WANANCHI KENYA WATAHADHARISHWA

n KENYA
BARAZA la Maaskofu Katoliki Kenya limewataka wananchi nchini humo kuweka kando tofauti zao ili kwa pamoja waweze kujenga nchi yao.
Baraza la Maaskofu Kenya limekishukuru Chama cha upinzani cha NASA kwa kufikisha malalamiko yake ya uchaguzi kwenye Mahakama kuu badala ya kesi hiyo kusikilizwa na kutolewa hukumu na raia mitaani, hali ambayo ingepelekea machafuko makubwa ya kisiasa nchini Kenya.
Uamuzi huu umeiongezea Mahakama kuu sifa ya kuweza kutatua migogoro ya wananchi katika hali ya usalama na amani. Maaskofu wanawaalika wananchi wote wa Kenya kuzingatia utawala wa sheria kwa kukubali na kutekeleza maamuzi yaliyotolewa na Mahakama kuu. Uhuru, heshima na haki ya Mahakama kuu vinapaswa kuheshimiwa hata kama kimsingi mtu hakubaliani na maamuzi yaliyotolewa na Mahakama kuu.
Maaskofu wanampongeza Jaji Mkuu David Maraga kwa maamuzi aliyoyafanya na kwamba, sasa changamoto iliyoko mbele yao ni kushikamana ili kujenga taifa kwa kujikita katika nia njema. Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linawasifu na kuwapongeza wananchi wote waliojitokeza kupiga kura, kwa amani na utulivu na kuwataka tena kujitokeza kwa wingi wakati wa kupiga tena kura ya marudio hapo tarehe 17 Oktoba 2017.
Wananchi wa Kenya wanahimizwa kufanya kampeni za kistaarabu, zinazowajibisha, ili hatimaye, kuwapata viongozi watakaosukuma mbele gurudumu la maendeleo ya wananchi wote wa Kenya. Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linavialika vyama vyote kushirikiana na Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini Kenya, IEBC sanjari na kuiachia uhuru wa kuweza kutekeleza majukumu yake pasi na kuingiliwa na wanasiasa.
Badala ya kuishambulia Tume huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya, wanasiasa watoe ushauri wa namna ya kuboresha utendaji wao wa kazi na kwamba, busara haina budi kutumika kwani si mambo yote yanaweza kufanyiwa marekebisho.
Maaskofu wanaunga mkono mchakato wa mabadiliko kwenye Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini Kenya, IEBC ili kuwajengea wananchi imani katika mchakato mzima wa uchaguzi wa marudio hapo tarehe 17 Oktoba 2017.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU