‘Imetosha kujenga makanisa sasa tuhudumie wagonjwa’

Kila jumuiya na Parokia viwe na mfuko wa wagonjwa


Na Pascal Mwanache, Singida

WITO umetolewa kwa waamini katika ngazi za jumuiya ndogo ndogo za Kikristo na Parokia kuwa na mfuko wa akiba kwa ajili ya wagonjwa, kwa kuwa hicho ndicho kipaumbele cha maisha ya mkristo ambapo kwa sasa mkazo umewekwa zaidi katika shughuli za ujenzi wa makanisa na miundombinu yake huku wakisahau kuweka akiba ya kujenga miili yao. 
Wito huo umetolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Singida Mhashamu Edward Mapunda wakati wa maadhimisho ya Siku ya 26 ya Wagonjwa Duniani ambayo kitaifa imefanyika katika Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu Puma, Singida. Askofu Mapunda amewataka waamini jimboni humo kuanza mara moja utaratibu wa kuwa na mfuko wa wagonjwa katika jumuiya na parokia na kuwa na mguso wa pekee katika kuwajali na kuwahudumia wagonjwa.
“Yesu alipambana na magonjwa yaliyowaangamiza watu kiroho na kimwili. Hiki kilikuwa kipaumbele cha Yesu na sasa ndicho kipaumbele cha Kanisa. Kwa njia za huduma ya afya na sakramenti mbalimbali za Kanisa watu wanaendelea kutakasika. Hicho kiwe pia kipaumbele cha jumuiya zetu yaani kuhudumiana kimwili na kiroho. Kwa namna hii wagonjwa watakuwa na matumaini ndani ya jumuiya na Parokia zetu” ameasa.
Aidha Askofu Mapunda amebainisha kuwa huduma za afya ni wito mtakatifu kwa kuwa muda unaotumika kuwahudumia wagonjwa ni muda uliotumika kitakatifu. Ameongeza kuwa kuhudumia wagonjwa ndiyo dini ya kweli na ibada kwa sababu anayehudumiwa ni Yesu mwenyewe. 
“Matendo ya huruma kwa wagonjwa ni ibada. Ni sehemu ya maisha ya kila siku, hivyo ni matendo endelevu. Familia, jumuiya ndogo ndogo za kikristo, parokia, jimbo na kanisa kwa ujumla lazima zijikite katika kuhudumia wagonjwa” ameeleza.
Katika hatua nyingine Askofu Mapunda ametoa wito kwa viongozi wa kiroho kuwahamasisha waamini kuwa na bima ya afya ili kukabiliana na changamoto za ukosefu wa huduma kwa wananchi wanaokosa fedha za matibabu pindi wanapougua.
“Nitafurahi kama jumuiya itahakikisha kwamba kila mwanajumuiya anakuwa na bima ya afya. Kila tunapoenda kusali tuulizane kama kila mmoja wetu ana bima ya afya, kama tunavyoulizana iwapo tumebeba Biblia na rozali” ameongeza.

Mkuu wa Mkoa wa Singida aliomba Kanisa
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi ameliomba Kanisa Katoliki Jimbo la Singida lifikirie kuwa na kiwanda cha kutengeneza maji ya dripu ikiwezekana ndani ya mwaka huu, akisema kuwa Bikira Maria ana makusudi ndani ya Singida kuwe na huduma pekee kwa ajili ya manufaa ya wananchi wote.
Pia amewaomba viongozi hao wa dini kuomba ili taifa liondokane na wagonjwa wasababishi wa magonjwa kama vile ubinafsi, rushwa, uvivu, wizi, uzembe kukosa uaminifu na uadilifu.
“Yasipoondoka haya tutafungua hospitali nyingi. Mtu anayeendekeza rushwa kwa mfano, atachelewesha haki, atapindisha sheria na kusababisha watu kuugua” ameeleza.
Aidha Dkt. Nchimbi amekiri kuwa Kanisa ni mkono wa serikali katika utoaji huduma za afya kwa kuwa wadau wakubwa wa utendaji wa serikali, huku wakitenda kiaminifu na hata kuwa darasa kwa wengine. Ametoa wito kwa wahudumu wa afya katika hospitali za serikali mkoani humo kuwapa ruhusa wagonjwa wanaohitaji huduma za CT Scan ili wakazipate katika Hospitali ya Mt. Gaspar iliyoko Itigi.
“Nataka niwaeleze kuwa mkoa wa Singida katika Hospitali ya Mtakatifu Gaspar Itigi kuna huduma ya CT Scan nzuri, bora na ya kiwango cha kimataifa ambayo hatujaitumia vizuri. Hospitali za serikali msiwacheleweshe wanaohitaji huduma ya CT Scan. Tukiri tu kuwa tumetindikiwa, kwa hiyo elekezeni mara moja mtu akapatehuduma pale Mt. Gaspar Itigi. Hapa Puma pia kuna huduma nzuri za tiba ya mifupa. Kuna madaktari bingwa kutoka Ujerumani, tutumie fursa hii bila kuchelewa” ameongeza.

Dkt Nchimbi agawa Rozari 700 kwa wagonjwa
Katika kuadhimisha siku hiyo ya wagonjwa waamini waliohudhuria walipata fursa ya kuwatembelea wagonjwa waliolazwa katika Hospitali ya Malkia wa ulimwengu Puma na kuwafariji kwa zawadi na sala zao, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi alikuwa kivutio kwa wagonjwa hao na waamini.
Kama ilivyo ada yake kila alipowasalimu wagonjwa, aliwahoji iwapo ni wakristo na iwapo wanahitaji rozari, na pindi wanapokubali basi yeye mwenyewe huwavalisha rozari hizo pamoja na kuwapatia zawadi nyingine.

Vyombo vya habari vya Kanisa vyatajwa kuwa faraja ya wagonjwa
Kiongozi lilifanya mahojiano na baadhi ya wagonjwa ambapo wengi wamekiri kuwa vyombo vya habari vya Kanisa Katoliki vimekuwa faraja kwao hasa katika kufuatilia yanayojiri ndani ya Kanisa, kufuatilia Misa Takatifu na kusoma tafakari.
“Ndiyo ninasoma gazeti la Kiongozi hasa tafakari za kila jumapili, na hata ninaposhindwa kwenda kanisani nafarijika kusikiliza Redio Maria” anaeleza Lukas Mbingu aliyelezwa hospitalini hapo. 

Kutoka chumba cha habari
Ili kuwafikia na kuwainjilisha wagonjwa na wenye uhitaji zaidi vyombo vya habari vya kanisa vinategemea uwezeshwaji na uungwaji mkono wa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kama ilivyofanya Kurugenzi ya Uchumi Endelevu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) ambayo imehakikisha gazeti la kiongozi linawahabarisha waamini juu ya maadhimisho na matukio ya siku ya wagonjwa 2018.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU