Ndoa zaidi ya 200 zafungwa Parokiani Mwambani Mbeya

Na Thompson Mpanji na Martha Mwalugala, Songwe

PAROKIA ya Mwambani katika Jimbo Katoliki Mbeya imefanikiwa kutoa Sakramenti Takatifu ya Ndoa kwa wanandoa 222 kwa muda wa mwezi mmoja na siku nane hali iliyotoa hamasa kwa waamini jimboni humo kushiriki Sakramenti hiyo.
Tukio hilo la kipekee limetokea katika Kanisa la Mtakatifu Karoli Lwanga Parokia ya Mwambani Jimbo Katoliki Mbeya katika wilaya ya  Songwe mkoani Songwe ambapo wanandoa  vijana kwa wazee wameamua kuuaga ukapera mbele ya maelfu ya wakazi  wa wilaya hiyo.
Akizungumza katika sherehe ya ndoa hizo iliyobebwa na kauli mbiu “kama kweli unanipenda tufunge ndoa! Tufunge ndoa kama unanipenda”, paroko wa Parokia ya Mwambani padri Laulian Mwambala amewapongeza waamini   walioitikia wito huo na kufanya maamuzi ya kuishi kikristo kwa mujibu wa sheria na taratibu za Kanisa.
Padri Mwambala amesema zoezi zima limehusisha ndoa  222 lakini kutokana na uhitaji na maombi ya baadhi ya Makatekista kuomba  ndoa nyingine  zikafanyikie katika vigango wamelazimika kuanza kufungisha  ndoa 152 kwa siku moja.
Amesema ndoa nyingine zimetafutiwa kufungwa katika Vigango vya Parokia hiyo na kufafanua kuwa Oktoba 25 zimefungwa ndoa 49 katika Kigango cha Mbala, Oktoba 28 imefungwa ndoa moja katika Kigango cha  Mkwajuni, Oktoba 29 zimefungwa ndoa 9 katika Kigango cha Saza, Novemba 4 imefungwa ndoa moja katika Kigango cha Mkwajuni na Mwambani ndoa moja, Novemba 5 zimefungwa ndoa saba katika Kigango cha Maleza, Novemba 11 imefungwa ndoa moja katika Kigango cha Mkwajuni na ndoa moja imefungwa Novemba 12 katika Kigango cha Mbangala na hivyo kufikisha idadi ya ndoa 222 ambazo tayari zimefungwa tangu Oktoba 22 hadi Novemba 12,2017. 
Paroko huyo amefafanua kuwa kadiri ya ratiba bado ndoa nne katika kigango cha Kalanda zitakazofungwa Novemba,19 na ndoa mbili katika Kigango cha Mkwajuni zinazotarajiwa kufungwa Novemba 25,2017 na hivyo kufikisha idadi ya Ndoa 228 kufungwa kwa muda wa miezi miwili tukio ambalo halijawahi kutokea katika historia tangu kuanzishwa kwa Parokia ya Mwambani.
Amebainisha kuwa siri ya kufikia  mafanikio hayo ni baada ya kutembelea familia na kubaini kuwa  watu walio wengi  wanaishi  bila kufunga ndoa  kutokana na kuhofia gharama za kufanya sherehe.
“Jamii nyingi hutumia gharama kubwa  kwa ajili ya maandalizi ya sherehe za Ndoa jambo ambalo ni la kidunia, watu wengi hawaelewi muunganiko kati ya Sakramenti ya ndoa na sherehe, wale  wote walioamua kufunga ndoa wamefungua ukurasa mpya katika maisha yao,” amesema padri Mwambala.
Aidha  padri Mwambala amefafanua kuwa ndoa yenye mke  na mume mwema inaleta afya njema kwa  kila  mwanandoa na watoto hivyo wanapaswa kuepuka maneno makali, chuki na ugomvi ambayo ni sumu  na chanzo  cha kutenganisha familia na matokeo ya malezi mabaya kwa familia.
“Upendo wa kweli ndio mzizi wa kila kitu,  ndoa siyo tamasha  la masikitiko bali ni tamasha  la  furaha ,wanandoa mnayo majukumu ya kuifanya ndoa kuwa chanzo cha furaha na amani siku zote na siyo kuifanya iwe kama kiwanda  cha  kutengenezea sumu, watoto wafurahie kuwepo kwa  baba  na  mama  wenye kuishi ndoa kwa malezi mazuri yanayotawaliwa na amani ya kweli,” amewaasa.
Ameongeza, “kwa wote mlioamua kufunga ndoa leo, mabadiliko yaanze leo katika kuonesha matendo mazuri kwa kuitana majina mazuri na maneno matamu matamu kila wakati  kama  baby, honey, laazizi wangu, jembe  langu, na kila mara ifanyeni ndoa yenu kuwa mpya.”
Ameelezea pia kuwa manufaa  ya kuishi viapo na kauli nzuri katika ndoa ndiyo siri kubwa kupata viongozi wazuri  katika Kanisa  na jamii kwa ujumla na kwamba shahada ya ndoa ni msaada mkubwa katika kudai haki  na hasa mirathi baada ya mwanandoa mmoja kufariki.
“Kupitia tendo hili takatifu, ninawaalika wale wanaoishi uchumba sugu wabadilike na kutambua umuhimu wa ndoa  na hasa katika dunia ya sasa ambayo inakumbana na changamoto nyingi.”
Hata hivyo KIONGOZI  limezungumza  na baadhi ya waamini waliofunga ndoa siku hiyo kwa nyakati tofauti ambapo Deogratias Ganji na Gregoli Pesambili wameelezea furaha yao na kwamba wamejiona wameuvaa utu mpya na kuuacha wa zamani  ambao ulikuwa wa kuwanyanyasa, kuwatesa na kuwapiga hovyo wenzi wao.
“Lakini leo tumekuwa ni kama tumeanza upya na kupitia baraka tulizopata na ujumbe tuliopewa tunajiona tumekuwa wapya kabisa na tunazifurahia ndoa zetu tofauti na hali ilivyo kuwa awali na tunajiona tulikuwa  wakosefu  kwa  wake zetu lakini tumeungama  na kuwaomba  wasamehe yale yote tuliyokuwa tunawakosea awali  tufungue ukurasa mpya wa baba  na mama mwema,”walisema kwa furaha  wanandoa hao kwa nyakati tofauti.
Hata hivyo wamewashukuru pamoja na kuwapongeza mapadri kwa juhudi zao bila kukata tamaa kwa kuwatembelea mara kwa mara licha ya kukutana na changamoto za hapa na pale hadi kufanikisha zoezi hilo muhimu katika maisha yao. Wameahidi kuwa mabalozi na walimu kwa wengine  ambao bado hawapo tayari kufunga ndoa.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU