CRS YAWARAHISISHIA HUDUMA YA MAJI WAKAZI KARATU




SHIRIKA la Catholic Relief Services (CRS) kwa kushirikiana na  mdau wake Grundfos Lifelink  A/S kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii Jimbo Katoliki Mbulu (DMDD) limebuni mradi wa kipekee na wa kwanza nchini Tanzania unaolenga kubadilisha mfumo wa  kulipia maji kutoka malipo ya baada kwa sasa na kuja kwenye malipo ya kabla kwa kutumia vocha katika utoaji wa huduma ya maji.

Kwa mujibu wa Meneja mradi kutoka CRS Mhandisi Ephraim Tonya, mradi huo unalenga kuhudumia watu zaidi ya 11,604 kwa awamu ya kwanza kutoka wilaya ya Karatu mkoani Arusha ulioanzia katika kijiji (1)  cha Gongali na mitaa minne (4) Karatu mjini ambayo ni Mjini kati, Bomani, Mazingira bora na Sabato vinavyohudumiwa na bodi ya  KAVIWASU na kijiji cha Qaru kinachohudumiwa na bodi ya ENDAWASU.

Mhandisi Tonya ameeleza kuwa lengo la mradi huo wa kulipa maji kabla ni kuwezesha  udumisho na uendelevu wa miradi ya maji, upatikanaji wa huduma muda wote mtumiaji anapohitaji, kuongeza ufanisi katika ufanyaji kazi wa miundombinu ya maji, kuongeza vyanzo vipya ya maji pamoja na kuboresha vyanzo vilivyopo.

Amesema mara nyingi katika bodi za maji kumekuwa na upotevu wa mapato yatokanayo na huduma za maji, hivyo mradi huo wa malipo kabla kwa kutumia vocha utasaidia kupunguza upotevu huo kutoka asilimia 39 kwa bodi ya maji ya KAVIWASU na asilimia 34 kwa bodi ya maji ya ENDAWASU kushuka kwa asilimia 20 bodi zote.

Tonya amesema kuwa upotevu huo husababisha miradi ya maji kutokuwa endelevu na mingine kufa na kusababisha waathirika wakuu ambao ni watoto chini ya miaka 5 kukosa afya na kudumaza akili zao.

Mhandisi Tonya amefafanua kuwa mradi huo umekuwa na mafanikio makubwa ambapo mradi wa KAVIWASU uliokuwa unakusanya sh.30,000 kwa mwezi kwa kituo cha umma awali kwa malipo baada, kwa sasa unakusanya sh.laki mbili kwa mwezi kwa mfumo wa malipo kabla.

Amefafanua kuwa fedha hizo ambazo hutokana na mradi zinawekwa katika akaunti maalum benki kwa lengo la kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo ukarabati wa miundombinu na pia upanuzi wa huduma za  maji kwa wilaya.

Mhandisi Tonya ameongeza kuwa mradi huo unafadhiliwa na shirika la Serikali ya Uingereza (UKAID) kupitia shirika la HDIF kwa awamu ya kwanza kwa maeneo tajwa na katika utekelezaji wake umegharimu kiasi cha shilingi milioni 630,550,700.

Kwa upande wake mhamasishaji mkuu kutoka Idara ya Maendeleo ya Jamii Jimbo Katoliki Mbulu (DMDD) Rither Mallewo ameeleza changamoto mbalimbali wakati wa utekelezaji wa mradi ikiwemo uelewa mdogo kutoka wa walengwa kutokana na mradi huo kuwa na teknolojia ya kisasa na wa kwanza nchini Tanzania.

Mallewo amesema kuwa kutokana na changamoto hiyo ya mradi kuwa wa kwanza Tanzania, waliwapeleka walengwa kujifunza nchi jirani ya Kenya na baada ya hapo mradi ulijikita zaidi kwa uhamasishaji ambao ulichukua mwaka mmoja ili kujenga uelewa wa pamoja kwa walengwa kwa ajili ya udumisho wa mradi huu wa R3W wilayani Karatu.

Comments

  1. Naomba mawasiliano ya mhandisi hii teknolojia nmeipenda

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU