"AFRIKA INAHITAJI MARAISI 50 KAMA MAGUFULI"


Na Stanslaus Likomawagi, Dodoma

MKURUGENZI wa Mtandao wa Tume ya Haki na Amani Afrika (yenye makao yake makuu mjini Washinton nchini Marekani) Padri Ariedi Okure wa Kanisa Katoliki amesema kuwa, Bara la Afrika linahitaji maraisi 50 kama Dkt. John Magufuli ambao watasaidia kujenga uadilifu katika Serikali, kukuza maendeleo na kujali watu wanyonge zaidi.

Padri Okure ambaye ni Raia wa Nigeria amesema hayo hivi karibuni Septemba 15 mwaka huu  wakati akizungumza na mwandishi wa habari mara baada ya kumalizika Kongamano juu ya haki katika Uporaji Ardhi na madhara kwa Watanzania na Afrika lililofanyika mjini Dodoma.

Ameweka wazi kuwa, yeye ni mwafrika anayefanya kazi ughaibuni lakini anajivunia sana pale anapoona juhudi kubwa anazozifanya Rais Magufuli ambazo zimemjengea heshima ndani na nje ya Bara la Afrika. Ameeleza kuwa, utendaji wake ni mzuri hauwezi kuulinganisha na Maraisi wengine wa Afrika.

Aidha amefafanua kuwa Dkt. Magufuli ameonyesha kwa dhati kuwa anawapenda wanyonge na anataka rasilimali za Tanzania ziwanufaishe watu wote wa nchi hii.

“Nikiwa Marekani nilifurahishwa na hatua yake ya kuamua fedha za maadhimisho ya sherehe za uhuru wa Tanzania zielekezwe kwenye miradi ya maendeleo kwa ajili ya kuwasaidia watu.

Hata zile fedha za hafla ya yeye kuzindua Bunge la 11 kuzipeleka Hospitali ya Taifa Muhimbili kununua vitanda na magodoro kwa wagonjwa ilitoa fundisho kwa dunia na kwa viongozi kuwa na moyo wa kuwasaidia wahitaji na wenye shida,” amesema Padri Okure.

Pia amefafanua kuwa, Raisi Magufuli anapaswa kuungwa mkono na Watanzania wote wenye mapenzi mema katika jitihada zake za kujenga Tanzania mpya na siyo kumkatisha tamaa.

“Najua hata maandiko yanasema Yesu alipingwa na maadui kutokana na kuwa mkweli, kupenda wanyonge na kusaidia wenye shida , hivyo Magufuli ni msaada kwa wanyonge” amesema Padri Okure.

Kuhusu matatizo mbalimbali ya Bara la Afrika Padri Okure amesema yanatokana na mambo mengi lakini kubwa ni rushwa ambayo imekuwa ni saratani ya kuzuia maendeleo na imesababisha hata mapigano kwa watu kugombea ardhi na rasilimali nyingine Barani humo.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU