HISTORIA FUPI YA UPADRI NA UINJILISHAJI TANZANIA-KUELEKEA JUBILEI YA MIAKA 150 YA UINJILISHAJI HUKO BUKOBA







 Nini maana ya Jubilei

KABLA hatujaendelea na maelezo juu ya historia ya  Upadri nchini Tanzania  na Uinjilishaji, kwanza tueleze kwa ufupi maana ya Jubilei. Neno Jubilei linatokana na neno la kiebrania lina maana ya kupiga tarumbeta kwa sababu ya furaha, uhuru na  kutubu baada ya kumaliza miaka hamsini.

Neno hili baada ya kuingia katika Kanisa Katoliki lina maana ya mwaka wa furaha, kumshukuru Mungu kwa baraka zake, kujipatanisha na Mungu kama una dhambi ulizotenda hasa kwa kuomba msamaha, kusamehe, mwaka wa matumaini, mwaka wa haki, mwaka wa kupokea sakramenti, mwaka wa kuweka maagano ya kumtumikia Mungu na ndugu zako kwa furaha na amani.

Jubilei inaambatana na kufanya hija kwenye sehemu takatifu, hii ndiyo maana tutafanya hija kwa kituo cha Hija cha Bikira Maria wa ludi kilichopo parokia ya Mugana, katika kufunga Jubilei wa Upadri tutafanya hija katika kituo cha Hija huko Bwanga Jimbo Kuu la Dodoma, hivyo hivyo katika kufunga Jubilei ya  Unjilishaji nchini Tanzania tufanya Hija katika Kituo cha hija cha Bagamoyo – Mlango wa Imani.

Uzinduzi wa jubilei
Baada ya kupata maana ya Jubilei hebu tuangalie tarehe za Uzinduzi wa Jubilei. Tarehe 1/10/2016,  itazinduliwa Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji ambayo tunategemea kilele chake kitakuwa 28/10/2018 kwenye kituo cha kitaifa cha hija- huko Bagamoyo- mlango wa Imani.

Siku hiyo pia itakuwa ya uzinduzi wa jubilei ya upadri katika Tanzania ambayo tunategemea kilele chake kitakuwa tarehe 15/8/2017 huko jimbo Kuu la Dodoma  kituo cha Hija cha Bwanga. Mapadri wa Kwanza walipadrishwa tarehe 15/8/1917 parokia ya Rubya Jimbo Katoliki Bukoba. Kama tunavyoona Jubilei ya upadri ipo ndani ya Jubilei ya Uinijilishaji. Haya matukio yanagusa Kanisa zima la Tanzania kwa sababu yanagusa Imani yetu.

Kwa hiyo tunawaalika  na kuhamasisha mapadri, watawa, waamini wote  na watu wenye mapenzi mema kuhudhuria sherehe za uzinduzi wa Jubilei ya miaka 150 ya Uinjilishaji na miaka 100 ya upadri katika Tanzania, utakaofanyika katika seminari ya Rubya jimboni Bukoba.

Pia kujiandalia sherehe za Kilele cha jubilei ya  upadri na Kilele cha Jubilei ya Uinjilishaji kwa tarehe zilizotajwa hapo. Tunapojiandaa kuadhimsha jubilei hizo tutajiandaa kiroho kwa semina, mafungo na kufanya hija katika vituo vya hija vya majimbo yetu, vya kanda na kimataifa.

Tarehe 1/10/2016 ilichaguliwa kuwa siku ya uzinduzi wa jubilei hizo kwa sababu ni sikukuu ya Mtakatifu Theresia wa Mtoto Yesu mlinzi wa misioni, mwanzo wa mwezi wa umisionari (Uinjilishaji) na Rozari takatifu, mapadri wa kwanza wa Rwanda waliosomea Rubya walipadrishwa tarehe  hiyo na mwisho ni siku ya kukumbuka kifo cha mwanzilishi wa Shirika la Roho Mtakatifu la  Francois Poullart des Places ambalo liliinjilisha sehemu kubwa ya Tanzania.


 Wakati wa Jubilei ni wakati wa kujitathimini
Kwa upande wa Upadri, ni nafasi ya kumshukuru Mungu kwa baraka zake kwa zawadi ya Sakramenti ya Upadri,  kwa mapadri 4 kutoka Tanzania na mapadri  3 kutoka Rwanda. Kwa kuinuliwa katika daraja la upadri  walionyesha kuwa inawezekana. Kwa hiyo ni nafasi ya kujitathimini, je zawadi hii tuliyopewa tunaiishi namna gani?

Je  tuna changamoto zipi katika maisha yetu na kutafuta dawa ya changamoto hizo. Kwa upande wa Uinjilishaji tunaangalia zawadi ya Furaha ya Injili  tuliyoipata na tunamshukuru Mungu. Tunaangalia maisha yetu ya Kiroho na maendeleo ya mwanadamu yaliyoletwa na ukristo hasa  elimu ya Mungu na ya dunia, shule, hospitali hata siku hizi tunaongelea vyuo vikuu, tunajitathimini , changamoto  zilizopo na kuangalia namna ya kwenda  mbele.

 Historia fupi ya seminari ya Rubya- mapadri wa kwanza walipopatikana

Seminari hii ya Rubya ilianzishwa  Novemba 1903  huko Kyegoroma Jimbo la Bukoba parokia ya Kagondo na Askofu John Joseph Hirth ( Mjerumani- kutoka eneo la Alsace ). Huyu alipokuwa Uganda  pia alianzisha seminari ya Villa Maria huko Uganda.

Katika nchi ya Uganda walipata mapadri wa kwanza mwaka 1913. Wakiwa ni padri Victor Mukasa Womeraka na Bazilio Lumu. Hawa mapadri walizikwa katika Kanisa Kuu la Villa Maria alipozikwa Askofu Streicher na Adrian Dgungu.

Waseminarist  walioanzia Kyegoromora walihamishiwa seminari ya Rubya  tarehe  21 Novemba 1904. Seminari ilianza na waseminari 30  na kufika Novemba 27 mwaka 1904 walikuwa 55. Rubya ilichaguliwa kuwa sehemu ya seminari kwa sababu ipo mlimani, Askofu  John Joseph aliona ni sehemu nzuri hasa kwa waseminari waliotoka nchi za Rwanda na Burundi waliozoea sehemu ya milima.

Wakati huo seminari ilikuwa chini ya vikariati ya Viktoria Nyanza ambayo iliongozwa na Askofu John Joseph Hirth. Wakati  huo vikariati hii ya Viktoria Nyanza ilijumuisha majimbo ya sasa Geita, Mwanza, Musoma, Kayanga, Rwanda, Bunda, Bukoba, Rulenge- Ngara, nchi ya Rwanda na Burundi.

Kwa hiyo waseminarista walitoka katika maeneo hayo. Waseminarista hawa baada ya kumaliza masomo yao ya seminari ndogo ya Rubya waliingia seminari kuu ya Rubya Mtakatifu Leo mwaka Oktoba 1909 wakiwa na waseminarista 18. Kati ya hao waliofikia upadri walikuwa wanafunzi 7.

Waseminarista walioingia  mwaka 1903 hakuna aliyefikia daraja Takatifu la Upadri. Wale ambao walipewa daraja la upadri  wa kwanza walitoka mwaka 1904  ambao walisajiliwa wakiwa  wanafunzi 33, mwaka huo walitoka mapadri  watano ambao ni Pd. Celestini Kipanda toka Ukerewe- Jimbo la Bunda, Pd. Barthasar Kafuko toka Nsasa Rwanda, Pd. Donatus Leberaho toka Issavi Rwanda,  Pd.Josephus Bugondo toka Issavi Rwanda naPd. Oscar Kyakaraba Jimbo la Bukoba.

Wale waliosajiliwa mwaka  1905 wakiwa 11, waliofikiwa daraja la Upadri walikuwa  Pd. Angelus Mwilabure kutoka Kome Jimbo katoliki Geita na Pd. Wilbard Mupapi kutoka  Jimbo katoliki Bukoba. 

Tarehe  (15/8/1917) mapadri wa Vikariati ya Viktoria Nyanza walipopewa daraja la upadri, pia padri wa kwanza wa nchi ya Jamhuri ya watu wa Kongo(ikijulikana kama Upper Congo) Padri Stephano Kaoze naye alipata daraja la Upadri katika sehemu ya Baudouinville.

 Na Jovitus Mwijage


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU