JIMBO KATOLIKI MAHENGE LAWAMWAGIA NEEMA WANAKIJIJI





KANISA KATOLIKI nchini limeendelea kuinjilisha kwa vitendo katika Jimbo Katoliki Mahenge baada ya kuwafikishia huduma ya nishati ya umeme wananchi zaidi ya elfu nane wa kijiji cha Lugalawa- Ludewa mkoa wa Njombe.



Akizungumza na gazeti hili, Mkurugenzi wa maendeleo jimboni humo Padri Nestory  ameeleza kuwa, Kanisa kama mama wa wote limeamua kuwagusa watu waishio vijijini ambao wametengwa na huduma za msingi za kijamii ikiwemo umeme, maji, hospitali nk.



“Tumeamua kusambaza umeme vijijini ili wananchi wapate fursa ya kujiendeleza kiuchumi na kuwa na unafuu wa maisha. Umeme huo una Megawati 1.7 ambao unasambazwa kwenye vijiji 20, shule za msingi na sekondari 43, vituo vya afya na zahanati 19, viwanda vidogo  na vya kati 340 pamoja na hospitali moja.



Hospitali na vituo vya afya vinahitaji umeme wa kudumu ambao utawawezesha kutoa huduma kwa kiwango kinachostahili. Viwanda vitaweza kuzalisha kwa haraka, wakulima watapata soko la uhakika na wafanya biashara wataweza kufanya biashara kwa wakati na watapata soko. Kwa kuanza tunaanza kuwasambazia watu elfu nne halafu tutaendelea na elfu nne waliobaki.



Umeme huo ni mwingi hivyo baada ya kuwasambazia watu elfu nane utakaobaki tutawauzia TANESCO,” ameeleza Padri Nestory.



Amesema kuwa, mradi huo wa kupeleka umeme vijijini utaisha Juni, 2018. Kwa sasa taratibu zote za kisheria na kitaalamu zimekamilika ambapo zinafanyika harakati za kusimika nguzo, kufunga nyanya na mambo mengine.



Ameeleza kuwa, si umeme tu bali jimbo hilo limeanzisha mradi wa ‘Soya ni pesa.’ Mradi huo ni kwa ajili ya kuondoa umasikini vijijini kwa kuwapatia mbegu ya soya wakulima hao ili walime kwa utaalamu na kukidhi mahitaji ya soko.



“Tuliona kuwa, soya ni moja ya zao lenye soko hapa nchini. Mradi huu umefadhiliwa na US Agricultural Department kupitia Catholic Relief service hapa nchini.



Tunachokitaka ni kuongeza uzalishaji wa soya vijijini . Hivyo tunatoa semina  juu ya kuchagua mbegu inayofaa, namna ya kuzalisha, kuvuna na kutunza  ili kupata mazao mengi yenye ubora wa soko.



Mradi huo umeongeza mradi ndani yake wa kufuga kuku. Soya ni chakula bora cha kuku. Hivyo mkulima akilima soya, wakati anavuna anapata chakula chake, mazao ya kuuza na chakula cha kuku.



Hivyo tunawapa mbegu ya soya na vifaranga ili waweze kulima na kufuga kwa pamoja.

Mradi huu umekuwa na mafanikio makubwa yanayoridhisha kwani baadhi yao tayari wamejenga nyumba, wanasomesha watoto na kujiinua kiuchumi,” amesema Padri Nestori.



Amesema kuwa, kwa mwaka jana na mwaka huu soko la soya limeongezeka kwani kilo moja wakulima hao wameuza kwa shilingi 1200 na kuna uhitaji mkubwa wa soya nchini.



Lengo la miradi hiyo ni kutaka tu kumuinua maskini kutoka katika hali duni na kuishi maisha bora ambayo anapata mahitaji yote ya msingi kwa mwanadamu.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU