‘WAZAZI WANAOSALI PAMOJA WANAJENGA MAADILI YA TAIFA’ ASK. KILAINI

n Na Sixmund Nyabenda

ASKOFU Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini amesema kuwa wazazi na wasimamizi wanapaswa kuwa kitu kimoja na kuwaelekeza watoto wao ili waendelee kuyashika waliyofundishwa.
Ameeleza hayo katika Ibada ya Misa Takatifu Parokia ya Watakatifu wote Kiluvya Jimbo Kuu la Dar es Salaam ambapo vijana 115 wamepokea Sakramenti ya Kipaimara. Katika mahubiri yake amesema kuwa, Kipaimara ni Sakramenti ya ukomavu na Mafuta ya Krisma wanayopakwa wana Kipaimara  yanaacha alama isiyofutika, na kupokea Roho Mtakatifu mioyoni mwao.
Aidha, Askofu Kilaini amesema kuwa kijana anayepata kipaimara tayari ni askari wa Kristo kwa sababu anayo mawazo mazuri, matendo mazuri, fikra nzuri katika kujituma kutekeleza tendo lolote linalotendeka kadili ya miongozo ya Kanisa.
“Mwanakipaimara asione haya kutaja maneno ya Mtume Paulo kuwa kuishi kwangu ni Kristo” amesisitiza.
Hata hivyo, wazazi na walezi au wasimamizi wa vijana ambao wamepewa Kipaimara wametakiwa kuendelea kuwalea vijana hao maana mafundisho waliyoyapata hayatoshelezi hali halisi ya imani yao bali kuendelea kuwaelekeza katika kumshuhudia Kristo.
“Ili kutengeneza jeshi la Kristo lazima malezi bora yaanzie ngazi ya familia. Mazingira ya nyumbani yakiandaliwa vizuri hasa wazazi kwa kusali pamoja, kufanya maamuzi ya busara kwa pamoja hata na watoto watakuwa na hekima katika kuishi maadili yao” amesema.
Pia wazazi wametakiwa kutofumbia macho mambo maovu ambayo yanaweza kuchangia watoto wao kuzama katika ulimwengu wa maovu na badala yake kuwafundisha vijana wao misingi ya Kanisa Katoliki na kuishikilia vema katika maisha yao.
Paroko wa Parokia hiyo Padri Maximilian Wambura, amempongeza Askofu Kilaini kwa kuwa tayari kuitika mwito wa kufika Parokiani hapo na kuwapa vijana Sakramenti ya Kipaimara, pia amewashukuru, Makatekista na Mafrateli kwa kazi nzuri ambayo wameifanya ya kuwaandaa vijana hao. Amewataka wazazi wadumishe mshikamano katika kuwalea vijana na pia kuendelea kuwahimiza katika kulinda, kusimamia, kutetea na kulitegemeza Kanisa la Kristo kwa hali na mali.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU