MSINGI WA KANISA KATOLIKI NI EKARISTI TAKATIFU

n Na Angela Kibwana, Morogoro

KANISA Katoliki kamwe haliwezi kuchoka katika kuadhimisha fumbo la Ekaristi Takatifu ambalo liliachwa na Yesu mwenyewe miaka elfu mbili iliyopita hasa siku ya Alhamisi kuu, kama kiini cha Kanisa na chimbuko lake linalomwezesha mwanadamu kupata neema ya utakaso mara baada ya kufanya toba.
Sakramenti ya Ekaristi takatifu ni utajiri wa Kanisa Katoliki katika maumbo ya mkate na divai ambapo Yesu alitoa mwili wake na damu yake kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu alipowaalika waamini kuula mwili wake na kuinywa damu yake ndio sababu ya Kanisa Katoliki kuendelea kuheshimu sakramenti hiyo kama chimbuko la Kanisa lenyewe
Wito huo umetolewa na paroko msaidizi wa parokia ya Bikira Maria wa Calmeli Dr Stan Rodrigues ambaye pia ni mtaalam katika masuala ya ndoa na familia katika adhimisho la kutoa sakramenti ya Ekaristi takatifu kwa vijana 86 iliyofanyika parokiani hapo Kihonda maghorofani jimboni Morogoro.
Dr. Rodrigues amesema kuwa inasikitisha kuona baadhi ya waamini kushindwa kutambua neema ipatikanayo katika mafumbo hayo, hali inayosababisha wengi wao kupokea sakramenti hiyo katika hali ya dhambi na wengine kushindwa kabisa kushiriki mafumbo hayo, akitolea mfano wanakwaya wa nyimbo za liturujia ambapo hali hiyo imekuwa dosari ndani ya Kanisa katika sehemu mbalimbali.
“Ninyi wanakwaya wataalamu sana kuimba na kucheza kanisani, inashangaza mmekuwa watazamaji kwa sababu mnahamasisha waamini kwa nyimbo nzuri lakini wakati wa komunio takatifu hamuendi kupokea, yale ambayo mnaimba lazima yaendane na maisha yenu ya kiroho msipoteze maana ya mafumbo haya, na utajiri wa Kanisa ambao Yesu ametuachia katika maumbo ya mkate na divai, utajiri huu una maana kubwa tuzingatie na kupokea,” Amesema Dr Rodrigues.
Aidha amesema kuwa wakati mwingine waamini wanadhani kwamba Sakramenti ya Ekaristi takatifu imewekwa kwa walio watakatifu na matajiri tu, kumbe sakramenti hiyo inamhitaji kila mmoja kuijongea akiwa katika hali ya utakataso ingawa Yesu haonekani kwa macho isipokuwa katika maumbo ya mkate na divai.
Mbali na hayo Dr Rodrigues amesema kuwa katika dunia hii kuna dini na madhehebu mengi sana, na hakuna mwanzilishi wa dini zaidi ya Yesu mwenyewe, hasa Kanisa Katoliki ambalo linaadhimisha kwa njia ya misa takatifu, hivyo ni wajibu wa wakatoliki kutetea imani yao kwa kuzingatia maneno ya Yesu siku ya alhamisi kuu akisema kuwa aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu ana uzima wa milele.
“Huo utajiri wa uwepo wa Ekaristi takatifu ndani ya Kanisa una maana tusipoteze, hakuna sakramenti kubwa kama Ekaristi takatifu japo zinachangamana, ujueni utajiri wa Kanisa Katoliki, Ekaristi ni chemchem ambayo inatupa nguvu ya kutembea katika uzima, hatuwezi kupoteza tunu hiyo. Mlango wa Kanisa Ekaristi takatifu na sakramenti zozote zile zina uhusiano wa karibu ndio maana hata mtu mgonjwa anahitaji kupewa mpako wa wagonjwa na padre,” Amesema Dr Rodrigues.
Hata hivyo kiongozi huyo wa kiroho ametoa wito kwa vijana hao 86 walioimarishwa kwa sakramenti ya Ekaristi takatifu kujenga imani kwa Yesu wa Ekaristi kiini cha imani ya Kanisa, kwa kuzingatia kanuni, mafundisho na sheria za Kanisa ikiwa ni pamoja na kuhudhuria misa za mara kwa mara katika dominika zote sanjari na ibada ya Ekaristi takatifu ambayo hufanyika siku ya alhamisi ulimwenguni pote.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU