TEC, Kwaya ya Vijana Michungwani kuunusuru Muziki Mtakatifu


Na Pascal Mwanache, DSM.

“MUZIKI wetu ni lazima uwe mtakatifu kwa sababu ni sehemu ya liturujia. Tangu zamani mafundisho mengi yamewekwa kwenye muziki. Hii itukumbushe kuwa sisi tumeitwa na kutumwa kuinjilisha na kutakatifuza, tuweze kuwagusa watu ili wamgeukie Mungu. Lakini kwa sasa uwanja wa muziki mtakatifu umevamiwa sana, ikiwa ni mbinu za shetani kushambulia yaliyo mema. Lazima vita hii tuishinde”.
Ni maneno aliyowahi kusema Askofu Salutaris Libena wa Jimbo Katoliki Ifakara, na Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia TEC.
Kwa muda mrefu sasa Gazeti Kiongozi limekuwa likichapisha makala mbalimbali kuhusu muziki mtakatifu, ili kuendeleza tunu hizo ya pekee kwa Kanisa, na kuwakumbusha watunzi wa kileo kufuata miongozo inayotoa mwelekeo sahihi wa utume wa uimbaji. Moja ya miongozo hiyo ni Hati ya Liturujia (Sacrosanctum Concilium), ambayo ni maelekezo yaliyotolewa na mababa wa Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikani.
Aidha, katika toleo lililopita tuliangazia sababu za kwa nini waamini wanapenda nyimbo za zamani iwe katika Adhimisho la Misa Takatifu au kwa kusikiliza. Nilitaja baadhi ya sababu kuwa ni Kushirikishwa kikamilifu, kwamba kazi ya muziki mtakatifu ni kuwasaidia waamini wasali vizuri, hii haina maana kwamba waamini wawe mabubu tu katika maadhimisho. Bali washiriki kuitikia, kuimba nyimbo wanazozifahamu au hata zile wasizofahamu ili mradi ziwe zinashikika kirahisi.
Pili Muziki wenye sala na tafakari, Moja ya mambo ambayo watunzi wa mwanzo hapa nchini walifaulu basi ni kutunga wakiwa katika hali ya sala.
Kumbe, kutokana na sababu mbalimbali na maombi ya wadau wengi wa muziki mtakatifu, kuna kila sababu ya kuhifadhi nyimbo zile za zamani ili ziwe kama hazina, funzo au darasa, na ukumbusho wa mchango mkubwa uliofanywa na watunzi wa zamani ambao kwa kiasi kikubwa walijitahidi kutunga wakiwa katika hali ya sala na tafakari. Pia iwe msaada kwa watunzi wanaochipukia ili wajifunze mema yaliyofanywa na watunzi waliopita.
Kutokana na hitaji hilo, Kurugenzi ya Mawasiliano katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) limeanza mchakato wa kuzikusanya nyimbo hizo za zamani zenye mafundisho, kisha kuzirekodi katika mfumo wa DVD ambapo waamini wataweza kujipatia kwa urahisi pale wanapohitaji.
 Na kwa kuanza, Kurugenzi hiyo imeandaa mkusanyiko wa nyimbo za zamani za Mama Bikira Maria, katika DVD iliyoimbwa na Kwaya ya Vijana ya Mtakatifu Cesilia, Parokia ya Mtakatifu Antony Maria Claret, Michungwani-Kimara, Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam. Albamu hiyo yenye mkusanyiko wa nyimbo 10 inayoitwa NIONGOZE MAMA WA YESU inazinduliwa Jumapili ya 33 A, yaani Novemba 19, 2017 ambapo waamini wote nchini wataweza kuipata kwa urahisi na kuenzi tunu za muziki mtakatifu.

Zoezi la ukusanyaji wa nyimbo za zamani ni endelevu. Kurugenzi, ikishauriana na wadau wa muziki mtakatifu, wanaliturujia na wote wenye mapenzi mema, itaendelea kuzikusanya nyimbo za vipindi mbalimbali vya Kanisa, kisha kuzirekodi kwa ruhusa maalum, ili kukabiliana na changamoto ya kupotea kwa nyimbo zile zilizopendwa, ambazo kwa sasa hazipewi kipaumbele katika maadhimisho mbalimbali.
Hii ni fursa kwa waamini na wadau wote wa muziki mtakatifu, kujipatia albamu hiyo kisha kuitazama na kutafakari zawadi ya Mama Bikira Maria katika maisha yetu ya kikristo hasa katika familia zetu.
Kwaya ya Vijana ya Mtakatifu Cesilia Michungwani, licha ya kuundwa na vijana, imekuwa ikijitahidi kuenzi nyimbo za zamani katika maadhimisho ya Misa Takatifu, hali inayowafanya waamini wajisikie kuwa sehemu ya Misa kwani inawawezesha kushiriki kikamilifu kuziimba nyimbo hizo.   Hii ni moja ya sababu iliyofanya ichaguliwe kushiriki katika kurekodi albamu hiyo, huku sababu nyingine ikiwa ni namna wanavyofuata maelekezo ya Liturujia katika Misa.
Haya ni miongoni mwa matunda ya uongozi thabiti, ushirikiano na hamasa ya Paroko wa Parokia ya Mt. Antony Maria Claret, Padri Wolfgang Silayo CMF, ambaye amekuwa daima mdau na mfuatiliaji wa nyimbo za zamani zinazoimbika kwa urahisi na waamini wote, zinazomuingiza muumini katika tafakari ya kina, huku maneno yake yakiwa ni mafundisho tosha.
Uzinduzi wa albamu hii ndiyo mwanzo wa kuendeleza jitihada za wadau wa muziki mtakatifu nchini, za kuhifadhi vizuri matini na rekodi za muziki mtakatifu zilizofanywa na watangulizi wa muziki huo.

Kwa wauzaji wa jumla na reja reja, au kama unataka kuwa wakala majimboni, piga 0657835343


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU