SEPTEMBA 8: SIKUKUU YA KUZALIWA BIKIRA MARIA



Mazingira ya Uzaliwa wa Bikira Maria Mtakatifu

UZALIWA au siku ya kuzaliwa kwa Bikira Maria Mtakatifu, au Kuzaliwa kwa Maria, au Kuzaliwa kwa Bikira Maria kunaihusu sikukuu moja ya Kikristo ya kumbukumbu ya kuadhimisha Uzawa wa Bikira Maria Mtakatifu.
Hata hivyo, kumbukumbu ya sikukuu hii haipo katika Kanuni ya siku hizi ya Kanisa Katoliki. Maelezo ya mapema au ya mwanzo mwanzo kabisa yanayogusia Uzawa wa Bikira Mtakatifu ni yale ya Yakobo, ambayo nayo hata hivyo, hayana uhalisia wala  uthibitisho wo wote.
Maelezo haya yanaonekana  katika Sura ya 5 Aya ya 2 ya hayo maandishi ya awali ya Yakobo ya uinjilisti. Maandishi haya yanayosema tu kwamba Wazazi wa Maria walikuwa Mtakatifu Anna na Mtakatifu Yoakimu yaliandikwa mwishoni mwa karne ya pili.
Kwa kawaida, Kanisa Katoliki linakuwa na kubukumbu ya kufa kwa watakatifu na si ya kuzaliwa kwao. Kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Maria na ile ya kuzaliwa kwa Yohani Mbatizaji ni kati ya zile kumbukumbu chache sana zinazozingatiwa na Kanisa Katoliki.
Uzingatiaji wa kumbukumbu za kuzaliwa kwa Maria na ule wa kuzaliwa kwa Yohani Mbatizaji umetokana na ule ukweli kuwa wawili hawa walikuwa wamechukua  ujumbe wa pekee sana katika historia ya ukombozi wa wanadamu. Sababu nyingine ni ile ya kimapokeo. Sababu hii ya kimapokeo ni kwamba, hawa hawa wawili, yaani Maria na Yohani Mbatizaji walikuwa watakatifu kuanzia kuzaliwa kwao.
Maria alikuwa amekingiwa dhambi ya asili na mwenzake Yohani Mbatizaji alikuwa amefanywa mtakatifu tangu alipokuwa tumboni mwa mama yake, Mtakatifu Elizabeti. Ukweli huu ni kwa mujibu wa tafsiri ya kimapokeo ya mwinjilisti Luka kama tusomavyo katika Lk 1:15, “Atakuwa mkuu mbele ya Bwana. Hatakunywa divai wala kileo, na atajazwa Roho Mtakatifu tangu tumboni mwa mama yake.”
Maandishi ya Dini ya Kiislamu kuhusu Uzawa wa Maria:
Labda utashangaa kusoma kuwa Uzawa wa Maria umeelezwa pia katika kitabu cha Qur’an. Katika sura ya sita ya kitabu hicho cha Qur’an, baba mzazi wa Mariam yaani Maria ametajwa kuwa alikuwa Imran (Yoakimu?) jina ambalo limepewa Sura hiyo ya kitabu cha Qur’an. Mama ya Mariam (Maria) alikuwa Hannah (Anna), kwa mujibu wa maelezo ya kitabu hicho.
Hannah (Anna) alikuwa daima anasali kumwomba Mungu amjalie kukipata kile alichokuwa anakitamani sana katika maisha yake, yaani mtoto. Katika sala zake hizo za maombi, Hannah (Anna) aliahidi kuwa iwapo sala zake zingesikilizwa, mtoto ambaye angempata, aliyemhisi kuwa angekuwa wa kiume angemtoa sadaka kwa Mungu.
Hannah (Anna) aliomba sana mtoto wake alindwe na asidhuriwe na shetani. Mapokeo ya Dini hiyo ya Kiislamu yanaeleza kuwa watoto waliozaliwa hapa duniani bila kuguswa na shetani ni wawili tu. Watoto hawa ni Mariam yaani Maria na Isa yaani Yesu.
Ibada kwa Maria inayotokana na huo ukweli kwamba alikingiwa dhambi ya asili na hivyo kustahili kupata hiyo heshima ambayo ni ya aina ya juu kabisa ya kuitwa “Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili” ni ibada inayozingatiwa na wengi katika ulimwengu wote wa Kikristo.
Yale maandishi ya Yakobo aliyokuwa ameyaandika mwishoni mwa karne ya pili, yanaeleza kuwa, Yoakimu, baba mzazi wa Maria alikuwa mtu mwenye uwezo wa kifedha na alikuwa tajiri katika moja wa yale makabila 12 ya Israeli. Pamoja na utajiri aliokuwa nao, Yoakimu na mke wake Anna walikuwa wanahuzunishwa na kitu kimoja. Kitu hicho kilikuwa kile cha kutokuwa na mtoto.
Hakuna maandishi ya kuaminika yanayoeleza mahali alipozaliwa Maria. Maandishi mengine yanaeleza kuwa Maria alizaliwa Nazareti, na mengine yanasema  alizaliwa Yerusalemu. Vyovyote viwavyo, inawezekana kabisa kwa mtu tajiri kama Yoakimu, kuwa na makazi Yudea na pia Galilea.
Tarehe ya sikukuu: Kimapokeo, tukio hili huadhimishwa tarehe ya 8 ya mwezi wa Septemba kama sikukuu ya Kiliturujia kwa mujibu wa Kalenda Kuu ya Kanisa Katoliki. Waamini wa Makanisa ya Kianglikana nao huadhimisha sikukuu hiyo tarehe hiyo hiyo ya 8 ya mwezi huo wa Septemba kwa mujibu wa Kalenda za Makanisa hayo ya Kianglikana.
Tarehe hiyo ya 8 ya mwezi wa Septemba huwa imepita miezi 9 baada ya Sherehe ya Bikira Maria Mtakatifu Mkingiwa Dhambi ya Asili. Sherehe ya Maria Mtakatifu Mkingiwa Dhambi ya Asili inasherehekewa tarehe ya 8 ya mwezi wa Disemba.
Maandishi ya awali kabisa yanayohusiana na Uzawa wa Maria yanaonekana katika waraka wa karne ya sita. Maandishi hayo yako katika wimbo unaogusia maadhimisho ya Uzawa wa Maria. Wengi wanahisi kuwa wimbo huu ulikuwa umetungwa na kuandikwa nchini Syria kwa sababu baada ya Mtaguso Mkuu wa Efeso Syria ilikuwa na vikundi vingi vya kidini vilivyomshabikia sana Maria kama Mama wa Mungu.
Kumbukumbu ya kwanza ya Kiliturujia inayohusiana na Uzawa wa Maria ni ile ya kutabarukiwa kwa Kanisa jipya la Bikira Maria lililokuwa limejengwa mahali palipokuwa panadhaniwa kuwa ndipo ilipokuwa nyumba ya wazazi wa Maria mjini Yerusalemu. Kanisa la kwanza lilikuwa limejengwa mahali hapo hapo kwenye karne ya tano.    
Wagriki wa Kanisa la Kiorthodoksi huadhimisha pia sikukuu hiyo ya Kuzaliwa Bikira Maria Mtakatifu tarehe hiyo hiyo ya 8 ya mwezi wa Septemba. Sikukuu hiyo huadhimishwa pia na Wakristo wa nchi ya Syria. Hawa nao huadhimisha sikukuu hiyo tarehe hiyo hiyo ya 8 ya mwezi huo wa Septemba.
Kwa kuwa maelezo ya Kuzaliwa kwa Maria yalikuwa yamefika kama hadithi kutokana na maandishi ya Yakobo ambayo hayakuwa na uthibitisho wowote, Kanisa Katoliki lilichelewa sana kuiasili sikukuu hiyo. Sikukuu ya Kuzaliwa kwa Maria ilianza kuadhimishwa Roma kuanzia mwishoni mwa karne ya saba.
Watawa wa kiume waliokuwa wametoka  sahemu za mashariki ndio waloifanya Roma ibadili msimamo wake wa kutokuadhimisha sikukuu hiyo na kuifanya sasa nayo pia iwe na msisimko wa kumbukumbu ya maadhimisho maalum ya Uzawa wa Maria.
Hatuambiwi, hata hivyo, hawa watawa wa kiume kutoka Mashariki walikuwa na hoja gani nzito iliyoweza kuiridhisha Roma mpaka ibadili msimamo wake uliokuwa umeshikiliwa kwa karne kadhaa.
Na Philip Komba





Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU