Utambulisho wa watawa uwe umoja na Upendo- Ask. Ruzoka

n Na Emanuel Mayunga Sumbawanga

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora Mhashamu Paul Ruzoka amewataka watawa nchini kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa wakizingatia karama za mashirika huku wakipendana na kusaidiana katika maendeleo ya jumuiya zao za kitawa.
Askofu Ruzoka ameyasema hayo hivi karibuni baada ya  Adhimisho la Misa Takatifu ya kumbariki Abate Pambo Martini OSB katika Abasia ya Roho Mtakatifu Mvimwa, Jimbo Katoliki Sumbawanga.
Akimpongeza baada ya kuchaguliwa kwake kuwa kiongozi wa Abasia ya Mvimwa, Askofu Ruzoka amemtaka Abate pambo kufanya kazi kwa moyo mkuu ulio na uvumilivu kwani amepewa majukumu mazito ambayo hakuyatarajia bali Mungu humchagua amtakae kwa ajili ya wengine ili aweze kuwa kiongozi .
“Kila cheo kina uzuri wake, magumu yake na uzito wake lakini Yesu Kristo alishatuelekeza kuonja magumu hayo. Itatokea wakati mwingine mtu akufunge mikono na kukupeleka usikotaka, hivyo tambua sana kuchaguliwa kwako kuwa Abate kwa niaba ya wanashirika, kunamkumbusha kila mtawa katika Abasia ya Mvimwa kuwa na umoja na upendo ili mumjenge Kristo Yesu katika abasia yenu ili jamii ya wakristo wapate manyunyu ya imani kutoka katika jumuiya yenu”  amesema Askofu Ruzoka
Akitoa shukrani kwa mwenyezi Mungu mbele ya waamini na viongozi mbalimbali wa kiserikali, Abate Pambo  amewashukuru watawa wenzake wa Abasia ya Mvimwa kwa kumchagua kuwaongoza akiwa kama abate wao, na kuwaomba kumpa ushirikiano wa dhati katika maendeleo ya kiroho na kijamii yatakayokuwa msaada kwa watu mbalimbali pasipo ubaguzi wala kujali dini, kabila, rangi na tofauti za kisiasa.
“Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipatia madaraka ya utumishi kwa wenzangu, pia namshukuru sana Baba Askofu Damian Kyaruzi kwa maombezi yake na zaidi sana kwa kunipatia Baraka ya uabate siku hii ya leo. Ni huyu baba ambae amenizaa katika upadri  Julai 10, 2005 na leo miaka 12 baadae amenibariki kuwa Abate akitanguliza  mafundisho ya dhati katika utume wangu, kwa kweli namshukuru sana”. amesema Abate Pambo.
Ameongeza kuwa cheo ni dhamana hivyo madaraka wanayokabidhiwa wanawiwa kuyatumia kwa hekima na busara. Amesema madaraka ni kwa ajili ya watu na utumushi, na hakuna anayepewa madaraka kwa ajili yake yeye mwenyewe.
 “Na zaidi tuendelee kutoa ushirikiano kwa serikali, vyama vya siasa, taasisi binafsi na mtu mmoja mmoja katika kuleta maendeleo ya kiroho, kiimani na kijamii. Pia tunaiomba serikali izidi kushirikiana na taasisi binafsi na mashirika ya dini katika kuboresha miundombinu katika  maeneo ya Mvimwa kama vile umeme, barabara za kudumu  na maji ili kurahisisha utoaji wa huduma za kijamii zilizopo maeneo hayo” amesema.
Abate Pambo Martini OSB Amekuwa ni abate wa tatu wa Abasia ya Mvimwa ambaye amesimikwa na Askofu Damian Kyaruzi wa Jimbo la Sumbawanga katika misa ambayo ilihudhuriwa na maaskofu kutoka majimbo mbalimbali kama vile Askofu Mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora,  Askofu Alfred Maluma wa Jimbo Katoliki Njombe, Askofu Evarist Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, Askofu Liberatus Sangu wa Jimbo Katoliki Shinyanga, na Askofu Gervas Nyaisonga wa  Jimbo Katoliki Mpanda.
 Wengine waliohudhuria maadhimisho hayo ni Abate Romei Mbota wa Abasia ya Agbam nchini Togo, Abate Oktavian Masingo wa Abasia ya Hanga, Abate Plasidius Mtunguja wa Abasia ya Ndanda,  na Abate mstaafu wa Abasia ya Hanga Thadei Mhagama. Viongozi wa serikali waliohudhuria ni pamoja na mama Anna Makinda, Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU