Ask.Kilaini:Papa Fransisko ametufungulia mlango wa huruma

Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini
ASKOFU Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini amesema kuwa ndani ya miaka mitatu ya utume wa Baba Mtakatifu Fransisko Kanisa limeshuhudia jinsi Papa huyo alivyowafungulia waamini mlngo wa huruma.

Ameeleza hayo hivi karibuni alipohojiwa na Kiongozi juu ya miaka mitatu ya utume wa Papa Fransisko kama Halifa wa Mtume Petro, ambapo amebainisha kuwa Papa Fransisko amelifundisha Kanisa kuwa binadamu hana haki ya kuhukumu bali kusaidia hasa katika kuwaita watu wenye shida na kuwasaidia.

“Papa Fransisko ametufundisha kuwa kazi yetu ni kumtafuta mtu yeyote aliyepotea. Ametenda na kufundisha kuwa kazi yetu ni kutafuta na kumrahisishia binadamu ili aweze kumrudia Mungu. Hivyo nasi tunakumbushwa kuwa tupo duniani tunapaswa kuisaidia dunia” ameeleza Askofu Kilaini.

Aidha Askofu Kilaini ameongeza kuwa mkazo wa Papa Fransisko katika utume wake umejikita katika ‘utu ndani ya Kanisa’ huku akilenga kuwatafuta wadhambi na kuwarudisha kutafuta uso wa huruma ya Mungu.

Amesema kuwa kamwe Papa Fransisko hayuko tayari kuvumilia ubaguzi au kuona wenye dhambi wakitengwa ndiyo maana daima anatafuta namna ya kuwarudisha binadamu kwa Mungu kwa kuwapatia fursa mbalimbali.

Ameongeza kuwa moja ya mafundisho muhimu ya Papa Fransisko ni kuwa hakuna aliye mtakatifu zaidi ya mwingine, binadamu wote ni sawa na kila mmoja amepewa namna ya kuutafuta utakatifu.

“Papa Fransisko ametupatia mtazamo mpya, wa kututaka kuwatafuta wenye dhambi. Mtazamo huu unatupeleka hatua moja mbele na kutafakari juu ya utu ndani ya Kanisa. Tukiwa hapa duniani anatutaka tuwatafute wenye dhambi na kuwarudisha kwa Mungu. Ameisaidia dunia katika mambo mengi ikiwa ni pamoja na utunzaji wa mazingira, kujali maskini, wakimbizi na wahamiaji na kutafuta wadhambi” ameongeza.

Masui: Papa ametatua changamoto za uharibifu wa mazingira kwa vitendo

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Caritas Tanzania chini ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Bw. Laurent Masui ameeleza kuwa utume wa Papa Fransisko umeiwezesha dunia kupata suluhisho lisilo la kinadharia juu ya uharibifu wa mazingira.

Masui ambaye pia ni mwanaharakati wa mazingira nchini amefafanua kuwa kupitia Waraka wa ‘Laudato Si’ Papa Fransisko ametoa jibu la tatizo la uharibifu wa mazingira, huku waraka huo pia ukiwa umesaidia uandaaji wa mpango wa maendeleo endelevu ya Milenia.

“Waraka wa Laudato si umeleta na kuboresha mtazamo unaotekelezeka juu ya kuhifadhi mazingira, na mtazamo huo umetutoa katika kufikiri kwa nadharia na unatoa dira katika kutunza mazingira kwa vitendo. Kabla yake kulikuwa na mitazamo tofauti huku kila mmoja akitaka mtazamo wake uheshimiwe, na katika hilo hakuna aliyetekeleza.

Ni ukweli kuwa Kanisa linaposema juu ya jambo Fulani linakuwa limetafakari na kupitia mitazamo yote inayolizunguka jambo hilo kabla ya kutolea maamuzi au ufafanuzi. Hivyo hata waraka huu umeangalia uhalisia na kutoa mwelekeo unaotekelezeka” ameeleza Masui.

Akitaja moja ya mambo muhimu yaliwekewa mkazo katika waraka huo, Bw. Masui ameeleza kuwa Papa amerekebisha ajenda ya ardhi na kuiweka sawa hasa kwa kusisitiza umuhimu wa ardhi kwa mtu mmoja mmoja na jamii.

“Waraka huu umegusa watu wengi hasa kwa jinsi ulivyotoa kipaumbele juu ya umuhimu wa kumiliki ardhi. Papa amefafanua kuwa ardhi ni makazi, ardhi ni kazi au ajira na ardhi ni utambulisho wa mtu, hivyo kwa msisitizo huu anataka kutueleza kuwa thamani yetu na utamaduni wetu upo katika kutunza na kumiliki ardhi” ameongeza.

Aidha Bw. Masui amesema kuwa Papa Fransisko pia ni mtetezi wa haki za binadamu hasa za wakimbizi na wahamiaji na mara kadhaa amekuwa akikemea na kushauri makundi mbalimbali na Jumuiya za Kimataifa kuhakikisha wanawatunza na kuwahifadhi wakimbizi.

Pia Papa ameshiriki jitihada za kutunza wakimbizi kwa kuagiza sehemu ya Kanisa yenye nafasi kutumika kuwahifadhi wakimbizi na wahamiaji huku mara kadhaa akitoa barua za kichungaji wakati wa maadhimisho ya siku ya wakimbizi duniani.


Machi 13, 2016 Baba Mtakatifu Fransisko ameadhimisha kumbukumbu ya miaka mitati tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU