MAPADRI WENYE TAMAA WAONYWA



ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora Mhashamu Paulo Ruzoka amewaasa mapadri kukaa chonjo na mali za ulimwengu huu unaopita ili wasiingie matatani na kuipoteza imani yao safi.
Rai hiyo ameitoa hivi karibuni katika adhimisho la Misa Takatifu na kutoa Sakramenti ya Daraja Takatifu ya Upadri kwa Shemasi Peter Fabian Kulwa hivi karibuni.
Akitoa mahubiri yake katika Kanisa la Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi Kipalapala Tabora, Askofu Mkuu Ruzoka amewataka mapadri kupeleka upendo wa Kristo kwa watu wote bila ya ubaguzi wowote.
Amesema Mtakatifu Matayo mtume na mwinjili alikubali kuacha kazi yake nzuri ya mshahara akakubali kumfuata Kristo, vivyo hivyo na padri anapoitwa hana budi kuacha yale yote yasiyoendana na wito mtakatifu wa upadri na kumsikiliza Kristo anachomtaka akifanye kwa watu wake.
Pia Askofu Mkuu Ruzoka amesema wito wa upadri ni zawadi toka kwa Baba Mungu ambayo padri anazawadiwa bila mastahili yake mwenyewe. Na kama mtu atasema nataka kuwa padri bila kuitwa na Kristo mwisho wa padri huyo huwa ni kukata tamaa.
“Padri anaitwa kuadhimisha makuu ya Mungu na si vinginevyo, hivyo ni vyema ajikabidhi kwa Kristo, na awe tayari kuadhimisha Sakramenti ya Upatanisho ambayo ndio Kristo alionesha kwa Mtakatifu Matayo na kumwambia amfuate.”
Aidha katika mahubiri yake Askofu Mkuu Ruzoka amesema sisi binadamu ni dhaifu hivyo ni vyema tuwe tayari kuhurumiana na kusameheana ili upendo wa Kristo umfikie kila mwanadamu na kuachana na moyo wa kulipiza kisasi.
Padri Peter Fabiani Kulwa anakuwa padri wa tatu tangu kuanzishwa kwa parokia ya Mtakatifu Yosefu Kipalapala.  Pamoja na mambo mengine parokia ya Kipalapala imemzawadia padri mpya gari dogo aina ya Tayota Lav 4 kwa ajili ya uchungaji.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU