MUSWADA WA HABARI: WADAU WATOA MAONI



MUSWADA wa Sheria ya upataji wa taarifa wa mwaka 2016 (The access to information bill 2016), umewasilishwa bungeni huku wadau mbalimbali wa tasnia ya habari wakitaka taaluma ya habari ipewe hadhi stahiki.
Kiongozi imeongea na baadhi ya wadau wa habari nchini ambapo pamoja na kupongeza hatua hiyo ya serikali, imewataka wabunge kutoa michango itakayowezesha kuboresha na kusimamia mambo muhimu yanayotarajiwa na wananchi.
Kwa upande wake Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino Mwanza (SAUT), Mlagiri Kopoka ameeleza kuwa, kupitia michango yao, wabunge hawana budi kusimama imara ili haki za kupata taarifa zisiporwe tena.
“Jambo la msingi tunalotazamia katika muswada huu ni fursa ya kupata taarifa hasa katika taasisi za umma. Uendeshwaji wa serikali unapaswa kuwa wazi, na siyo wa siri tena. Katika hili wabunge wetu wanatakiwa kusimama imara ili haki yetu ya kupata taarifa isiporwe tena” ameeleza Kopoka.
Aidha Kopoka ambaye pia ni mwandishi wa makala na vitabu, ametahadharisha kuwa matarajio ya watanzania ni kufanyiwa marekebisho kwa vipengele vinavyopora uhuru wa kupata taarifa.
“Tusipofanya hivyo tutajikuta tuna sheria mpya huku mambo yakiwa ni yale yale” ameongeza.
Naye Denis Mpagaze, mwandishi na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano katika Chuo Kikuu cha Askofu Mkuu James Songea (AJUCO), ambacho ni Chuo Kikuu Kishiriki cha Mtakatifu Agustino (SAUT), amesema kuwa muswada huo usaidie kufanya taaluma ya habari iheshimike.
“Kuna haja ya kuifanya taaluma ya habari itambulike na kuheshimiwa. Na ili tasnia hii iweze kuwa taaluma ni lazima kuwe na mafunzo ya muda mrefu, tuwe na vyuo vinavyoaminika na vyenye ubora, wahadhiri waliobobea na bodi itakayosimamia taaluma hiyo” ameeleza Mpagaze.
Pia Mpagaze ameweka wazi kuwa kukithiri kwa utitiri wa vyuo visivyokuwa na sifa za kutoa mafunzo ya uandishi wa habari, kunachangia kushuka kwa hadhi ya taaluma hiyo. Aidha ameonya kuwa uandishi wa habari ni kazi inapaswa kufanywa na watu wenye weledi na siyo waliokosa kazi ya kufanya.
“Zile fikra kuwa mtu yeyote anaweza kuwa mwandishi wa habari ziishe. Unakuta mtu amemaliza darasa la saba, kwa kuwa ana sauti nzuri basi anafaa kuwa mtangazaji. Ni lazima turatibu taaluma ya habari ndipo mambo mengine kama maslahi ya waandishi yatakapoboreshwa” ameongeza.
Michango ya wabunge
Baada ya muswada huo kupelekwa bungeni katika mkutano wa nne wa bunge la 11, Septemba 6, 2016 wabunge mbalimbali walipata fursa ya kutoa michango yao katika muswada huo.
Kwa upande wake Mbunge wa Rufiji, Mohamed Mchengerwa amesema kuwa kupitishwa kwa muswada huo kutawasaidia wananchi kupata taarifa kuhusu miradi na utekelezaji wa majukumu ya serikali.
“Utasaidia upatikanaji wa taarifa zilizopo katika chini ya himaya ya wizara na taasisi zilizopo chini yake. Pia tutambue kuwa nchi hii ni ya wananchi. Kupitishwa kwa muswada huu kutatoa fursa kwa wananchi wetu kupata taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo” ameeleza.
Tanzania itakuwa nchi ya tano Barani Afrika kupitisha sheria ya upatikanaji wa taarifa, huku ikiwa nchi ya 67 duniani kupitisha sheria hiyo. Nchi ya kwanza kupitisha sheria hiyo ni Newzland, ambayo ilipitisha sheria hiyo mwaka 1766.
Maelezo ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo
Akiwa mkoani Mbeya mwezi Aprili mwaka huu, Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo Nape Nnauye aliwaeleza wadau wa habari wa mikoa ya Mbeya na Songwe kuwa muswada huo tayari umeshafanyiwa marekebisho, ambapo mwaka jana uliondolewa bungeni baada ya kupigiwa kelele na wadau kuwa ulihitaji kufanyiwa marekebisho katika baadhi ya vifungu.
Nape alieleza kuwa muswada huo umebeba mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na maslahi ya waandishi wa habari, tatizo la utitiri wa vyuo vya habari visivyokuwa na sifa ambavyo havina budi kuondolewa, huku ukilenga kurudisha heshima ya tasnia ya habari.
“Muswada huu mzuri na utasaida kuleta suluhishi la malalamiko ya kuwepo kwa sheria kandamizi, pia itasaidia kukuza tansia ya habari pamoja na kuifanya tasnia ya habari kuheshimiwa kama tansia nyingine”,amesema Nape.

 Na Pascal Mwanache, Dar es salaam

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU