KANISA KATOLIKI KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI




IDARA ya Afya ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) imefanya mkutano wa Mwaka ili kutathmini utendaji kazi pamoja na kujadili mbinu za kuboresha utoaji huduma za Afya katika hospitali na vituo vya Afya vinavyomilikiwa na Kanisa Katoliki nchini.
Mkutano huo umefanyia hivi karibuni katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Kurasini jijini Dar es Salaam ukijumuisha Makatibu wa Afya Jimbo, madaktari wa hospitali zinazomilikiwa na  Kanisa Katoliki, wasimamizi na Wakuu wa Vituo vya Afya vya Kanisa Katoliki.
Akifungua mkutano huo Mwenyekiti wa Kamati ya Afya TEC Askofu Mkuu Jude Thadeus Ruwaich amesema kuwa anatumaini mkutano huo utaleta matokeo yenye tija katika kuboresha utoaji wa huduma ya afya kwa hospitali na vituo vya afya chini ya Kanisa Katoliki kwa wananchi.
Ajenda kuu ya mkutano huo ni "Kuimarisha uwezo wa Vifaa vya Afya katika hospitali na vituo vya Afya vya Kanisa Katoliki kutoa huduma  bora: Kutathmini uwezo, fursa, udhaifu, changamoto na kuangalia suluhisho" kwa lengo maalum la kubaini njia za ubunifu juu ya utoaji wa huduma za afya, upatikanaji wa huduma za afya bora, fedha ambazo ni moja ya mikakati ya kuendeleza mifumo ya utoaji wa huduma za afya na kuboresha mawasiliano kati ya TEC na taasisi za afya katika majimbo.

“Ni matumaini yangu kuwa majadiliano yetu yatatusaidia kufikiria kwa kiasi kikubwa juu ya kile tunachokifanya, jinsi tunavyofanya ili mwishowe tupate matokeo yaliyokusudiwa ambayo yanaboresha upatikanaji na ubora wa huduma za afya tunayozitoa.

Wakati wa mkutano wa mwaka jana, tulijitolea kuboresha upatikanaji wa huduma za afya bora katika taasisi za afya za Kikatoliki. Mkutano huu pia utajadili hali ya utekelezaji wa hatua za vitendo ambazo tulikubaliana wakati wa mkutano wa mwisho.

Nimeambiwa kuwa wakati wa mkutano wa mwaka huu, Tanzania Christian Madical Associations (TCMA) ilijadili pia changamoto ambazo tunakabiliwa nazo katika kutoa huduma za afya kwa jamii kama vile masuala yanayohusiana na rasilimali za afya, fedha, mikataba ya watumishi na ubora wa huduma. Pia ulipendekeza baadhi ya njia za kutatua.

Hivyo ninawahimiza kujadili kwa kina na kuzipitia ili kuhakikisha kuwa watu wote wanapata huduma bora za afya zinazotolewa katika Taasisi za Afya Katoliki.”

Mkutano huo umewashirikisha wakurugenzi wa afya majimboni, wakuu wa vitengo pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya afya wakiwemo wakurugenzi na wakuu wa Idara mbalimbali za Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
Baadhi ya maadhimio ya mkutano huo ni pamoja na kutumia teknolojia katika kukusanya mapato ya hospitali, kuzingatia maadili ya Kanisa Katoliki katika utoaji huduma, kuhamasisha wananchi kuwa na bima ya afya ili kuwa na uhakika wa kupata matibabu.
Aidha kuibua mikakati itakayohakikisha utoaji wa huduma za afya utakuwa endelevu na kuwa na majadiliano na serikali ili mpango wa kutoa huduma za afya  bure kwa makundi maalumu  yasiathiri Hospitali za Kanisa na vituo vyake kuendelea kutoa huduma za Afya kwa wananchi.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU