KUTUKUKA KWA MSALABA WA BWANA WETU YESU KRISTO

KAnisa huadhimisha Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo tarehe 14 Septemba kila mwaka. Katika Kanisa la Mashariki Sikukuu hiyo inatukuzwa sana na huadhimishwa kama sherehe. Tumeona vema kueleza kifupi historia ya Sikukuu hiyo.

Kifo cha Msalaba
Adhabu ya kumsulubisha mhalifu kufa msalabani ilikuwa ya kikatili  sana na yenye maumivu  makali sana. Mhalifu alikufa polepole kwa mateso na aibu kubwa sana kutokana na kusulibiwa akiwa uchi.  Adhabu hiyo iliyoanzia sehemu za Asia-ndogo ilienea hata kufika magharibi. Wagiriki au Wayunani hawakuitumia sana adhabu hiyo kwaniilidhalilisha na kuwapa mateso sana waliopata; lakini Warumi waliitumia mara nyingi  kwa watumwa katika mataifa ambayo yalikuwa chini ya dola yao. Wahalifu waliokuwa magaidi, wevi sugu na waliopinga serikali walipata adhabu hiyo bila huruma.
Kwa kawaida wahalifu waliopata adhabu ya kutundikwa msalabani walipigwa  kisha walibebeshwa gogo la msalaba mpaka walipofika mahali waliposulubiwa. Hapo kulikuwa limesimikwa tayari gogo la kumsimamisha mhalifu. Wahalifu walivuliwa nguo zao na kutundikwa msalabani. Waliachwa vile katika mateso makali wakiteseka kwa baridi hasa wakati wa majira ya baridi. Wakati wa joto kali waliteseka kwa joto kali, kiu na njaa. Pengine waliopita kando, waliwachekelea na kuwatukana wahalifu hao.
Ingawa Bwana Yesu hakuwa na kosa lolote, alipata adhabu hiyo kwa sababu Wayahudi walidai asulubiwe. Wayahudi wenyewe walikiona kifo cha kutundikwa msalabani kuwa kifo cha laana kama ilivyoandikwa na Mose katika Kumbukumbu la Torati kwamba “aliyetundikwa amelaaniwa na Mungu”. Kwa hiyo alitakiwa kuzikwa siku hiyohiyo alipokufa bila kuchelewa; la sivyo alisababisha unajisi katika nchi(Rej Kumb 21:22-23).

Msalaba wa Kristo
Aliposulubiwa Yesu, msalaba wake haukufikiriwa kuwa mti  wa maana, bali kama gogo au mti uliotumika kama adhabu kwake, ingawa Mitume na wengine walifahamu kwamba hakustahili adhabu ile; hakuwa na kosa. Mti wa msalaba wa Yesu uliachwa tu.
Hata hivi kifo chake Yesu msalabani kilipata kuwa ishara ya sadaka na ukombozi wa watu tangu wakati wa Mitume. Mtume Paulo aliweza kufundisha na kuandika: “Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulubiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu”(1Kor 1:22-24).
Tena Mtume Paulo katika waraka wake kwa Wakaristo wa Galatia aliweza kuandika kwa imani na uhakika: “Lakini  mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu chochote ila Msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu. Kwa sababu kutahiriwa si kitu wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya” (Gal 6:14-15).
Basi, kifo cha Yesu Kristo Msalabani ni kifo cha sadaka ya kuwakomboa wanadamu; wote wanaomsadiki wanakuwa viumbe vipya. Kwa hiyo  mti wa Msalaba wake umekuwa na thamani kubwa katika imani ya Kikristo tangu wakati wa Mitume.

Kutukuka kwa Msalaba
Kadiri ya mapokeo ya Alexandria ni kwamba Mtakatifu malkia Helena alipokwenda kuhiji Yerusalemu aliubaini na kuuvumbua Msalaba wa Yesu Kristo tarehe 14 Septemba 320. Kumbe wakati huo huo makanisa makubwa yakawa yanajengwa juu ya kilima cha Golgotha. Kanisa moja lilijengwa pale aliposulubiwa Yesu na jingine pale alipozikwa. Kanisa lililojengwa pale aliposulibiwa huitwa Kanisa la Msalaba na  lile lililojengwa pale alipozikwa huitwa Kanisa la Ufufuo. Makanisa hayo yote mawili yalitabarukiwa siku moja, tarehe 13 Septemba, 335 kwa vile yalivyokuwa jirani. Siku iliyofuata, tarehe 14 Septemba 335, Msalaba wa Yesu, ambao Mtakatifu malkia Helena alikuwa ameuvumbua, uliletwa kwa heshima na fahari kubwa na kuwekwa mahali pa heshima ili waamini waweze kuutukuza kwa ibada kubwa.
Matukuio hayo ndiyo chanzo cha Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba kwani kila mwaka tendo la kuutukuza msalaba liliadhimishwa mjini Yerusalemu na baadaye limeenea sehemu nyingine. Tayari katika karne ya tano Sikukuu hiyo ilikuwa inaadhimishwa katika kanisa kuu la Konstantinopoli. Mwishoni mwa karne ya saba Sikukuu hiyo ilikuwa imepokewa na kuadhimishwa pia katika kanisa la Roma. Katika makanisa makuu hayo ya Yerusalemu, Konstantinopoli na Roma walikuwa na vipande vikubwa vya Msalaba wa Yesu.  Tarehe 14 Septemba ilikuwa kawaida katika makanisa hayo kuvitoa kwa ibada vipande hivyo vya mti wa Msalaba wa Bwana ili waamini waweze kuviheshimu na kuutukuza kwa ibada. Adhimisho hilo liliitwa kutuzwa au kutukuka kwa Msalaba.

Misa ya Sikukuu
Wazo kuu la Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba ni kifo chake Yesu Kristo ambacho kimewaletea ukombozi watu wote. Wimbo wa mwanzo ni maneno ya Mtume Paulo kwa Wagalatia ambayo tumeyanukuu hapo juu. Kifo cha Yesu juu ya Msalaba kimeleta wokovu, maisha halisi ya neema na ufufuo wetu.
Katika sehemu ya mwanzo ya Sala ya Ekaristi, yaani Utangulizi,  tunaona ukuu wa mti wa Msalaba wa Yesu Kristo ambao ni kinyume cha mti wa bustani ya Aden. Mti ule wa bustani ya Adeni ulikuwa chanzo cha dhambi kwa wazee wetu Adamu na Hawa, wakapoteza uzima wa kimungu waliokuwa nao. Kumbe  kwa njia ya mti wa Msalaba Yesu, Kristo ametuletea neema yaani uzima wa Kimungu ndani yetu; tukombolewa.
Pale yalipoanzia mauti yaani dhambi, na uzima uanzie hapo hapo katika mti, na yule aliyeshinda katika mti, ashindwe pia katika mti wa Msalaba. Shetani alifautu kuleta mauti kwa kupitia mti wa bustani, kumbe kwa njia ya mti wa Msalaba uzima na ufufuko umepatikana. Mti wa Msalaba umekuwa mti wa ushindi kwa njia ya Yesu Kristo.

Tuutukuze msalaba
Kila tunapoadhimisha Liturujia tunaanza  kwa kupiga Ishara ya Msalaba. Kwa ishara hiyo tunaumbuka ukombozi wetu. Kwa kawaida hata katika Sala za kila siku, Mkristo inampasa kuanza kwa Ishara ya Msalaba na kumaliza kwa ishara hiyo. Hapana budi kufanya ishara hiyo vizuri na kwa ibada, isije ikawa tu mazoea.

Tena ni vema kuwahimiza Wakristo kuwa na msalaba angalau msalaba moja katika kila nyumba. Nyumba ya Mkristo inayokosa msalaba inakosa kitu muhimu sana. Msalaba ulio na sanamu ya Bwana Yesu ubarikiwe na kuhani na uwekwe barazani au sebuleni ili kuwa ishara ya imani yetu na uwakinge katika mabaa na kuwaletea Baraka wote. Baraka iwafikie  siyo tu wanaoishi katika nyumba, bali hata wageni na wote waingiao katika nyumba hiyo. Kila Mkristo asiuonee aibu Msalaba wa Kristo bali aone fahari kuwa nao.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU