CARITAS-TUNAWEKA KAMBI BUKOBA

Na Pascal Mwanache, Dar es salaam
KUFUATIA majanga yaliyosababishwa na tetemeko la ardhi lililoikumba baadhi ya mikoa ya Kanda ya Ziwa, hasa Mkoa wa Kagera, Idara ya Caritas, katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania imedhamiria kuweka kambi Mkoani Kagera.
Akizungumza na Gazeti la Kiongozi, Katibu Mtendaji wa Caritas Tanzania, Laurent Masui ameeleza kuwa tayari idara hiyo imepeleka maafisa wake mkoani Kagera, kwa ajili ya kufanya tathmini ya awali itakaowezesha kubaini ukubwa na madhara ya tetemeko hilo.
“Sisi tutaendelea kuwepo pale kwa kuwa hiyo ndiyo kazi yetu. Awali ya yote ni lazima tutambue msaada wa aina gani unaohitajika; ni wa dharula, wa haraka au wa muda mrefu. Hivyo lengo la kupeleka wataalamu wetu ni kufanya tathmini itakayotusaidia kuwa na vipaumbele vinavyoakisi mahitaji ya muda huu” ameeleza Masui.
Pamoja na timu ya wataalamu wa Caritas kuwasili Bukoba na kuanza kufanya tathmini, Masui amebainisha kuwa ofisi ya Caritas Taifa imewasilisha fedha zipatazo Tsh Milioni 10 katika ofisi ya Caritas Jimbo Katoliki Bukoba, ikiwa ni hatua za awali za kusaidia wahanga wa tetemeko hilo.
Aidha Masui amesema kuwa utoaji wa misaada kwa wahanga hao ni lazima ujali mahitaji halisi ya waathirika hao, na kushauri kuwa lazima kuwe na kipaumbele katika kutoa misaada mbalimbali.
“Tetemeko limeathiri huduma za kijamii, miundombinu na maisha ya wakazi husika, hivyo misaada tunayoitoa ni lazima iongozwe na kipaumbele kadiri ya mahitaji. Ni lazima tukaone watu wanahitaji nini ili tuweze kujua kipaumbele ni kipi. Tutaweka kambi Kagera, na kambi hiyo itakuwa endelevu” ameongeza.
Madhara mpaka sasa
Vifo vya waathirika wa tetemeko la ardhi mkoani Kagera mpaka kufikia Septemba 14 vimefikia watu 17.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Salum Kijuu, shule za sekondari za Nyakato na Ihungo mkoani humo zimefungwa kwa muda wa wiki mbili kutokana na miundombinu yake kuharibika, huku wanafunzi wakiruhusiwa kurudi katika familia zao baada ya kuonekana kuathirika kisaikolojia.
Aidha licha ya tetemeko hilo kuyakumba maeneo kadhaa ya mkoa huo, Kijuu amebainisha kuwa  Manispaa ya Bukoba ndiyo iliyoathiriwa zaidi, kwa kuwa na idadi ya vifo 17, kujeruhi watu 252, kati yao 169 wakiwa wamelazwa hospitalini, takribani  nyumba 753 zimeanguka, na nyumba 1,037 kupata nyufa. Athari za tetemeko hilo pia  zimezikumba Halmashauri za Wilaya ya Bukoba, Misenyi, Muleba, Karagwe na Kyerwa.
Michango mbalimbali na mahitaji
Kwa mujibu wa RC Kijuu, fedha zinazohitajika kukabiliana na janga hilo ni zaidi ya Tsh bilioni 2.3 kwa ajili ya mahitaji mbalimbali ya waathirika, na tayari serikali ikihamasisha na kupatikana zaidi ya Sh bilioni 1.4.
Kati ya fedha hizo zilizopatikana, TSh milioni 700 zilikuwa ahadi, TSh milioni 646 pesa taslimu, Dola za Marekani 10,000, Euro 10,000 na mifuko 2,800 ya saruji, huku kampuni za mafuta ya Oilcom, GBP na Moil, zikijitolea kujenga shule mbili za sekondari zilizoathiriwa na tetemeko hilo.
Kwa mujibu wa Kijuu mahitaji yanayohitaji kwa haraka ni dawa, tiba na vifaa tiba, vifaa vya ujenzi mabati 90,000 yenye gharama ya Tsh bilioni 1.7, saruji mifuko 9,000 yenye thamani ya Tsh milioni 162, mbao zenye thamani ya Tsh milioni 450 na misumari yenye thamani ya Tsh milioni 12 ambapo jumla ni Tsh bilioni 2.3.
Pia Kijuu amewaomba wananchi, wadau na marafiki walioguswa na janga hilo katika mkoa na nje ya mkoa, wachangie michango yao kupitia akaunti ya maafa iliyopo katika benki ya CRDB yenye namba 0152225617300 na kwa walioko nje watumie Swift code:CORUtztz, huku akiomba watakaowiwa kutoa wawasiliane na ofisi yake kwa maelezo zaidi.
Septemba 10, 2016 majira ya saa 9.27 alasiri mji wa Bukoba ulikumbwa na tetemeko la ardhi, ambalo nguvu ya mtetemo wake ulikuwa ni 5.7 kwa kutumia skeli ya “Ritcher”. Ukubwa huo ni wa juu kiasi cha kuleta madhara kama yalivyotokea.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU