UBINAFSI NA TAMAA VINAITESA DUNIA

Misingi ya ukweli imefichwa
n Na Sarah Pelaji, Dar  es salaam

BAada ya dunia kuendelea kukumbwa na machafuko ya mauaji, utekaji, vita, kuumizana, na kunyanyasa watoto, Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Fransisko amesema viongozi wasiishie tu kuona huruma juu ya mateso ya watu bali watafute chanzo na suluhisho ili dunia iwe mahali salama pa kuishi.
Papa Fransisko amezungumza hayo wakati alipohutubia waamini kwenye sala ya malaika wa Bwana Septemba 20 mwaka huu katika Viwanja vya Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro Vatikani.
“Waamini na viongozi wasiwe watazamaji, wanaosikitishwa na matukio mbalimbali yanayotendeka sehemu mbalimbali za dunia, bila kujishughulisha hata kidogo kutafuta chanzo na suluhisho ili kusaidia unyanyasaji wa mwanadamu duniani kukoma.
Ni vyema, ikiwa kama waamini watajiuliza swali la msingi, ikiwa kama kweli wana huruma, wanaweza kusali na kujishughulisha kadiri ya nafasi na uwezo wao yale wanayoyaona yakitangazwa kwenye vyombo vya mawasiliano ya jamii. Haitoshi kuwaonea watu huruma, bali kuchukua hatua madhubuti ili kuwasaidia.”
Kufuatia rai hiyo iliyotolewa na Baba Mtakatifu, baadhi ya Maskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania wamesema kuwa, dunia inateswa na ubinafsi, madaraka ya mali na utawala usiojali wengine.
Akizungumza na Gazeti Kiongozi, Askofu wa Jimbo Katoliki Geita Mhashamu Flavian Kassala amesema kuwa ubinafsi umewasababisha watu hususani viongozi kujiona wanastahili kuliko wengine.
“Ndiyo maana wanasahau sura ya Mungu ndani wa watu wengine, wanasahau utu wa mwanadamu wenye thamani isiyopimika. Wanajihesabia haki hata kama wamekosea, ubinafsi unawasahaulisha kuwa wana mapungufu, wanahitaji kusamehe na kusamehewa.
Kuanzia mtu binafsi kuelekea kwenye taasisi inakuwa mbaya zaidi pale taasisi inapogubikwa na ubinafsi unaosababisha isahau mahitaji msingi na haki za wengine.
Anayeongoza taasisi anachochea dhuluma, uonevu na kunyanyasa wengine kwa sababu tu ana nguvu. Hajali utu wa watu wake, anashirikiana na wengine kunyanyasa watu kwa kujihesabia haki ya madaraka na mali. Hicho ndicho chanzo cha mateso na maumivu ya watu duniani,” amesema Askofu Kassala.
Aidha ameeleza kuwa, ubinafsi unaanzia kwa mtu binafsi, taasisi ndipo uende kwenye mataifa ambapo wachache wanapewa dhamana ya kuongoza wengi. Watu hao wakiwa na ubinafsi, wanapitisha sera zilizo na ubinafsi.
“Tunateseka kwa sababu watawala na viongozi wamekataa ukweli kwamba kuna masikini wanahitaji kusaidiwa, wanatunga sera zilizo na ubinafsi ndiyo maana kuna biashara za unyonyaji na maamuzi yaliyogubikwa na ubinafsi wa kupendelea upande mmoja.
Tumekataa misingi ya kweli (Fundamenta truth) unaotupa miongozo ya namna ya kuishi ambayo kwa asili Mungu alishaiweka.
Msingi wa ukweli kuwa huyu ni mama, baba, mzazi wangu ama mtu mwingine mwenye utu ni ukweli.
Tumefuta  ukweli huo, ndiyo maana tunawafanyia  mambo ambayo hayastahili kwa sababu tumekataa watoto na tunawaona watoto sawa na watu wazima, tunawafanyia ukatili, tunawanyanyasa wazazi wetu, tunaumizana kwa sababu tumefuta misingi ya kweli. Aliye na utu anafahamu utu wa mwingine hawezi kumuumiza na hili halihitaji mtu awe na dini Fulani,” Amefafanua Askofu Kassala.
Hata hivyo amesema ukweli, utu na kuthamini ubinadamu unajengwa na kuimarishwa zaidi na chachu ya imani hususani chachu ya Injili. Ndiyo maana anasisitiza jamii hususani dini kuwekeza kwenye imani, malezi na maadili kwa watoto.
“Katika imani kuanzia kwa watoto wetu, tutapoteza imani, kujua ukweli (Fundamental truth).Inaweza ikaenda kwenye mataifa, na mtu huyu ana madaraka makubwa. Wao kama viongozi kwa pamoja wanaweza kupitisha sera za kibaguzi, za unyonyaji na kusahau wengine. Tumebaki tunapiga kelele juu ya haki za binadamu, kusaidia masikini, lakini, je, tunatenda? Kama mtu binafsi ninatenda? kama taasisi inatenda? kama mataifa yanatenda?.
Tukitenda tutashinda, lakini tukibaki tunaongea tu, kunyoosha vidole, sera zitakuwa nzuri sana lakini hazina watendaji. Na sera zitakuwa zimetawaliwa na ubinafsi uleule kama vile mwanadamu alivyoumbwa kwa sura na mfano wa Mungu lakini akaamua kufunga macho akaisahau ile sura ya Mungu ndani mwake na kwa wengine.
Ubinafsi unaleta biashara zisizo na usawa, wizi, mauaji, vita, umiliki wa silaha.
Kabla ya imani iko miongozo ambayo Mungu ametuwekea ndani mwetu. Mfano kuelewa kuwa kuua ni dhambi haihitaji uongoke katika imani, kuelewa kwamba wahitaji wanahitaji msaada, kuelewa haki za binadamu maana binadamu na haki na mahitaji msingi, huhitaji dini! Dini inatupa mwelekeo na hatua nyingine ya hayo ambayo ni ya kawaida. Hata Tamko la haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa halina itikadi za dini, kabila wala taifa.
Ni la haki za msingi za binadamu kwani kwa asili anahitaji mavazi, chakula, anahitaji kuishi. Hayo hayasubiri mtu awe na dini, ni fundamental truth. Tuache ubinafsi, tusafishe dhamiri, tuwe na utu,” Amesema.

Askofu Niwemugizi; Mtu asiyemwamini Mungu ni hatari, anafanya lolote
Kwa upande wake Askofu wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara Mhashamu Severine Niwemugizi amesema kuwa, ni kweli hata katika taifa letu kuna matatizo ya utekaji nyara hususani watoto, kuua watu, dhuluma, kuteswa n.k. lakini yote amesema ni kukubali kutawaliwa na ubinadamu, tamaa na kumuacha Mungu.
“Ukisoma Wagalatia 5 Mtume Paulo anaeleza vizuri sana akisema kuwa mwili hushindana na roho. Mwanadamu akiruhusu tamaa ya mwili kushinda tunda la roho anakuwa na vurugu nyingi.
Anakuwa na uchu wa madaraka yasiyojali wengine, anakuwa na tamaa ya mali, umaarufu kwa kunyanyasa na kuumiza wengine.
Tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uadilifu, utu wema, fadhili na uaminifu. Kumbe tunahitaji watu (waamini, wananchi) pamoja na viongozi wanaoongozwa na Roho ya Mungu. Ukikosa matunda ya Roho wa Mungu lazima ufanye mambo kinyume na Amri za Mungu na kuficha dhamiri kwani unatawaliwa na tamaa zako binafsi kwa kutesa wengine,” Amesema Askofu Niwemugizi.
Amesema kuwa, ingawa yapo mataifa yasiyomwamini Mungu (secular) lakini yanathamini utu wa mwanadamu. Pia yapo mataifa kama Tanzania yanayo mwamini Mungu lakini halijaweka maadili kikatiba hivyo haki inaweza kuvunjwa  na kubakia kusema taifa hili linamwamini Mungu wa maneno.
Tuweke vipaumbele vyetu vya kujenga taifa lenye amani kikatiba kwamba hakuna mtu anaweza kukiuka.
Taifa letu lifundishe maadili kuanzia shule za awali ili kulea dhamiri zinazoheshimu utu wa mwanadamu. Dhamiri nyoofu inaheshimu utu, haki, usawa, inajali wanyonge, inasikiliza, inakosoa na kukubali kukosolewa, inakubali msamaha na kumheshimu Mungu. Anayeenda kinyume na hayo anaweza kufanya mambo ya ajabu,” Amesisitiza Askofu Niwemugizi.

Askofu Banzi- Uvuguvugu wa imani  chanzo cha matatizo

Akizungumzia juu ya umwagaji damu duniani, Askofu wa Jimbo Katoliki Tanga Mhashamu Anthony Banzi  amesema kuwa, uvuguvugu wa imani ndiyo chanzo cha yote kwani mwenye imani ana hekima, anamuogopa Mungu.
“Inaelekea hatujainjilisha vya kutosha. Tufanye uinjilishaji wa kina ili watu wawe na hofu ya Mungu, wajali utu wa mwanadamu pamoja na thamani yake.
Wakristo waliobatizwa leo hii wanaacha imani yao inayofundisha msamaha, kusikiliza dhamiri, kuheshimu uhai. Wapo waliobatizwa na leo hii wanajiita wakristo tena wa Kanisa Katoliki lakini wapo vuguvugu, mguu mmoja ndani ya imani mwingine nje.
Ni wabinafsi wa kujilimbikizia mali na madaraka. Chako ni changu , changu ni chetu. Hapana tuendelee kuwapa mafundisho ya imani ili waachane na ubinafsi uliopindukia ambao ndicho chanzo cha umwagaji damu duniani.
Tusisitize uinjilishaji mpya kwa kila mtu. Hakuna mtu asiyehitaji Katekisimu endelevu. Tuwe na mikakati mbalimbali ya kuwekeza kwenye imani ili tutengeneze taifa linalomcha Mungu. Watu wenye huruma wanaoguswa na mahangaiko ya jirani zao.  Hiyo ndiyo kazi yetu viongozi wa dini,” Amesisitiza Askofu Banzi.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU