WAAMINI OMBEENI TAASISI ZA KANISA- ASK. MSONGANZILA

n Na Veronica Modest Musoma
WAAMINI wa Kanisa Katoliki Jimbo Katoliki Musoma wamekumbushwa  kuombea taasisi zote za Kanisa zinazotoa huduma katika jamii ili ziweze kuendelea kutoa huduma hizo kwa jamii kiroho, kielimu na kiafya kwa kuwa lengo la taasisi hizo ni kumuhudumia mwanadamu bila ubaguzi.
Hayo yamesemwa  hivi karibuni na Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila wakati wa ibada ya kumshukuru Mungu kwa Parokia ya Kiabakari kwa kutimiza miaka 25 tangu kuzinduliwa rasmi mwaka 1992.
Askofu Msonganzila amewakumbusha waamini wa Jimbo hilo kuwa wanaposherehekea miaka 25 ya kuzaliwa kwa parokia yao wasisahau kuziombea taasisi zote zilizopo chini ya Jimbo na Parokia hiyo ya kiabakari ikiwemo shule, Zahanati na huduma zote za kuroho kwa kuwa kituo cha Kiabakari  ni kituo cha kikanda cha Lango la huruma  ambacho mahujaji  mbalimbali wanafika kwa ajili ya kusali na kutoa shukurani kwa Mwenyezi Mungu.
 “Huduma zinazotolewa na taasisi zetu zilizopo chini ya Jimbo letu la Musoma zina lengo la kumuhudumia mwanadamu, na ndiyo maana taasisi hizi zinahudumia bila ubaguzi na zinaitwa kumbakumba, hivyo nawaomba sana waamini tuweke mikakati wa kuwaombea watu wa mataifa ili waendelee kuziombea taasisi zetu” amesema Askofu Msonganzila.
Askofu Msonganzila amewaomba waamini kuhakikisha wanasimama imara katika imani yao, na kutokubali  majaribu waliyokumbana nayo ndani ya miaka 25 kuwakatisha tamaa katika kuitetea imani yao, kwa kuwa kila penye mafanikio kuna changamoto pia.
Amesema kuwa atajitahidi kuhakikisha ifikapo 2018 kituo cha hija cha Kiabakari  kinatangazwa kuwa kituo cha hija cha Kitaifa, baada ya kupata  baraka zote kutoka kwenye kikao cha Maaskofu  kitakachofanyika  hivi karibuni Jijini Dar Es Saalam.
 Kwa uapande wake Paroko wa Parokia ya Kiabakari Padri Wojciech Koscielniak amesema kuwa wanamshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai kwa kusherehekea miaka 25 ya Parokia hiyo baada ya kutangazwa rasmi na Hayati  Askofu Justine Samba Agosti 21 mwaka 1992, ambapo katika risala yake aliomba siku moja kituo hicho cha hija kiweze kutangazwa kituo cha Hija cha Kitaifa kwa kuwa watu wa Mataifa mbalimbali wanafika katika kituo hicho kwa ajili ya kuhiji. 


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU