MIAKA 150 YA UINJILISHAJI TANZANIA NA 100 YA UPADRI KUZINDULIWA BUKOBA OKTOBA MOSI




KANISA Katoliki nchini linatarajia kuzindua Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara na miaka 100 ya Upadri Mosi Octoba 2016 huko  Rubya Jimbo Katoliki Bukoba.



Taarifa kutoka Kurugenzi ya Uchungaji ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) zimesema kuwa, siku hiyo hiyo itakuwa pia ni uzinduzi wa yubilei ya upadri katika Tanzania ambayo kilele chake kitakuwa Agosti 15, 2017 (Mapadri wa Kwanza walipadrishwa tarehe 15/8/1917 parokia ya Rubya Jimbo Katoliki la Bukoba) huko Jimbo Kuu Katoliki Dodoma, pia Kanisa linatarajia kuwa  na hija katika Kituo cha Bwanga huko Dodoma.



Yubilei ya upadri ipo ndani ya Yubilei ya Uinijilishaji, hivyo matukio hayo yote yanagusa Kanisa zima la Tanzania kwa sababu yanagusa Imani ya Kanisa Katoliki.



Hivyo waamini, mapadri, watawa na watu wote wenye mapenzi mema wanaalikwa na kuhamasishwa kuhudhuria sherehe za uzinduzi wa Yubilei ya miaka 150 ya Uinjilishaji na miaka 100 ya upadri katika Tanzania, utakaofanyika katika seminari ya Rubya jimboni Bukoba.



Taarifa hizo pia zinaeleza kuwa, Mosi Oktoba mwaka huu  ilichaguliwa kuwa siku ya uzinduzi wa yubilei hizo kwa sababu ni sikukuu ya Mtakatifu Theresia wa Mtoto Yesu mlinzi wa misioni, mwanzo wa mwezi wa umisionari (Uinjilishaji) na Rozari Takatifu, mapadri wa kwanza wa Rwanda waliosomea Rubya walipadrishwa tarehe  hiyo na ni siku ya kukumbuka kifo cha mwanzilishi wa Shirika la Roho Mtakatifu....... ambalo liliinjilisha Afrika ya Mashiriki.



Kwakuwa sherehe hizo ni za kitaifa, waamini kutoka majimbo yote 34 ya Kanisa Katoliki nchini wanaaswa kushiriki wakiongozwa na utaratibu uliopangwa kuwa siku ya kufika Bukoba ni Septemba 30, 2016 na kuondoka Oktoba 3, 2016.

Uzinduzi utakuwa Mosi Oktoba 2016 na kutakuwa na Hija huko Nyakijoga Oktoba 2, 2016.

 Gharama za kila mshiriki bila kuweka nauli ya kwenda huko Bukoba ni TZS 150,000/=.

 Fedha hiyo itagharamia  milo yote utakapokuwa kule tangu tarehe 30/9 mchana mpaka siku ya kuondoka tarehe 3/10 asubuhi, malazi kwa siku tatu, usafiri wa kutoka Bukoba kwenda Seminari ya Rubya, kutoka Seminari Rubya kwenda Parokia ya Mugana kwa Hija Nyakijoga na kurudi Bukoba.



Mapadri wanakumbushwa kwenda na mavazi meupe ndiyo yatakayotumika katika Liturujia siku  hizo.



Askofu Kilaini azungumza

Askofu Msaidizi Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini amezitaja Yubilee hizo kama matunda ya uinjilishaji toka mwaka 1868 ulipoingia Bagamoyo.



‘Katika Yubilee hizi ambazo zitazinduliwa huko Rubya ni katika kusherekea miaka 100 ya upadri toka mwaka 1917 tulipopata mapadri wa kwanza ambazo kilele chake ni mwaka 2017 na miaka 150 ya uinjilishaji Tanzania bara ambazo kilele chake ni mwaka 2018’ amesema Askofu Kilaini.



Pia aliongeza kwa, Yubilei ya miaka 100 ya upadri na 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara zinazinduliwa kwa pamoja kwa sababu ni matukio makuu mawili yanayofanana kwa sababu uinjilishaji ndio uliotuletea mapadri wazawa.



 ‘Tunawakaribisha maaskofu, mapadri watawa na waamini wote katika uzinduzi huo wa kipekee hapa Bukoba ili tuweze kuimarisha imani yetu na kufahamu ni wapi imani yetu ilitoka’ amesema Askofu kilaini.



Katika uzinduzi huo kivutio kikubwa ni katika Seminari ya Kwanza Kuu ya Mtakatifu Leo ambapo jengo lake bado lipo mpaka leo na ndilo liliokuwa likitumika kama darasa na wakati mwingine kama bweni.



‘Seminari ya Mtakatifu leo bado ipo lakini majengo mengine yaliyokuwa yamejengwa kwa msonge yalishabomoka lakini tunaimani watakaokuja watajifunza kitu kutoka katika seminari hiyo,’ameeleza.



Historia ya uinjilishaji Tanzania Bara.

Kanisa katoliki lilianza kazi yake Tanzania Bara miaka 150 iliyopita ikitokea Zanzibar mwaka 1868.

Historia yake inaanza mwaka 1860, Askofu Maupoint wa Reunion alipomtuma Padri wake Fava pamoja na watawa kuanzisha mission ya Zanzibar.

Kwa bahati mbaya kwa wakati ule Zanzibar ilikuwa ni kitovu cha biashara ya utumwa na asilimia kubwa ya wakazi wa Zanzibar walikuwa waislam hivyo kufanya ugumu wa kupata wazawa wa kuweza kuwabatiza na kukuza imani katika Zanzibar.

Lakini kwa sababu Askofu Maupoint asingeweza kufanya kazi kubwa sana aliomba shirika la Roho Mtakatifu ili liweze kuja na kusaidia katika uinjilishaji wa Zanzibar.

Kutokana na changamoto za biashara ya utumwa Zanzibar, Shirika la Roho Mtakatifu lilihamishia uinjilishaji wao Tanzania Bara baada ya kuona hawapati matunda ya kazi yao ingawa walibaki na kituo cha kuendelea kufanya kazi Zanzibar.



 Mnamo tarehe 4 march 1868 Shirika la Roho Mtakatifu lilikuja na mapadri wawili, Padri Antoine Horner na Padri Etienne Baur pamoja na mabruda wawili Celestine na Feliocian walifika Bagamoyo na kuanzisha uinjilishaji.



Ingawa walikutana na changamoto mbalimbali huko Bagamoyo wamisionari hao walianzisha vijiji vya watumwa ili kuweza kuwakomboa watumwa na hata waingereza walipokomesha biashara hiyo shirika la Roho Mtakatifu walipata watumwa wengi sana kutoka kwa waingereza kama ishara ya kumaliza biashara ya watumwa.



Licha ya kupata shida nyingi ikiwa ni pamoja na ugonjwa wa malaria, wamisionari hao walianza kueneza injili katika maeneo yote waliyokuwa wakipita kuingia Tanzania Bara eneo la  Morogoro na mwaka 1890 walifika katika maeneo ya  mlima Kilimanjaro na kusali misa yao ya kwanza katika mlima kilimanjao ikiwa pia na kuukabidhi mlima huo kwa Mama Maria na ukawa mwanzo mkubwa wa mafanikio ya uinjilishaji hasa katika maeneo ya Vunjo na Kilimanjaro.

Mapadri wa Roho Mtakatifu wakafungua Mission ya Kibosho baada ya Vunjo na Kilimanjaro na kuelekea maeneo ya Rombo na Moshi ndipo wakaanza kusambaa maeneo ya Tanga, Arusha na kufanya Arusha kuwa Makao yao Makuu mpaka sasa.

Baada ya Shirika la Roho Mtakatifu kuinjilisha sana maeneo hayo kwa wingi,  Shirika la Mapadri Weupe walifuata wakitokea Algeria walipokuwa wakifanya utume wao huko baada ya kusikia juu ya uenezaji injili Afrika ya Mashariki na Kati.



Alikuwa ni Baba Mtakatifu Leo wa Kumi na Tatu aliyewaruhusu Mapadri Weupe (White Fathers)  kufika Bagamoyo na kupokelewa na mapadri wa Roho Mtakatifu. Wakaanza uinjilishaji wao katika maeneo ya Unyanyembe Tabora.



Kutoka hapo Mapadri Weupe waligawana katika sehemu kuu mbili, sehemu ya kwanza ilikwenda maeneo ya kusini kuelekea Ujiji na sehemu ya pili ilikwenda maeneo ya kaskazini kuelekea Mwanza.

Kundi hili la kwanza lililoelekea Ujiji lilirudi baada ya kupata changamoto hasa pale walipotaka kwenda Rwanda na kwa wakati ule Ujiji ilikuwa ni kitovu kikuu cha biashara kiasi ambacho iliwawia ngumu kuendelea kukaa na kunya uinjilishaji pale Ujiji.

Waliporudi pia Tabora wahakufanikiwa sana kwa sababu Tabora yalikuwa Makao Makuu ya Mtemi Milambo na uislamu ulikuwa umeshamiri sana hivyo walikimbilia maeneo ya Kalema mwabao wa ziwa Tanganyika mwka 1886 na kuweka Makao yao Makuu hapo iliyokuja kuinjilisha maeneo yote ya Sumbawanga, Mbeya na Rukwa.



Baadaye walirudi Tabora na kukaa kwa kiasi maeneo ya kipalapala na wakafanikiwa zaidi walipoweka kambi maeneo ya Ushirombo na kuwa mission yao kubwa katika maeneo ya Unyanyembe. Baadye sana walirudi na kwenda tena Ujiji na Tukuyu.



Kundi la pili lililoelekea Mwanza wao walifika kuelekea katika Ufalme wa Kabaka kwa sababu walijua kuwa ufalme wa Kabaka kati ya Baganda kuna uwezekano mkubwa sana wa kuinjilisha kwa maana walijuwa wakiweza kumshika mfalme wa Kabaka wataweza kuinjilisha kabila lote na ufalme wote.

Padri Roodey aliyekuwa maarufu sana kama Padri mapera ambaye pia aliyewaongoza Mashahidi wa Uganda akiwa na mapadri wenzake waliweka makao yao maeneo ya Bukumbi baada ya kupata urafiki na Mtemi Rwoma wa maeneo ya Bukumbi na kujenga Makao yao Makuu ya Mapadri Weupe kwa upande wa kaskazini.



Mapadri Weupe walipigana vita vya pili na mtemi wa Uganda Mwaka 1892 na kufukuzwa na kuuwawa kwa wakristo 22 wakatoliki na 22 wakianglikana ambao ndio Mashahidi wa Uganda.



Baadhi yao walifanikiwa kukimbila Bukumbi na wengine wakaenda kusini mwa Ufalme wa Kabaka uliokuwa unaitwa budu ambao makao makuu leo ni masaka.

Mwaka 1892 kundi la mapadri na wakatoliki kutoka budu walivuka na kuingia bukoba na kufungua makao yao ya kwanza ya Missioni ya Kashozi ambayo ndiyo iliyoinjilisha maeneo ya Rulenge -Ngara na ukanda wote wa Mkoa wa Kagera.

Ingawa Makao Makuu ya Mapadri Weupe yalikuwa Bukumbi lakini Askofu John Hirth aliyekuwa Askofu wa Ukanda wote wa ziwa victoria alikuwa akikaa katika mission ya Kashozi.



Mission hiyo ya Kashozi na wamisionary wake ndio inayotupa historia nzima ya mapadri wa kwanza Tanzania Bara na kufunguliwa kwa seminari ya kwanza mwaka 1903 iliyokuja kuzaa matunda ya mapadri wa kwanza.



Historia hii ya jinsi uinjilishaji ulivyoingia Tanzania Bara miaka 150 iliyopita ndiyo inayotoa fahari kwa Kanisa la Tanzania kufanya Yubilee ya miaka 100 toka mapadri wa wa kwanza kupadrishwa katika Seminari ya Mtakatifu Leo Rubya Jimbo Katoliki Bukoba mwaka 1917.







Hii ndiyo historia ya Mapadri wa Mwanzo

Mwaka 1892 Askofu John Hirth alipofukuzwa kutoka Uganda kati ya vita ya kwanza ya wakristo na waislam na vita ya pili kati ya waangikana na wakatoliki aliingia Bukoba na kuanzisha mission ya kashozi mwaka 1892 na mwaka 1897 akenda kufungua mission ya Katoke Jimbo la Rulenge-Ngara.



Baadaye alianzisha seminari katika bonde la Kyegokola mahali ambapo walikuwa wanafanya matambiko na penye hali ya hewa mbaya .

Kutokana na hali hiyo, alihamisha seminari hiyo kutoka Kyegomola mwaka 1904 na kuanzisha seminari maeneo ya Rubya ambako ni mahali penye mwinuko, hali ya hewa nzuri, ndizi nyingi na baridi.

Hivyo seminari ndogo ya kwanza ilianza mwaka huo 1904 huko Rubya ingawa mawazo ya wengi walidhani anaazisha shule ya secondari ya kawaida .

Lakini toka mwanzo Askofu hirth alitaka kuwa na mapadi waafrika hivyo alianza kufundisha kilatini kama ulaya na masomo yote ya upadri kama ulaya pia.

Hali hiyo iliwafanya baadhi ya wamisionari kwenda kumshitaki kwa kutoa sababu mbili moja ikiwa anawapatia wazawa elimu kubwa mno inayowazidi waafrika na pili anataka kuwa na mapadri wakati bado hata waamini hawajawa wengi wakutosha ambao wengi wao walikuwa wakiamini katika mambo ya jadi.



Lakini Askofu Hirth alisimama katika kuamini kuwa waafrika wanaweza kuwa mapadri.

Wanaseminari wa mwanzo walitoka Kagera, wengine katika maeneo ya usukumani na kwa namana ya kipekee katika kisiwa cha Ukerewe na Kome na wengine kutoka Rwanda na Burundi.

Mwaka 1909 Askofu Hirth alianzisha seminari Kuu ili kuwezesha wanaseminari kupata elimu ya juu zaidi na seminari hiyo ilianza pale pale Rubya na kuitwa Seminari Kuu ya Mtakatifu Leo Rubya.

Lakini kuanza kwa Seminari Kuu kukachochea mgongano kati yake na mapadri wenzake kwa sababu ya kutokuamini kwao juu ya mwafrika kuwa padri sawa sawa na mapadri wa kizungu.

Kazi ya kufundisha na kuandaa mapadri iliendelea na mwaka 1917 seminari ya Mtakatifu Leo ilipata  wanafunzi saba ambao walipata upadri, wanne walitoka Tanzania na wawili Rwanda na mmoja kutoka Burundi



Katika hao wanne watanzania wawili walitokea Bukoba na wawili walitoka Mwanza katika visiwa vya Ukerewe na Kome.



Mnamo tarehe 15/8/1917 ndipo Tanzania ilipata mapadri wa kwanza waliopadrishwa katika Seminari ya Mtakatifu Leo Rubya.



Mapadri hao ni pamoja na Padri Wilboad Mupapi aliyetokea Kashozi Bukoba, Padri Oscar Kyakaraba aliyetokea Kashozi Bukoba, Padri Celestine Kipanda aliyetokea Kagunguli Ukerewe na Padri Angelo Mwilabure aliyetokea katika Visiwa vya Kome Mwanza.



Mapadri wengine wa Rwanda wao walipata upadri Rwanda baada ya vikarieti ya Nyanza kugawanywa na kupata vikarieti ya Kivu ndipo askofu Hirth alihamishiwa huko na aliwachukua wanafunzi hao wawili na kuwapatia upadri tarehe 7/10/1917 huko Rwanda.

Mapadri hao wa Rwnada walikuwa ni Padri Donatus Reberaho aliyejiunga katika Seminari ya Rubya November 1904 akiwa ni mwanafunzi wa 42 na wa pili alikuwa ni Padri Josephus Bugondo aliyejinga mwaka huo huo na wenzake ila yeye alikuwa mwanafunzi wa 47 kuingia Rubya Seminari.

Padri aliyetokea Burundi alikuwa ni Padri Balthazar Kafuko ambaye yeye alikuwa mwanafunzi wa 38 kujiunga katika Seminari ya Rubya.



 KURUGENZI YA MAWASILIANO TEC






Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU