“DINI INAYOHUBIRI FEDHA KULIKO HUDUMA HAIFAI”

n Na Pascal Mwanache
MKUTANO Mkuu wa 17 wa Shirikisho la Masista Wakatoliki nchi za Afrika Mashariki na Kati (ACWECA) umefunguliwa hivi karibuni jijini Dar es salaam na kuandika historia nchini, ambapo ufunguzi huo umehudhuriwa na Rais wa Baraza la Kipapa la Maisha ya waliowekwa wakfu Mwadhama Joao Kardinali Braz de Aviz kutoka Vatikani.
Katika Misa Takatifu ya ufunguzi wa mkutano huo Kardinali Joao amewaasa watawa wanaounda shirikisho hilo kutomezwa na tama ya fedha katika utume wao na badala yake wajikite katika kutoa huduma bila kutegemeamalipo ya hapa duniani.
Amesema kuwa watawa wanapaswa kuwa kimbilio la watu hasa wale wanaoteseka na kutengwa katika jamii, kwa kuwa mamlaka waliyonayo watawa ni mamlaka ya kuhudumia wanyonge kwa kuliishi Neno la Mungu.
“Fedha inaamrisha kilakitu. Fedha ina nguvu na msukumo mkubwa katika ulimwengu wa leo. Fedha inasababisha vifo, silaha, hofu na vita. Hatupaswi kuitumikia fedha, bali tunapaswa kumtumikia Mungu” ameeleza.
Aidha amesema kuwa dini inayohubiri fedha kuliko huduma haiwezi kuwa dini ya kweli,na kusema kuwa hiyo ni changamoto kubwa katika ulimwengu wa leo. Pia amesema kuwa haitoshi kwa mtawa kuishia katika kusoma Biblia tu bali mtawa anapaswa aishi mtindo wa maisha kama mkristo, kama walivyoishi wafuasi wa Kristo.
Pia amewakumbusha watawa kuishi fadhila na karisma za waasisi na waanzilishi wa mashirika yao badala ya kujikita katika mambo mapya yasiyoendana na uhalisia wa maisha ya utawa.
Wakati huo huo Waziri wa Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu Jenister Mhagama amesema kuwa uwepo wa Umoja wa Masista Afrika Mashariki na Kati umesaidia maendeleo ya nchi hizo na kuwa sehemu muhimu ya kuimarisha Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Amesema kuwa kupitia mashirika hayo ya kitawa, miradi mbalimbali nahuduma za kijamii imetekelezwa na hivyo kuharakisha maendeleo ya nchi zaukanda huo, huku huduma hizo zikitolewa bila kujali tofauti za dini, rangi na hali za maisha.
Pia  ameziomba Taasisi mbalimbali za dini za Kanisa Katoliki nchini ziendelee kukuza maadili na utawala bora ili kuliepusha taifa dhidi ya rushwa, dawa za kulevya, ukimwi na viongozi wasiokuwa waadilifu.
“Mchango mkubwa unaotolewa na watawa ni bidii yao ya kufanya kazi ya kutoa huduma nchini. Uwepo wa masista umekuwa chachu ya maendeleo ya Kanisa mahali popote, hakika wao wamekuwa nguzo imara. Tunawaomba msimamie maadili katika taasisi zenu ili kukuza utawala bora na maendeleo ya watu” ameeleza.
Mkutano huo wa 17 wa  Shirikisho la Masista Wakatoliki nchi za Afrika Mashariki na Kati (ACWECA) umefunguliwa Agosti 26, 2017 na unatarajiwa kufanyika hadi Septemba 2, 2017 katika kituo cha mikutano cha Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Kurasini jijini Dar es salaam.
Umoja huo unaundwa na nchi 9 ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Malawi, Zambia, Ethiopia, Sudani ya Kusini, Sudani na Eritrea. Baadhi ya wageni waliohudhuria ufunguzi wa mkutano huo ni pamoja na Askofu wa Jimbo Katoliki Bunda Mhashamu Renatus Nkwande, Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mhashamu Eusebius Nzigilwa, na Balozi wa Papa nchini Askofu Mkuu Marek Solczyński.

Wakati huo huo wajumbe wa Mkutano Mkuu wa ACWECA wamefanya uchaguzi na kumchagua Sista Cesilia Njeri wa Shirika la Wadada wadogo wa Mtakatifu Fransisko wa Asizi kuwa Mwenyekiti mpya wa ACWECA.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU