Kanisa liwe mfano wa kuigwa kufuata sheria za kodi-Katibu Mkuu TEC


IMEELEZWA kuwa Kanisa Katoliki nchini linapaswa kuonyesha mfano katika kufuata taratibu zote za kodi kwa kuwa sheria za kodi zinazosimamiwa nchini zilikuwepo kwa muda mrefu ila zilikuwa hazisimamiwi na kufuatiliwa.
Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri Raymond Saba wakati akifungua semina ya siku nne kwa wahasibu na wasimamizi wa miradi wa majimbo katoliki mbalimbali nchini, inayofanyika katika Kituo cha Kurasini-Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
Semina hiyo inayolenga kuwajengea uwezo wa usimamizi wa fedha na miradi washiriki hao imeandaliwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki (AMECEA) kwa kushirikiana na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
Padri Saba amesema kuwa majimbo hayana budi kufuata utaratibu wa kujisajili, kuhakiki mahesabu, na kuongeza kuwa uhakiki huo ni lazima uanze katika ngazi za parokia.
“Kama Kanisa tunapaswa kuwa mstari wa mbele kufuata sheria za kodi za nchi. Sheria na taratibu hizi siyo ngeni, zilikuwepo katika nchi yetu ila zilikuwa hazisimamiwi vizuri na kufuatiliwa” ameeleza Padri Saba
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa AMECEA Padri Chrisantus Ndaga amewaambia wahasibu hao kuwa semina hiyo inapaswa iwajengee uwezo utakaosaidia taasisi mbalimbali zilizoko majimboni na kugusa ngazi ya chini katika parokia.
“Semina hii iwasaidie na ninyi mkaandae semina kama hizi huko majimboni. Tukumbuke kuwa mambo haya ya fedha na miradi yanagusa taasisi ambazo majimboni kwetu ziko nyingi. Kwa hiyo sisi tunalo jukumu la kufikisha ujuzi huu katika ngazi ya chini kabisa, ikiwezekana hata katika jumuiya ndogo ndogo” amesema Padri Ndaga.


Na Pascal Mwanache, Dar es salaam

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU