ASK.KILAINI:VURUGU SI SULUHU.



ASKOFU Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini ametoa wito kwa watanzania kutojihusisha na vurugu na vita visiwani Zanzibar, huku akiwaonya wanasiasa kutowashinikiza wananchi katika kufanya maamuzi.
Ameeleza hayo hivi karibuni na kuonyesha kusikitishwa na vitendo vinavyoashiria uvunjifu wa amani Zanzibar, ikiwa ni pamoja na matukio ya milipuko ya mabomu na uchomaji wa nyumba na ofisi.
“Tunapiga magoti mbele ya Mungu kuomba amani na hata mara moja haiwezekani kukubaliana na vitendo vinavyoashiria uvunjifu wa amani. Tunasikitika na hatukutarajia kuona matukio kama hayo yakitokea nchini mwetu, ambacho ni kisiwa cha amani Sisi kama viongozi wa dini hatuingilii siasa ila tuna wajibu wa kushauri juu ya mwenendo wan chi.” ameeleza Askofu Kilaini.
Askofu Kilaini pia amewataka wananchi kutokubali kutumiwa na wanasiasa katika kufanya vurugu, na kusisitiza kuwa hakuna nchi yoyote duniani inayopata suluhu kwa kufanya vurugu, na badala yake amewaomba wadumu katika amani na maelewano kwa kuwa hatma ya nchi yao ipo mikononi mwa wananchi wenyewe.
“Tunaomba amani itawale huko Zanzibar, na inapotokea tofauti basi watafute namna ya kwenda bila kuleta vurugu. Vurugu na vita siyo suluhisho katika kutatua migogoro, hivyo katika kutoelewana ni lazima wafike mahali watafute suluhu kwa amani. Watambue kuwa wote ni ndugu, wakianza mafarakano hakuna atakayepona” amebainisha Askofu Kilaini.
Aidha amewataka wananchi wote kuwa wazalendo na mabalozi wa amani na kuwaomba wapinge hali ya vurugu inayohatarisha usalama na utulivu nchini, kwa kuwa wao ndiyo wahanga wakubwa wa ukosefu wa amani. Ameleza kuwa ni jambo la busara kujifunza kupitia katika nchi ambazo zilijiingiza katika vurugu kama njia ya kutafuta suluhu na badala yake zikaingia kwenye machafuko yasiyokwisha.
“Vitendo vya milipuko ya mabomu ni dalili za ugaidi, hivyo basi kila mtanzania anapaswa kupinga aina yoyote ya vurugu. Tutafute suluhu kwa amani, vurugu haiwezi kuleta amani. Hakuna nchi yoyote duniani iliyopata suluhu kwa vurugu. Tujifunze kwa nchi ambazozilijiingiza katika vurugu na mpaka leo hawajapata muafaka” ameongeza.
Pia amezitaka pande zozote zinazokinzana kutafuta suluhu na kudai haki kwa amani. Ameeleza kuwa vurugu ni kielelezo cha kupotea kwa utu, hivyo kila mmoja ana wajibu wa kulinda amani.
Hivi karibuni kumekuwa na matukio ya milipuko ya mabomu na uchomaji wa ofisi Zanzibar, ambapo nyumba anayoishi Kamishna wa Polisi Zanzibar, Hamdan Omar Makame iliopo Kijichi nje kidogo ya mji wa Unguja imeshambuliwa kwa kulipuliwa kwa bomu.

Paschal Mwanache,TEC 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU