KARDINALI PENGO AZINDUA PAROKIA MPYA MISUGUSUGU.





ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewaongoza waamini wa Misugusugu na wageni waalikwa kutoka parokia tofauti za Jimbo hilo kwenye sherehe za kuzindua parokia mpya ya Mt. Polycarp Misugusugu, sanjari na uzinduzi wa nyumba ya mapadri iliyojengwa parokiani hapo pia usimikaji wa msalaba wa kumbukumbu juu ya kilima kilichopo pembezoni mwa parokia hiyo.
Katika mahubiri yake kwenye ibada hiyo ya misa takatifu, Kardinali Pengo amesema kuwa kwa kiburi cha Adam na Eva maisha yetu yametuwia magumu lakini bado Mungu anatupenda kwa upendo wake mkuu kwetu, akamtuma  mwanaye Yesu Kristo aje kutukomboa kupitia kwa mama yetu Bikira Maria aliyekuwa mtii na mnyenyekevu mbele za Mungu, hivyo kila mkristo adumu katika upendo kila wakati.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa  Parokia hiyo mpya, Adolf Mrema amesema, ‘Ni furaha iliyopitiliza kwa hatua tuliyoifikia kwa sababu tutakuwa na uhakika wa kufanya adhimisho la Ekaristi Takatifu ambayo ndiyo nguvu yetu, kwani bila Ekaristi hatuwezi kufanya chochote.’’
Aidha Mwenyekiti huyo wakati wa kusoma historia kwa Mwadhama Kardinali Pengo amesema ukatoliki katika eneo la Misugusugu ulianza na familia tano mwaka 1971 zikiongozwa na marehemu Mzee Nemes Daud Luzua aliyehamia katika kijiji cha Misugusugu akitokea Matombo Morogoro. Mzee Nemes  aliungana  na familia za marehemu Mzee Athanas Masenga aliyehamia toka parokia ya Lugoba, pamoja na familia za marehemu Mzee Arbogast Matembele, Amandus Mponda na Gustav Mtumbuka aliyehamia Misugusugu akitokea Kipatimu. Familia zote hizi tano zilikuwa zikikutana  nyumbani  kwa Mzee Nemes kwa sala chini ya mti wa mkorosho tangu  mwaka 1971 na wakati huo hapakuwa na kigango wala Jumuiya na waamini wengi katika familia hizi hawakuwa wamebatizwa wala kufunga ndoa.
Misugusugu ilitangazwa kuwa kigango mwaka 1980 chini ya parokia ya Tumbi/Kibaha, na sasa ni parokia rasmi na vigango vya Zogowale, Ngeta na Makazi mapya vimewekwa chini ya parokia hii na idadi ya Kanda ni mbili ikijumuisha jumuiya 22.
Parokia ya Mt. Polycarp inaongozwa na Paroko Joseph Kazikunema, ambapo kwa mujibu wa taarifa, uzinduzi wa Parokia hiyo umeleta neema kubwa ikiwemo watoto 130 kubatizwa, ndoa 27 kubarikiwa na Mapadri kutembea nyumba kwa nyumba kuwafahamu waamini na kuamsha uhai wa imani.
Uzinduzi huo pia ulihudhuriwa na kwaya mashuhuri ya Mwenyeheri  Anwarite toka parokia ya Makuburi, huku Mwadhama akizindua DVD mpya ya kwaya ya Mt. Polycarp Misugusugu waliyo itoa hivi karibuni.

Na Philipo Josephat, DSM

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU