SERIKALI IANGALIE UPYA WALIOFUKUZWA KWA VYETI FEKI

n Na Rodrick Minja, DODOMA.

SERIKALI imeombwa kuangalia upya hatua yake ya kuwatoa katika ajira watumishi waliogundulika kuwa na vyeti feki kwa kuwalipa japo kwa kuwafuta jasho.
Rai hiyo ilitolewa na Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi TUCTA Yahya Msigwa katika washa ya watalaam ya kupitia sera za Ukimwi na afya kazini.
Alisema kuwatoa katika ajira bila kuwapa chochote kunawafanya watumishi hao kuwa masikini ghafla ukizingatia kuwa katika maisha yao walitegemea  mishahara.
Msigwa alisema kuwa pamoja na TUCTA kutokuwa na tatizo na uamuzi huo wa serikali,lakini watumishi hao wengine wana mikopo kwenye taasisi mbalimbali za fedha ikiwa ni pamoja na benki.
“Kitendo cha kuwaondoa ghafla watumishi hao nafikiri hata hizo taasisi zilizokuwa zikiwakopesha zitaathirika kwa kuwa  mikopo hairejeshwi hivyo suala hilo liangaliwe,’’alisema.
Alisema ingawa ni makosa kisheria kwa mtumishi kuwa na cheti feki lakini iangalie kwa jicho la karibu kuwa watumishi hao wanawategemezi pia.
“Sisi kama TUCTA hatuna ugomvi na serikali lakini ombi letu serikali iangalie jinsi ya kuwasaidia watumishi hawa hata kuwalipa fedha kidogo kwani walikuwa watumishi wazuri tu,” alisema .
Alisema tatizo siyo wao bali ni mfumo uliokuwepo wakati wakiingia kwenye ajira zao kipindi cha nyuma.
Aidha katibu huyo aliwataka viongozi wanaohudumia matatizo ya wafanyakazi kutatua matatizo hayo kwa  kipindi kifupi.
Alisema kumekuwa na matatizo mengi ya wafanyakazi ambayo huchukua muda mrefu kutatuliwa jambo ambalo linawakatisha tama watumishi hao.
Akizungumzia masuala ya Ukimwi katibu huyo alisema ni vyema watumishi wenye maambukizi ya Ukimwi sehemu za kazi wakapewa haki zao kama watumishi wengine.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU