Mama ajifungua watoto watano, wote wafariki

n Na Doreen Aloyce, Katavi 
Hivi karibuni mama mmoja kwa jina la Spora Yohana (30) Mkazi wa kijiji cha Wachawaseme kata ya Utende Wilaya ya Mlele Mkoani Katavi amejifungua watoto watano ambao wote wamefariki dunia baada ya kukosa msaada wa wataalamu wa Afya.
Akizungumza na gazeti hili Spora (mama wa watoto hao) amesema kuwa, 
alijifungua watoto watano wa kiume watatu na wawili wa kike kabla ya wakati maana amejifungua wakiwa na miezi nane badala ya tisa.
“Nilijifungulia nyumbani majira ya saa kumi na moja asubuhi nilipoanza kusikia maumivu makali na hatimaye kuanza kujifungua mmoja baada ya mwingine na mpaka kufikia saa mbili nilimaliza na kujiandaa kupelekwa kwenye Zahanati.
Sikuenda hospitalini mapema kutokana na kwamba sikutarajia kujifungua  kwani muda wake ulikuwa bado hivyo alidhani ni maumivu ya kawaida ambayo nimekuwa nikiyapata siku zote kutokana na tumbo langu kuwa kubwa.
Baada ya kujifungua, watoto wangu wakaugua wote kwa pamoja na kupoteza maisha tukiwa kwenye jitihada za kuwakimbiza hospitalini,” amesema Spora.
Akizungumza kwa unyonge Spora kuhusiana na tukio hilo amesema kwamba amesikitishwa na tukio hilo kwa jinsi alivyohangaika kubeba mimba iliyosababisha tumbo kuwa kubwa kuliko kawaida ijapokuwa alikuwa akifurahia kuhisi watoto wake wakicheza ingawa alikuwa hafahamu kuwa amebeba watoto watano.
“Nimebeba mimba ya watoto watano, nimejifungua watoto watano. Ingawa wamefariki mimi ni mama wa watoto watano hivyo siko tayari kubeba ujauzito tena. Nawaombea tu kwa Mungu watoto wangu wapumzike kwa amani,” amesema Spora.
Mganga Mkuu wa Zahanati  hiyo Daktari Lucia Kafumu ameeleza kuwa mama huyo walimpokea majira ya saa nne asubuhi akiwa amejifungua watoto wake ambao walipoteza maisha kabla ya kufika hospitali na kupatiwa huduma ya afya.
Amesema kuwa kutokana na miezi ya watoto hao kama wangepatiwa huduma wakiwa kwenye zahanati wangeweza kuokoa maisha yao huku akisema changamoto kubwa ni elimu kwa wananchi kwani bado wana mila potofu za kuwaamini waganga wa kienyeji na wakunga jambo ambalo linasababisha vifo kwa akina mama wengi.
Amewataka wananchi hususani wajawazito kuwa na kasumba ya kufika kwenye zahanati kwa ajili ya kupata huduma stahiki za afya na kupunguza vifo vya mama na mtoto.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU