MAGUFULI SAFI, ILA ATUPE KATIBA MPYA-ASKOFU NIWEMUGIZI


ASKOFU Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki Rulenge Ngara amesema anaridhishwa na utendaji kazi wa Rais John Magufuli kwa nia yake ya kuleta maendeleo nchini, lakini anamuasa aangalie vipaumbele vya wananchi ikiwemo kuwa na Katiba Mpya.
Akizungumza na Gazeti Kiongozi baada ya kumaliza Mkutano wa zaidi ya asasi 80 za Kiraia wa kufufua mchakato wa katiba uliofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Askofu Niwemugizi amesema kuwa, ni wazi Rais John Magufuli anapambana na ufisadi kwa ajili ya kulinda rasilimali za nchi, anahamasisha wananchi kulipa kodi kwa maendeleo ya nchi lakini atafanikiwa endapo atakuwa na Katiba ambayo ndiyo dira ya nchi.
“Ile tathmini ya mwaka mmoja wa utendaji kazi wa Rais Magufuli ni wazi ilionesha kazi alizozifanya na mafanikio na wananchi tuliridhika tukaona kuwa kweli tumepata Rais.
Kazi ya kupambana na rushwa, maadili kwa viongozi wa umma na amengine mengi, lakini ili aweze kuyaendeleza awe na katiba madhubuti. Aangalie maoni ya wananchi kupitia ile iliyokuwa inaongozwa na Warioba aone wanataka kujiongozaje ili awe na Katiba madhubuti.
Hata kama kipaumbele cha Serikali ya awamu ya tano si Katiba Mpya lakini Katiba hiyohiyo ndicho kipaumbele cha watanzania. Ikiwa Rais amewekwa madarakani na wananchi ana wajibu wa kuangalia vipaumbele vyao. Awasikilize wananchi.
Ieleweke kuwa, si uchochezi kuhamasisha ama kushawishi Serikali ianze mchakato wa Katiba Mpya kwani ni kazi ya asasi za kiraia kuchochea maendeleo. Hatuwezi kupata maendeleo kama hatuna dira ya Taifa. Hatuwezi kufanikiwa kama Taifa kama tunaongozwa na Katiba yenye mapungufu,” amesema Askofu Niwemugizi.
Amesema yeye kama kiongozi wa dini alishapinga Katiba pendekezwa kwani ilikuwa haikidhi mahitaji wa wananchi na ilikiuka maadili ya nchi pamoja na imani yake kwani ilikuwa haielezi wazi mipaka ya uongozi, uhai wa mwanadamu kwamba unaanzia tumboni.
Amesema Katiba lazima iwe imebeba maoni ya wananchi ambayo yameainishwa kutokana na namna wanavyotaka kujiongoza.
“Katiba si mapendekezo ya Bunge ingawa wabunge ni wawakilishi wa wananchi, lakini lazima wasikilize wananchi wanataka nini. Ninasisitiza haya kwani hatutaki Katiba itakayochezewa.
Wabunge hawana mamlaka ya kurekebisha Katiba kwa mahitaji yao bali lazima iwekwe kikatiba kuwa, marekebisho ya Katiba ama kipengele katika Katiba kinaweza kurekebishwa kwa mamlaka ya wananchi. Hatutaki Katiba inayochezewa.
Wananchi ndiyo watoe maoni kuhusu kubadilisha Katiba si bunge. Vitu vya msingi lazima wapewe ridhaa na wananchi,” amesisitiza.
Ameziasa taasisi za kiraia kuacha kuogopa kuzungumza yale mahitaji muhimu ya wananchi kwani ni wajibu wao. Wasiogope kuitwa wachochezi kwa kutaka maendeleo ya nchi.

 Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU