KUADHIMISHA PASAKA KWA SIKU NANE

KUADHIMISHA PASAKA KWA SIKU NANE

TUANZE kwa kujikumbusha neno Pasaka. Mwenyezi Mungu alilikomboa taifa lake Waisraeli kutoka utumwa wa Farao nchini Misri kwa tendo la Pasaka alipopita kuwaua wazaliwa wa kwanza wa wanadamu na wanyama katika nyumba za Wamisri ndipo Farao alipowaacha huru Waisraeli waondoke(Kut 12:1-14).
Tendo hili la Mwenyezi Mungu kuwakomboa watu wake kutoka Misri lilikuwa kubwa na muhimu sana katika historia ya Waisraeli; waliliadhimisha kila mwaka, na walipofanya vile waliona  ukombozi wao anatendeka upya. Pasaka ni kupita kwa Bwana (Kut.12:12-13 ).
Mateso kifo na  Ufufuko
Kwetu Wakristo Pasaka ni pia kupita kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Baada ya kuadhimisha Karamu ya mwisho na kuweka Sakramenti ya Ekaristi, Upadri na amri ya Mapendo,  Bwana Yesu alianza  Pasaka yake yaani kuteswa, kufa msalabani, kuzikwa na hatimaye kufufuka kwake.
Pasaka isieleweke tendo la Ufufuko pekee, bali kupita kwake Bwana katika matendo hayo yote. Ni kwa sababu hiyo kilele cha kuadhimisha Liturujia yetu ni Siku Tatu Kuu za Pasaka katika siku ambazo tunaadhimisha matendo hayo yote. Tendo la kufufuka ni kilele au upeo wa Pasaka, kupita kwa Bwana. Kwani hatuwezi kuadhimisha Ufufuko bila mateso na kufa kwake.
Kutokana na Pasaka kuwa kilele cha Ukombozi wetu Kanisa huadhimisha Sherehe hiyo kwa namna ya pekee sana kama siku moja ndefu ya siku nane. Siku nane hizo huitwa Oktava.
Neno hilo hutokana na neno la kilatini octo maana yake nane. Kwa hiyo Oktava ya Pasaka ni siku nane za kuadhimisha Pasaka tangu Dominika ya Pasaka mpaka Dominika ya pili ya Pasaka. Hakuna Maadhimisho mengine  siku hizo bali ni PASAKA TU.
Asili ya Oktava
Kanisa imepokea utaratibu wa kuadhimisha Oktava kutoka kwa Waisraeli. Wao waliadhimisha sherehe zao kuu  za kidini kwa muda wa siku saba au nane. Sikukuu ya Pasaka  ambayo tumeitaja hapo juu iliadhimishwa kila mwaka kwa muda wa siku saba na muda huo walikuwa wakila mikate isiyotiwa chachu.
Sikukuu ya Vibanda pia ilikuwa kati ya sikukuu kubwa katika dini ya Waisraeli. Walijenga vibanda na kuishi humo kwa siku nane wakiadhimisha tendo la kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa safari yao kutoka Misri: kwani walipokuwa njiani wakitembea kwenda Isareli walifanya vituo sehemu mbalimbali. Katika vituo hivyo walijenga vibanda na kuishi humo mpaka walipoamua kuendelea na safari yao.
Kutokana na hali hiyo Liturujia ya Kanisa Katoliki imepokea utaratibu wa kuadhimisha Sherehe ya Pasaka kwa namna ya pekee kwa Siku nane.
Katika historia, karne za Kati, kulikuwa Sikukuu kadhaa zilizoadhimishwa kwa Oktava lakini katika marekebisho Oktava nyingi zikaja kufutwa. Tumebaki na Sherehe mbili tu ambazo tunaadhimisha kwa Oktava katika Liturujia ya Kanisa, Noeli au Krismasi na Pasaka.
Oktava ya Noeli imeruhusu kuwa na sikukuu kadhaa zinazoadhimishwa katika siku hizo nane lakini Oktava hii ya Pasaka hairuhusu Sikukuu ye yote. Iwapo Sherehe yoyote inaangukia wakati wa Juma Kuu au Oktava hupelekwa mbele na kuadhimishwa Jumatatu baada ya kumaliza Oktava ya Pasaka.
Tunaadhimisha Juma Kuu au Juma Takatifu kuanzia Dominika ya Matawi ya Mateso ya Bwana na kufuatiwa na  Ufufuko wake kwa muda wa siku nane.
Hii ndiyo Siku
Katika kila siku ya Oktava ya Pasaka Liturujia husisitiza: Hii ndiyo Siku aliyoifanya Bwana, tufurahi na kuishangilia, Aleluya(Zb 118:24). Maneno hayo humaanisha kwamba siku nane ni kama siku moja ndefu yenye urefu unaolingana na siku nane.
Kila siku ni kama Dominika ile ya Pasaka. Kwa maneno mengine: Ukuu na hadhi ya Dominika ile ya Pasaka ni kubwa hivi inaadhimishwa katika siku hizo nane. Ndiyo maana kila siku katika siku nane hizo tunasali: Hii ndiyo
siku aliyoifanya Bwana ...Inafaa sana kuliimba Shangilio hilo kila linapotokea, iwe wakati wa Misa au wakati wa Masifu ya Asubuhi hata ya Jioni; kwani ni ujumbe mkubwa katika Oktava ya Pasaka.
Sekwensia ya Pasaka
Katika siku nane hizo kuu za Pasaka wakati wa Adhimisho la Ekaristi ni vizuri kuimba shairi hilo muhimu Victimae Paschali  ndivyo sekwensia hiyo muhimu inavyoanza kwa kilatini. Mtunzi wake kwa uhakika hafahamiki lakini kwa hakika limetungwa mnamo karne ya 11 au 12.
Beti wa kwanza na wa pili unatoa wito kumtukuza Mwanakondoo aliyewakomboa kondoo wake. Huyo Mwanakondoo   ni Kristo asiye dhambi. Beti zinazofuata ni mazungumzo kati ya mitume na Maria Magdalena. Hatimaye linaishia na sifa kwa Mfalme mshindaji na kumwomba atuhurumie.
Mshumaa wa Pasaka
Jambo jingine muhimu sana ambalo ni ishara kubwa  katika kipindi chote cha Pasaka ni mshumaa wa Pasaka.  Tunakumbuka  Alhamisi kuu baada ya kuhamisha Ekaristi nguo na mishumaa ziliondolewa altareni ishara ya Bwana wetu kuingia katika mateso yake.
Mshumaa wa Pasaka unaowashwa baada ya kubariki moto mpya nje ya kanisa ndio unaoongoza maandamano kuingia kanisani ishara ya Kristo anayefukuza giza la dhambi.
 Kwa namna ya pekee katika siku hizo nane mshumaa wa Pasaka uwe unawashwa wakati wa Maadhimisho yote ya Liturujia, iwe adhimisho la Ekaristi au Masifu ya Asubuhi au Masifu ya Jioni.
Ni jambo la kupongeza sana kuona parokia nyingi waamini wanashirikishwa katika kusali au kuimba Masifu ya Asubuhi kabla ya Misa. Basi mshumaa huo wa Pasaka uwe unawashwa sio tu wakati wa Misa inapoanza, bali bali mwanzoni mwa Masifu hayo ya Asubuhi, ishara ya kumshangilia Yesu Mfufuka. Inapoanza misa ndipo iwashwe mishumaa ya altareni.
Kuwaombea Wakristo wapya
Wakristo waliobatizwa katika Mkesha wa Pasaka na kuvishwa nguo nyeupe walitakiwa kuja kanisani kila siku katika Oktava  wakiwa na nguo zao nyeupe.
Sala za Misa katika Oktava mara nyingi zinawataja hao kwamba waizingatie kwa dhati hiyo imani waliyoipokea. Katika Oktava, Kanisa lilikuwa likiwaombea kwa namna ya pekee wakristo hao wachanga ili wawe imara katika maisha yao mapya.
 Kwa mara ya mwisho walipotakiwa kuja kanisani na nguo zao nyeupe ilikuwa Dominika ya pili ya Pasaka, ndiyo kilele cha  Oktava. Kutokana na kuja kanisani na nguo nyeupe basi Dominika hiyo ikaja kujulikana kama Dominika nyeupe, jina ambalo  limetumika mpaka miaka ya karibuni. Papa Benedikto XVI (kumi na sita) aliipa  Dominika hiyo jina jipya: Dominika ya Huruma ya Mungu.
Katika kuadhimisha Oktava ya Pasaka kulikuwa na mkazo wa pekee kuwahimiza wakristo wapya waliobatizwa Mkesha wa Pasaka pia wakristo wengine kushiriki misa hasa juma hilo la Oktava.
Siku hizo zilikuwa pia nafasi kwa wakristo hao wachanga kupata mafundisho  yaliyowasaidia kuimarisha imani waliyoipokea. Hatuna budi sote kuimarisha imani yetu kwa kushiriki Misa wakati wa Pasaka.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU