SHINYANGA WAPATA MAPADRI WAPYA

n Na Joachim Mahona

ASKOFU wa Jimbo Katoliki Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu ametoa Daraja Takatifu ya Upadri kwa mashemasi wawili wa Parokia ya Nyalikungu – Maswa, mapema  Agosti 22, 2017.
Misa hiyo ya upadrisho  imefanyika katika viwanja vya Kanisa la Bikira Maria Malkia wa Mashahidi wa Afrika mjini Maswa na kuhudhuriwa na mapadri kutoka ndani na nje ya jimbo la Shinyanga, Viongozi wa serikali, Watawa pamoja na waamini.
Wakati wa misa hiyo Askofu Sangu amemshukuru Mungu kwa kulijalia Jimbo la Shinyanga kupata Makasisi wapya. Mapadre hao wapya ni James Jidasanja na James Misana ambao walikuwa miongoni mwa mashemasi watatu waliopewa daraja la ushemasi na askofu Sangu mnamo Februari 2 mwaka huu 2017 katika kanisa kuu la Mama Mwenye Huruma Ngokolo mjini Shinyanga.
Akitoa neno mara baada ya misa kwa niaba ya mapadri na waamini wa parokia ya Nyalikungu, Paroko wa Parokia ya Nyalikungu Padri Simon Maneno ametumia nafasi hiyo  kuwakaribisha mapadri hao wapya katika urika wa mapadri  na kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Mapadri hao wapya ndani ya Jimbo.
Pia amemshukuru askofu wa jimbo la Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu kwa kuongeza watenda kazi wengine watakosaidia kazi ya kikuhani katika Jimbo la Shinyanga.
Akizungumza kwa niaba ya mwenzake mara baada ya misa ya upadrisho padri mpya James Jidasanja amemshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha kufikia daraja hilo la upadri na pia wamewashukuru wazazi wao na wote waliowasaidia kufikia wito huo huku wakimshukuru  Askofu Sangu kwa kukubali kuwapa daraja takatifu la upadri na kuwaweka kuwa miongoni mwa makasisi wa jimbo la Shinyanga.
Akizungumza kwa niaba ya serikali katika sherehe hizo  za updrisho Mkuu wa Wilaya ya Maswa Dkt. Seif Shekalaghe amepongeza juhudi zinazofanywa na Kanisa Katoliki kwa kuunga mkono juhudi za serikali za kuwaletea maendeleo wananchi kwani kwa muda mrefu limekuwa mdau mkubwa wa maendeleo  kwa kushirikiana na serikali na hasa katika nyanja za elimu na afya. 
Ametoa mfano jinsi Kanisa lilivyoweza kuanzisha taasisi nyingi za kielimu ikiwemo shule za sekondari pamoja na kujenga Hospitali ya Rufaa ya Bugando iliyoko jijini Mwanza ambayo inahudumia Watanzania wengi bila ubaguzi.
Mkuu huyo wa wilaya pia alilielezea Kanisa Katoliki kuwa lina mchango mkubwa  katika kudumisha amani na utulivu wa nchi na alitumia nafasi hiyo  kuwataka wananchi kuwa macho na watu wanaotaka kuvuruga amani na kuhakikisha wanailinda amani iliyopo ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa katika vyombo vya ulinzi na usalama pale wanapoona  kuna viashiria vya uvunjifu wa amani ili hatua ziweze kuchukuliwa mapema.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU