Nchi za AMECEA zaaswa kujitathmini kama zimefikia madhumuni ya waasisi

n  Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam
Nchi wanachama wa Umoja wa Mabaraza ya maaskofu Afrika Mashariki na Kati (AMECEA) zimepewa changamoto ya kujitathmini kama zimefikia malengo ya umoja huo tangu miaka ya 1960-2018.
Hayo yameelezwa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa AMECEA Padri Dr. Ferdinand Lugonzo katika semina ya siku nne kwa wahasibu na wasimamizi wa miradi wa majimbo katoliki mbalimbali nchini, inayofanyika katika Kituo cha Kurasini-Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
Padri Lugonzo amesema kuwa, AMECEA ilizaliwa kwa lengo la kuwa na mbinu za pamoja  za kichungaji kwa maslahi ya watu wa kanda hiyo ya AMECEA.
Miongozo ya Mababa waanzilishi wa AMECEA ilikuwa kuimarisha na kuendelea katika nyanja mbalimbali kwa ajili ya kuimarisha Imani Katoliki na maendeleo ya jamii katika kanda hiyo.
 Pia lengo jingine lilikuwa ni kuwa na Mpango Mkakati  wa muda mrefu  uliowekwa katika Mkutano  Mkuu wa AMECEA (Plenary) uliofanyika Julai 1961 Msimbazi, Dar es Salaam ukiwa na  dhamira kuu ya  “Kesho ya Kanisa la Afrika.”
 “Katika mkutano huo mkuu (1961) palikuwa na ajenda saba ambazo ninapenda leo mzipitie muone kama mwaka huu 2018 tumefikia wapi kama TEC na kama majimbo ya Tanzania na parokia zenu.
Ajenda ya kwanza ilikuwa Kanisa na Vyombo vya habari: Uanzishwaji wa vituo vya televisheni, radio na uchapishaji wa magazeti. Je, Tanzania imefikia wapi na inatumiaje hivi vyombo kufikisha lengo msingi la AMECEA? Je, hali ya mada hii katika nchi wanachama wa AMECEA imefika wapi?
Ajenda ya pili ilikuwa, Mafunzo ya Kiroho kwa Mapadri wa majimbo, ya tatu  Mahitaji ya Kituo cha uchungaji  na  malezi endelevu, . 
Ajenda ya nne ilikuwa ni  uwezekano wa kuwa na Chuo Kikuu cha AMECEA au angalau Chuo Kikuu kishiriki. Ya tano ni  kuwa na Programu ya Kujitegemea .
Agenda ya sita ilikuwa  Muelekeo wa  Shule za Kikatoliki na Elimu  Katoliki (haja ya kuwa na silabasi ya dini ya kikristo) na ya saba ni Haki na Masuala ya Amani katika ukanda wa AMECEA.
Jukumu kubwa la AMECEA ni kuhamasisha na kuwezesha familia ya Mungu kuwa na moyo wa uinjilishaji na maendeleo mfungamano.
Kuwa manabii wa kumshuhudia Kristo katika ukanda wa AMECEA,  kuwa mashahidi na manabii  wa Kristo, kwa kukuza umoja, haki, amani .
Tufikiri na kutenda zaidi ya kile kilichopo kuanzia  ngazi ya Baraza yaani taifa, kushuka kwenye majimbo na parokia zetu na  kukabiliana na masuala pana ambayo yana  umuhimu  na kuligusa bara letu na Kanisa la kiulimwengu.
‘Tufikiri kiulimwengu tutende kiafrka kwa kuchukua mada za kiulimwengu na kuzifanyia kazi katika mazingira yetu kama vile nyaraka mbalimbali za Kanisa, masuala ya umoja wa mataifa nk,” amesisitiza Padri Lugonzo.
Amesisitiza mapadri, maaskofu na waamini kufanyia kazi masuala ya kimataifa yanayogusa ukanda wa AMECEA akitolea mfano wa majimbo mangapi, parokia, jumuiya ndogondogo na familia wanajua waraka wa ‘LAUDATI SI’ wa Papa Fransisko ambao ni waraka kuhusu Mazingira na mabadiliko tabia nchi.
Amesisitiza umuhimu wa kujua mada za kimataifa na mada za kiulimwengu kuanzia ngazi ya taifa, majimbo, parokia na familia ili kuzifanyia kazi katika mazingira ya kiafrika.
   Padri Lugonzo ametoa mada pia kuhusu utawala wa mali za Kanisa na rasilimali. 
Akisisitiza juu ya  uelewa wa jinsi Kanisa linavyofanya kazi kwa kuhusisha utume wa Kanisa, Ushirikiano, Miundo mbinu na Utawala.
“Lengo kuu la Kanisa ni kuinjilisha na kwa wale watawala wenye mamlaka wanapaswa kutoa ushirikiano na watendaji ili kufanikisha shughuli za Kanisa. Bila ushirikiano katika shughuli za maendeleo tutakwama mahali.
Katika kusimamia rasilimali za Kanisa na kupata maendeleo yenye tija lazima kutumia wataalamu kwa kuweka watu stahiki katika kazi stahiki awe mlei ama mkleri ilimradi awe na taaluma na uzoefu wa kazi ili tupate ufanisi,” amesisitiza Padri Lugonzo.
Ameziasa taasisi za Kanisa na idara zake kuwa na miongozo, kanuni na sera hasa kanuni za fedha, uchungaji nk. ili kuwe na utaratibu unaoeleweka kuanzia ngazi ya taifa, majimbo na parokia na waamini wajue na kuelewa kanuni hizo.
Amesema miongozo na kanuni hizo ziwe wazi  na siyo za  mtu mmoja. 
Amesema kuwa, Kanisa halifanyi kazi na mtu mmoja, hivyo katika kumiliki rasilimali lazima kuwe na sera ambayo si ya mtu binafsi bali ya taasisi ili kuepuka changamoto ya kufanya kazi kiholela na kukwama pale mtendaji anapoondoka.
Ametaka Baraza la Maaskofu ambalo linashikilia ngazi ya kitaifa kuwezesha ofisi za majimbo na vitengo vyake kuwa na miongozo stahiki inayoongoza idara zao na kuwa na wataalamu wa kuendesha shughuli za maendeleo.
“Tuwe na ushirikiano wa ofisi za taifa, majimbo na parokia ili kuwa na mifumo rasmi inayoongoza hususani kwenye fedha na umiliki rasilimali zote za Kanisa.
“Mfuate sera na miongozo ya nchi ili kukwepa matatizo. Makanisa yetu, shule, ardhi, hospitali nk. ziwe na vibali vya umiliki (umiliki wa halali) ili kukwepa changamoto za kunyang’anywa ardhi na huko ndiko kufanya kazi kwa kutumia taaluma,” amesisitiza.
Hata hivyo amesisitiza kuwa, katika nyanja zote za Kanisa, cheo ama kazi mtu anayopewa lazima atangulize moyo wa  kujitoa kufanya huduma na uinjilishaji kwasababu Kanisa Katoliki lipo kwa ajili ya huduma na uinjilishaji.
Viongozi pia wameaswa kuajiri watu sahihi katika kazi sahihi kulingana na taaluma na uwezo wao ili kuzuia kufanya kazi chini ya kiwango.
Yapo mengi ya kujitathmini yakiwemo maendeleo ya jumuiya ndogondogo ambayo ni uhai wa Kanisa, kupambana na umasikini na maradhi ukiwemo ugonjwa wa ukimwi , kuzifanya familia za kiafrika kuwa chombo za uinjilishaji nk.
Ikumbukwe kuwa nchi wanachama wa AMECEA ni Elitrea, Ethiopia, Tanzania, Uganda, Zambia, Sudani, Kenya, Uganda na Malawi.


Na Sarah Pelaji, Dar es salaam 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU