NCHI YETU BADO INAHITAJI NGUVU ZA KUJENGA UCHUMI-ASK. NGALALEKUMTWA

n  Na Getrude Madembwe, Iringa.
ASKOFU wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amesema kwamba bado nguvu inahitajika katika kuimarisha uchumi wa wananchi.
Askofu Ngalalekumtwa amezungumza hayo hivi karibuni wakati wa ziara ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu alipotembelea wilaya ya Mafindi  kugagua miradi mbalimbali wilayani humo.
“Uchumi wetu bado una shida sana nakaa na watu maeneo mengi nazunguka hasa vijijini unaona jinsi watu wanavyohangaika kufanya shughuli ili waweze kuwasomesha watoto wao.
Suala la muhimu wataalamu wa masuala ya kilimo na mifugo watoe elimu ili kipato cha mwananchi kiongezeke,” amesema Askofu Ngalalekumtwa.
Aidha akizungumzia ujumbe wa kwaresma 2018 uliotolewa na  Maaskofu Katoliki Tanzania, Mhashamu Ngalalekumtwa amesema ni kawaida kwa maaskofu hao kutoa ujumbe huo kila mwaka.
“Kila mwaka tunapenda watu wajue sisi viongozi wao wa kiroho tunakazia mambo gani. Huwa tunasisitiza masuala yanayolenga kujenga haki, upendo na umoja na haya yakiwepo ndipo maendeleo ya kweli yatapatikana,” amesema Askofu Ngalalekumtwa. 
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya  Mufindi Jamhuri David amesema kwamba kwamba katika halmashauri yake ukusanyaji wa mapato unaongezeka mwaka hadi mwaka ambapo mwaka 2017 hadi Januari 2018 halamshauri hiyo imekusanya bilioni 7.900 ikiwa ni asilimia 78% ya malengo na jitihada walizojipangia.
Bw. David amesema kwamba mwaka 2015 hadi 2016 halmashauri hiyo imekusanya bilioni 11.700 na mwaka 2016 -2017 wamekusanya bilioni 13.8 sawa na ongezeko la asilimia 22%.
“ Halmashauri yetu inatoa  mchango mkubwa katika ukusanyaji wa kodi tukishirikiana na mamlaka ya ukusanyaji wa mapato (TRA) na mapato yetu yanaongezeka kila mwaka, ni jitihada  za serikali ukusanyaji wa mapato kutoka sekta  mbalimbali kama vile viwanda na mazao ya misitu,” amesema Bw. David.
Makamu wa Rais Suluhu ameipongeza halmashauri hiyo kwa ukusanyaji mzuri wa mapato, wazalishaji wa chakula na ameahidi kuwa pembejeo za kilimo zitapatikana kwa wakati na bei rahisi.
 Aidha Bw. David amesema kuwa vyanzo vya ndani ukusanyaji wa mapato pia umeongezeka kwani mwaka 2015 -2016 wamekusanya bilioni 4.396, mwaka 2016 – 2017 wamekusanya bilioni 4.882 na mwaka 2017 hadi Januari 2018 halmashauri imekusanya bilioni 2.289.
 Mkuu huyo wa wilaya ya Mufindi amesema kuwa halmashauri yake imejiwekea mikakati  mbalimbali katika ukusanyaji wa kodi na wameimarisha vizuizi vya maliasili, wameziba mianya ya rushwa, pia halmashauri hiyo ina asilimia 70% ya viwanda vinavyosaidia kuongeza mapato.
 Akizungumzia mradi wa ujenzi wa jengo la ghorofa ambalo litakuwa na maabara 3 za sayansi, chumba kimoja cha kompyuta na vyumba vya 5 madarasa mkondo wa kidato cha 5 na 6 katika shule ya sekondari ya Mgololo iliyopo wilayani humo, mkurugenzi wa Halamashauri ya Mufindi Profesa Riziki Shemdoe amesema kwamba mradi huo hadi ukamilike utagharimu Tsh. Milioni 450 na umefadhiliwa na kiwanda cha Karatasi Mufindi (Mufindi Paper Milling MPM).
 “Mradi huu unafadhiliwa  na kiwanda cha karatasi Mufindi na ulianza rasmi mwaka 2016 tunatarajia utakamilika ifikapo Aprili 2018 na utagharimu kiasi cha Tsh.Milioni 450, hadi sasa tumetumia Tshs. Milioni 325” amesema Profesa Shemdoe.
 Katika ziara yake Makamu wa Rais amefungua zahanati ya Kising’a iliyopo katika halmashauri ya Iringa ambayo imejengwa kwa nguvu za wananchi wakishirikiana na Asasi group Company waliochangia Milioni 125. 
Katika Wilaya ya Kilolo Mama Samia amesema serikali itajenga barabara ya kiwango cha lami yenye urefu wa Km. 35 iliyopo wilayani humo, pia amefungua jengo la Utawala na madarasa 3 yaliyojengwa na halmashauri hiyo na nguvu za wananchi wa  maeneo hayo.
 Akitoa majuisho kwenye ukumbi wa siasa ni Kilimo uliopo katika halmashauri ya Iringa, Makamu wa Rais Suluhu amesema kwamba amefurahiswa na utunzwaji wa mazingira katika baadhi ya maeneo ya mkoa wa Iringa na ametahadharisha kwamba kama watu wataendelea kukata miti hovyo bila kupanda huenda hali ya hewa iliyopo itatoweka siku zijazo.
 “Maeneo ya Mkoa huu yana sura 2, sura ya kwanza mmetunza mazingira vizuri na sura ya pili inaonyesha kuna uharibifu wa vyanzo vya maji kuna maumbile ya mabonde na milima, ongezeko la watu linakua , watu wakae lakini wasifanye shughuli zozote kwenye vyanzo vya maji” amesema Makamu wa Rais na kuongeza kuwa
 “ Iringa ya miaka 10 hadi 15 iliyopita si kama ya sasa, joto laanza, kateni miti na mpande miti, msiharibu pia vyanzo vya maji, sharia ile watu wakae mita 60 kutoka vyanzo vya  maji ifuatwe, msiharibu kiharibu mnakumfuru Mungu”.
 Ameutaka mkoa kuwa  na mkakati katika suala la kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI, ina asilimia 11% kitaifa Mkoa wa Iringa unashika nafasi ya pili.
Makamu wa Rais amekuwa na ziara ya siku 5 mkoani Iringa na amefungua miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo mkoani humo.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU