CARITAS MBEYA YAWAWEZESHA MABINTI WALIOTELEKEZWA


WITO umetolewa kwa wazazi na jamii  kwa ujumla kuwatia moyo na kuwapatia  stadi za maisha  ikiwemo elimu ya ujasiriamali wasichana wadogo wanaopewa ujauzito na kutelekezwa  badala ya kuwaacha wakikata tamaa ya maisha.

Ushauri huo umetolewa  na mfuatiliaji wa vikundi vya mabinti walea pekee kutoka Idara ya  CARITAS na Maendeleo, Jimbo Katoliki Mbeya anayeshughulikia maeneo ya Jiji la Mbeya, Magdallena Mwashala  alipokuwa akizungumza na KIONGOZI  mara baada ya kumtembelea mmoja wa mabinti walea pekee kujua maendeleo yake katika maeneo ya Tambukareli, Kata ya Itezi jijini Mbeya.
Magdallena  amesema kuwa msichana Jane Ndangali  ni miongoni mwa wanakikundi cha Amka ambaye  alijikuta amejiingiza katika mahusiano na kuzalishwa watoto wawili  na baadaye kutelekezwa na mwenzi wake, lakini  baada ya kuhamasishwa kujiunga katika kikundi amefanikiwa kupewa mafunzo mbalimbali ya ujasiriamali, utunzaji wa fedha, kuishi katika maadili mema, kujua haki zake na za mtoto pamoja na stadi za maisha.
Amesema  baada ya kupatiwa mafunzo msichana huyo amekuwa miongoni mwa wanakikundi cha Amka  walioweza kupata mafanikio makubwa yakiwemo ya kutunza familia yake bila kumtegemea mtu yeyote.
"Unaweza kukata tamaa ya kuishi baada ya kuona kila kukicha ni matatizo na vifo vinaendelea kuisonga  familia yenu  na hatimaye  ukajikuta unatumbukia  katika mikono unayodhani ni ya watu salama  na  wasamaria wema kumbe la hasha, unajiingiza katika matatizo zaidi lakini jamii inapaswa kukusaidia kwa kuwa jirani nawe na kukushauri na hata kukusaidia kwa hali na mali na ndivyo Caritas tunavyofanya katika kuisaidia jamii," amesema Magdallena.
Ameongeza,"vijana wanapojikuta wameingia katika matatizo na makundi yasiyofaa hawapaswi kutelekezwa bali kuwasogelea, kukaa na kuzungumza nao na  wanaweza kubadilika kuwa vijana wema na wa mfano wa kuigwa katika jamii."
"Ndivyo ilivyomtokea Jane Ndangali msichana mwenye umri wa miaka 26 baada ya kutelekezwa, kwa sasa anailea vyema familia yake  kwa kufanya bishara za viazi mviringo na kufyatua matofari, anapanga tanuru yeye mwenyewe  na kuchoma  na kuuza na amejenga nyumba yake ya kuishi na familia yake," amefafanua Magdallena.
Akizungumza na Kiongozi, msichana huyo ameishukuru Idara ya Caritas na Maendeleo Jimbo Katoliki Mbeya kwa kumfuata  na kumshawishi kujiunga katika kikundi na baadaye kupatiwa mafunzo yaliyomsaidia kufikia hatua aliyopo.
Hata hivyo Jane ametoa ushauri kwa wasichana wenzake kuwa wanapokumbwa na matatizo wasijifiche na badala yake watafute ushauri kwa  watu mbalimbali ikiwemo kujiunga katika vikundi  hali inayowasaidia  badala ya kujitenga na matokeo yake wanaweza kuathirika zaidi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa kikundi cha  mabinti walea pekee cha Tupendane kilichopo Mtaa wa Gombe Kaskazini, Kata ya Uyole, jijini Mbeya, Happy John  amempongeza msichana  mwenzao kwa hatua  aliyoifikia na kwamba wao wanatamani kufikia hatua hiyo.
"Na sisi katika kikundi chetu tunafyatua matofari, tupanga tanuru, kuchoma  na kuuza matofari pamoja na kutengeneza nguo aina ya batiki, lakini tunawashauri  wasichana wenzetu waache kukata tamaa na maisha. Pia jamii isipende kuwatenga  vijana wanaowaona wanapotea na badala yake wajenge utamaduni wa kuwasogelea na kuzungumza nao  ikiwemo kuwatia moyo," amesema.

 Na Thompson Mpanji, Mbeya

Msichana mlea pekee Jane Ndangali (wa tatu kutoka kushoto) katika picha ya pamoja na mfuatiliaji wa vikundi cha walea pekee kutoka Idara ya  CARITAS na Maendeleo, Jimbo Katoliki Mbeya anayeshughulikia maeneo ya Jiji la Mbeya, Magdallena Mwashala(wa kwanza kushoto) baada ya kumtembelea kujua maendeleo yake katika maeneo ya Tambukareli, Kata ya Itezi jijini Mbeya.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU