mkuu wa Wilaya pamoja na kuunganishwa na wawezeshaji hasa IR-VICOBA na kamati za PETS ili tuweze kuwafikia walengwa wengine,” amesema.
Shughuli za Usimamizi wa Mradi wa Uendelezaji wa Utu wa Mwanadamu wilayani Temeke chini ya TEC zilianza mwaka 2008.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU